MHE. ASHA OMAR RASHID: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, ninashukuru kwa kunipatia fursa hii nami kuuliza swali langu la nyongeza. Pale Mkoani kwangu Kaskazini Pemba pana Kituo cha Polisi cha muda mrefu. Kituo kile kilizinduliwa tarehe 25 Juni, 1979. Kwa kuongezeka wananchi katika Mkoa ule wa Kaskazini Pemba. Je, ni lini Serikali itajenga vituo vya polisi katika Wilaya ya Micheweni na Wilaya ya Mkoa wa Kaskazini Pemba pamoja na jengo la RPC wa Mkoa wa Kaskazini Pemba?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Asha Omar, Mbunge wa Viti Maalum, Kaskazini Pemba, kwa swali lake zuri; na nimpongeze sana kwa kuwa karibu sana na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama hasa Jeshi la Polisi na kubaini pia changamoto zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilieleza katika majibu yangu ya msingi wakati nikijibu wiki iliyopita, kwamba kwa upande wa ujenzi wa vituo vya polisi vya mkoa tulikuwa tunakiri kwamba tuna mikoa mitano ambayo ilikuwa haina vituo vya polisi; lakini kwa upande wake alikuwa anaongelea zaidi kuhakikisha kwamba anafanya ukarabati wa jengo la RPC katika Mkoa wa Kaskazini Pemba, ambalo hilo nalo lipo kwenye mpango wa ukarabati kama ambavyo tunaendelea nao. Kwa sasa tuna miradi 56 ya ukarabati nchi nzima katika ngazi na maeneo mbalimbali. Kwa hiyo ninaamini kwamba tukienda kwenye hatua ya pili ya mpango wa kukarabati jengo hilo nalo litaingia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa yale majengo mawili ya wilaya kwa maana Wilaya ya Wete na Wilaya ya Michiweni Kaskazini Pemba nayo yapo kwenye majengo 75 ambayo kwa sasa ama yapo kwenye hatua ya ukarabati ama ujenzi upya kwa wilaya zetu 75 za nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Serikali kupitia Jeshi la Polisi tupo kwenye hatua ya kukamilisha mpango mkakati wa miaka mitano ijayo. Wakati tukiendelea na hatua hiyo, tunaendelea vilevile kutathmini hali ya majengo ya vituo vya polisi, makazi ya askari na maeneo mengine yakiwemo hospitali na majengo ya mazoezi ya vikosi vyetu vya Field Force na mengineyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitambue, wapo Wabunge wengi ambao wamehitaji ama kujengewa ama kufanyiwa ukarabati vituo vya polisi. Kwa ruhusa yako ninaomba niwatambue Mheshimiwa Florence George Samizi, Mheshimiwa wa Kigoma, Mheshimiwa Joseph Copriano Isack au Kadogo wa Monduli wamehitaji hilo, ninatambua pia hitaji lake, Mheshimiwa Anne Kilango Malacela naye na nimemwahidi nitakwenda pia kwenye eneo lake, pamoja na Mheshimiwa Ester Bulaya naye pia alihitaji pale Bunda Mjini, naye nimemwahidi pia nitakwenda.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuwasilisha.