Supplementary Questions from Hon Zacharia Paulo Issaay (8 total)
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru. Kwa kuwa ni miaka mitatu sasa taarifa ya Wizara ya Mazingira na Wizara zingine mtambuka kuhusu Maziwa ya Babati, Basutu, Tlawi kule Mbulu na Mkoa wa Manyara kwa ujumla haijarudishwa na kazi haijafanyika; je, ni lini Waziri atakwenda Mbulu kutembelea hayo Maziwa? (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa nafasi hii. Ninaomba kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri ya maswali yote mawili ya Waheshimiwa Wabunge. Vilevile, nimshukuru Mheshimiwa Mattar na Mheshimiwa Spika wewe pia, pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote kwa kunipongeza jana na leo kwa kuweza kuchaguliwa kwenye nafasi ya Makamu wa Rais wa Baraza la Mazingira la Umoja wa Mataifa.
Mheshimiwa Spika, ninaomba niongezee sasa kujibu maswali ya Waheshimiwa Wabunge kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza ni dhahiri kabisa nafasi hii ambayo tumeipata inachangiwa na kazi kubwa na mafanikio makubwa na heshima kubwa ambayo Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan na nchi yetu iliyojenga katika Jumuiya ya Kimataifa ndiyo ikawezesha kuweza kupata heshima hii ya kuweza kupata nafasi hiyo.
Mheshimiwa Spika, kupitia nafasi hiyo tunaweza kunufaika katika masuala mengi; moja ni kuhakikisha kwamba tunapenyeza vipaumbele vyetu kama Taifa katika kukabiliana na changamoto za mazingira ikiwemo mabadiliko ya tabianchi, upotevu wa Bioanuwai, masuala mengine mbalimbali yanayohusu ikiwemo nishati safi na kadhalika. Hiyo pia itatusaidia kuweza kunufaika na fedha mbalimbali (fursa za kifedha) kupitia Mifuko ya Mazingira kwenye Jumuiya ya Kimataifa.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge wa Mbulu aliuliza swali la Ziwa Babati. Ninataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba yeye pamoja na Mheshimiwa Mbunge wa Babati Mjini tulizungumza nao kuhusiana na jambo hilo. Hivi sasa ninavyozungumza leo kuna timu ya wataalam imekwenda kule Babati kufanya tathmini ili kuhakikisha kwamba tunafanya nini kwa kupata hatua za dharura za kuweza kukabiliana na tatizo hilo.
Mheshimiwa Spika, wakati huo huo, Serikali ina mkakati wa muda mrefu ikiwemo kununua mitambo ya kukabiliana na changamoto ya magugu maji katika maeneo yote yaliyoathirika na magugu maji katika nchi yetu. Kwa hiyo, hatua za kwanza za dharura tayari tumeanza nazo leo, lakini baada ya muda siyo mrefu tayari tutapata fedha kupitia Serikali Kuu (kupitia Hazina) ili tuweze kupata mitambo ya kukabiliana na tatizo hilo.
Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Serikali ilikusudia kujenga stendi ya mabasi, soko, dampo na machinjio katika Mji wa Mbulu kwa kupitia Mradi wa TACTIC. Hadi sasa Serikali imefikia hatua gani katika kutekeleza mradi huu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO): Mheshimiwa Spika, ujenzi wa stendi katika Mji wa Mbulu ni sehemu ya Miradi ya TACTIC tutakayoitekeleza katika awamu ya tatu. Hivi sasa Serikali inaendelea na ukamilishaji wa Usanifu wa miradi yote 18, kwa maana ya miji yote 18 iliyomo kwenye awamu ya tatu. Mara tu baada ya usanifu kukamilika, taarifa zote tutazikusanya na tutakwenda hatua inayofuata ya kutangaza zabuni kumpata mjenzi, pamoja na mkandarasi mshauri. (Makofi)
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Je, ni lini Serikali itatekeleza ujenzi wa barabara ya Magara – Mbuyuni – Mbulu kwa kiwango cha lami ambapo ni ahadi ya Makamu wa Rais kwa miaka mitano sasa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hii barabara ni kweli inapita kwenye escapement ambapo tunachokifanya sasa hivi ni kujenga kiwango cha zege kwenye ile miinuko mikali ili magari yaweze kupita wakati tunatafuta fedha, lakini kikubwa atakubaliana na mimi kwamba lile Daraja la Magara tulishalikamilisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tunaendelea kutafuta fedha kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami, lakini kikubwa sasa ni kujenga kwa kiwango cha zege kwenye ile miinuko mikali. (Makofi)
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana. Kimsingi masuala haya ya kuchangisha wazazi kupitia shule zetu nchini hayawezi kuepukika kwa baadhi ya maeneo. Kwa mfano, walimu wanaojitolea sasa hivi katika shule zetu nchini ni wengi sana ambao hawajaingia kwenye mfumo wa ajira na ile michango yao inachangwa na wazazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haioni kuwa ni wakati muafaka wa kufanya mapitio upya ya maeneo ambayo yangeruhusiwa kwa mfumo usio rasmi kuchangia ama kwa namna nyingine yoyote ili kuleta uwiano wa kutoa huduma hii ya nafasi ya kufundisha kwa wanafunzi wetu nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilishapitia na itaendelea kupitia kwa kadri itakavyohitajika na kutoa miongozo na maelekezo ya maeneo ambayo Kamati, Bodi na Vikao na mikutano rasmi ya wazazi inaweza ikafikiria kuchangisha ikiwa kutakuwa kuna ulazima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatujaacha dirisha wazi kwamba kila mchango uchangishwe, na ndiyo maana tumeweka utaratibu na Mkuu wa Wilaya na Serikali yake wanajiridhisha kwamba mchango huu ni sehemu ya michango ambayo inaweza ikawa na tija zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Issaay kwamba, tutaendelea kuboresha, na ikiwa kuna maeneo, kuna michango holela na isiyokubalika, tutachukua hatua ili kudhibiti michango holela katika maeneo hayo.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana. Ninaishukuru sana Serikali kwa kazi kubwa na kumlipa mkandarasi wa barabara ya Mbulu - Garbabi - Haydom. Je, kwa kuwa mkandarasi huyu hadi sasa hajarudi site, ni lini mkandarasi wa Mbulu - Garbabi - Haydom atarudi na kuanza kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ni kweli tuna vipande viwili Mbulu - Garbabi na Labay - Haydom ambapo mkandarasi anayetekeleza ni mkandarasi mmoja na tumeshamlipa fedha aliyokuwa anatudai. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mkandarasi atarudi site kwanza kufanya kazi ya kuhakikisha kwamba zile njia za diversion zinapitika, lakini pia kuendelea na kazi ya ujenzi kwa kiwango cha lami.
Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kumwagiza Meneja wa Manyara ahakikishe mkandarasi anarudi site na kuhakikisha kwamba maeneo yote ambayo yalikuwa na changamoto za kutopitika yanapitika wakati anaanza kuijenga hiyo barabara yote kwa kiwango cha lami katika vipande hivyo viwili.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana. Kwa kuwa, idadi hii ya vijana wanaojitolea nchini ni kubwa sana. Je, Serikali haioni kuwa, kuna umuhimu mkubwa sasa wa kufanya takwimu na tafiti, kwa ajili ya idadi ya waliojitolea kwa miaka mitatu hadi sasa, ili Serikali ione namna pekee ya ...
MWENYEKITI: Mheshimiwa Zacharia, zungumza kwa ufanisi akuelewe. Naona Naibu Waziri anapata mashaka na swali lako.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa, vijana wengi sasa hivi wanajitolea kwenye shule zetu na tunashindwa kuwaambia wasiendelee kujitolea kutokana na umuhimu wa nafasi walizoshika na masomo wanayofundisha. Serikali haioni kuwa, ni wakati muafaka sasa wa kuchukua takwimu sahihi ya vijana hawa waliyojitolea kwa miaka mitatu, ili iweze kutoa mwongozo sahihi wa namna ya hao vijana watakavyohudumiwa. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay. Kama nilivyosema kwamba, utaratibu wa ajira sasa unaenda kwa njia ya ushindani kwa sababu, tumejiwekea sera ambayo inatuongoza namna ya kuwapata watumishi wanaoingia katika ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la nyongeza linaeleza namna ambavyo tunaweza kuwatazama kwa karibu wale vijana ambao wanajitolea kwenye shule zetu; tayari Ofisi ya Utumishi imeanza kuweka mkakati wa kuwafuatilia vijana hawa, ambao wanajitolea, lakini utaratibu upo palepale kwamba, watafuata mwongozo ule wa kujitolea wanapoingia kwenye ajira zile za kujitolea, hasa kwenye shule zetu. Kama nilivyosema, mwongozo huu utaelekezwa kwenye shule, utaelekezwa kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa, kwenye taasisi, kwenye Idara na Wizara zote, ili utumike, kwa ajili ya kuwapata vijana wa kujitolea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ajira zile za kujitolea ni kuwaandaa vijana wetu waendeleze taaluma walizozipata vyuoni au shuleni, ili wanapokwenda kupambana katika ajira waweze kutumia vizuri ujuzi walioupata. Kwa sababu, wanapopata ile nafasi ya kujitolea inawapa uwanja mpana wa kuelewa field au kada zao, ili waweze kupambana katika ushindani wa ajira. Ahsante.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Barabara ya Mlima Magara katika Jimbo la Mbulu Mjini barabara yenye jiografia ngumu sana, na kwa kuwa mkandarasi aliyekuwa anajenga zege katika Mlima Magara amesimama kwa muda wa zaidi ya mwaka moja; ni lini mkandarasi atarudi site ili akamilishe zege katika Mlima Magara?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI K.n.y. WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia barabara yake muhimu ambayo kimsingi mkandarasi alikuwa site kama alivyoeleza amesimama.
Mheshimiwa Spika, mara tutakapokamilisha taratibu za fedha tukishamlipa mkandarasi huyo atarejea kufanya kazi na wewe Mheshimiwa Mbunge na wananchi tunaomba muwe na subira kwa kipindi hiki.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana. Barabara ya Mbulu – Garbabi ni barabara aliyopewa mkandarasi wa Kichina kwa miaka minne sasa. Sehemu ya barabara hiyo kutoka Mbulu Mjini kwenda Tlawi ama kwenda pale Tlawi haijatengenezwa kwa miaka minne sasa, mkandarasi huyu wa Kichina anayejenga lami kwa muda mrefu ameshindwa kutengeneza hicho kipande. Mheshimiwa Waziri, nini kauli ya Serikali kumsimamia huyu mkandarasi ili atengeneze hiyo barabara kuondoa adha kubwa sana kwa wananchi wa eneo hilo?
WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Issaay, Mbunge wa Mbulu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kweli katika hii barabara tuna mkandarasi huyu aliyekwisha kumtaja na tayari sehemu ya barabara hii wiki mbili zilizopita tumeilipa. Tumelipia fedha ya kuhakikisha kwamba mkandarasi anarudi site. Ninafahamu ya kwamba hajarudi site bado na moja ya sababu ilikuwa ni hali ya hewa, lakini ninamwagiza sasa mkandarasi na ninamwagiza Meneja wa TANROADS wa Mkoa na TANROADS Makao Makuu kuhakikisha kwamba wanamrudisha mkandarasi, anaanza ujenzi mara moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na ile sehemu iliyobaki ya kilometa zile 25 ambazo zilikabidhiwa kwa mkandarasi, lakini hazijafanyiwa kazi kwa sababu ya kukosekana kwa fedha ya awali ya malipo kwa mkandarasi yule. Ninamwagiza pia Meneja wa TANROADS kwa kuwa barabara hiyo ina mkandarasi wake, lakini hajaanza kazi, bado wajibu huo ni wa kwetu wa kuhakikisha kwamba tunaiboresha ili iweze kupitika wananchi wapate unafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wakati huu yule anapoanza na wao TANROADS mara moja waanze kwa kuisafisha barabara ile ili watu wa Mbulu waweze kupitisha mazao yao ikiwa ni pamoja na mazao ya kilimo kama vile vitunguu na kadhalika kwa urahisi vinavyokwenda sokoni katika Miji ya Arusha, Miji wa Babati na nchini kote kwa ujumla wake. (Makofi)