MHE. SAID I. MZIMBA aliuliza: -
Je, lini Serikali itatenga Bajeti kwa ajili ya ukarabati wa vituo vya Polisi Mtambile na Kengeja kwa kuwa vimechakaa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Said Ibrahim Mzimba, Mbunge wa Mtambile, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekwishafanya tathmini ili kubaini gharama halisi za ujenzi wa Kituo kipya cha Polisi cha Kengeja baada ya kituo kinachotumika sasa kuwa kichakavu na kwamba hakiwezi kufanyiwa ukarabati. Kiasi cha fedha shilingi milioni 165 zinahitajika. Tathmini kwa ajili ya kubaini gharama halisi ya ukarabati wa Kituo cha Polisi Mtambile zimefanyika na kiasi cha fedha cha shilingi milioni 90 zinahitajika. Fedha kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa Vituo vya Polisi vya Kengeja na Mtambile zinatarajiwa kutengwa toka kwenye Bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2026/2027.