MHE. DICKSON N. KUTEVELE K.n.y. MHE. JESCA J. MAGUFULI aliuliza: -
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha vijana wanapata ujuzi sahihi na kunufaika kupitia Akili Mnemba (AI)?
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Jesca John Magufuli, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kushirikiana na Sekta Binafsi na taasisi za Kimataifa kuhakikisha vijana wanajengewa ujuzi sahihi wa matumizi ya akili mnemba. Vilevile, Serikali imeandaa Mkakati wa Kitaifa wa matumizi salama ya Teknolojia ya akili mnemba unaolenga kukuza ujuzi kuanzia ngazi ya elimu ya msingi hadi vyuo vikuu ili kujenga hazina ya wataalamu mahiri nchini. Aidha, Serikali kupitia Tume ya TEHAMA imepitia mitaala 110 ya vyuo vikuu 32 vyenye Mlengo wa TEHAMA ili kuhakikisha vyuo hivyo vinajumuisha Moduli za Akili Mnemba, hatua inayolenga kuendana na mahitaji ya soko la ajira pamoja na kuzalisha vijana wenye ujuzi wa teknolojia ya kisasa ikiwemo akili mnemba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa Mkakati wa Kitaifa wa Akili Mnemba utahusisha uanzishwaji wa vituo vya ubunifu nchini katika Mikoa ya Lindi, Dodoma, Tanga, Dar es Salaam, Arusha, Mwanza, Mbeya, na Zanzibar. Sambamba na vyuo hivyo, Serikali inakamilisha taratibu za kuanza ujenzi wa Taasisi ya Taifa ya Teknolojia ya Kidijiti katika eneo la Nala – Jijini Dodoma, ambayo itajikita katika utoaji wa mafunzo kwa teknolojia zinazoibukia ikiwemo akili mnemba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi yatakayochochea ubunifu, kuimarisha ushindani wa Kimataifa na kuhakikisha manufaa ya teknolojia ya akili mnemba na teknolojia nyingine zinawafikia wananchi wote kwa maendeleo jumuishi na endelevu.