Answers to Primary Questions by Hon. Switbert Zacharia Mkama (3 total)
MHE. CONDESTER M. SICHALWE aliuliza:-
Je, upi mpango wa Serikali kupunguza gharama za vifurushi kwa Kampuni zote za simu?
WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa vile nami ni mara yangu ya kwanza, nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa imani yake kwangu na kuniteua kuwa msaidizi wake kama Naibu Waziri wa Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari. Ninapenda niahidi kwamba nitafanya kazi hii kwa uaminifu mkubwa kwa weledi kwa nguvu zangu zote na akili yangu yote.
Mheshimiwa Spika, baada ya utangulizi huo, kwa niaba ya Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, ninaomba nijibu swali la Mheshimiwa Condester Michael Sichalwe, Mbunge wa Momba, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa upatikanaji wa huduma za mawasiliano kwa gharama nafuu kwa wananchi. Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari pamoja na taasisi zake za Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) na Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha huduma za simu, intaneti na data zinakuwa rafiki kwa wananchi.
Mheshimiwa Spka, hatua zilizochukuliwa ni pamoja na:-
(i) Kusimamia ushindani wa haki miongoni mwa Kampuni za simu ili kuchochea ubunifu na upatikanaji wa vifurushi vya gharama nafuu vinavyokidhi uwezo wa wananchi;
(ii) Kufanya mapitio ya gharama na tozo mbalimbali ili kuhakikisha utozaji unazingatia gharama halisi za huduma na kumlinda mlaji wa mwisho;
(iii) Kuhimiza matumizi ya miundombinu ya pamoja ili kupunguza gharama za uendeshaji;
(iv) Kuendelea na Ujenzi wa miundombinu ya Mawasiliano ikiwemo Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano, minara ya mawasiliano maeneo ya vijijini na yasiyo na mvuto wa kibiashara pamoja na ujenzi wa vituo vya kuhifadhi data. Hatua hii inachangia kushuka kwa gharama za huduma, hususan intaneti ya faiba majumbani na maofisini.
Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kufuatilia mwenendo wa soko na kuchukua hatua stahiki za kisera na kikanuni ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za mawasiliano kwa gharama nafuu na sekta inaendelea kuchangia maendeleo ya uchumi wa kidijiti nchini.
MHE. ENG. FADHILI S. CHILOMBE aliuliza:-
Je, Serikali ina mkakati gani wa kujenga mnara wa mawasiliano katika Vijiji vya Kazamoyo, Imani na Kilimani katika Jimbo la Tunduru Kusini?
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Mhandisi Fadhili Sandali Chilombe, Mbunge wa Tunduru Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha miaka minne jumla ya minara 1,041 imejengwa na inatoa huduma za mawasiliano kwa wananchi. Kati ya minara hiyo, minara 758 imejengwa kupitia Mradi wa Tanzania Kidigitali ambao ulizinduliwa rasmi na Mheshimiwa Rais, tarehe 13 Mei, 2023.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) inaendelea na jitihada za kufikisha huduma za mawasiliano katika maeneo yote yaliyosalia ambapo tarehe 5 Desemba, 2025 mikataba ya kufikisha huduma za mawasiliano katika Kata 201 ilisainiwa na utekelezaji wake unatarajiwa kukamilika mwezi Machi, 2027.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mwaka wa Fedha 2025/2026, Serikali kupitia UCSAF imepanga kufikisha huduma hizo katika maeneo mengine 280, yakiwemo maeneo ya kimkakati kama vile reli ya kisasa, hifadhi za Taifa, barabara kuu na maeneo ya mipakani.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kwa kushirikiana na taasisi zake na makampuni ya simu, inaandaa Mkakati wa Kitaifa wa Miaka Mitano (2025 – 2030) wa ujenzi wa minara ya mawasiliano ya simu wenye lengo la kumaliza au kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto ya upatikanaji wa huduma za mawasiliano nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Lukumbule ina minara minne ya mawasiliano iliyojengwa na Makampuni ya Simu ya VIETTEL (mnara mmoja) na TTCL (minara miwili) pamoja na mnara wa Helios Towers Tanzania ambao Vodacom, Airtel na Honora wanautumia kwa pamoja kwa kuweka vifaa vyao vya mawasiliano. Aidha, kutokana na changamoto ya mawasiliano katika Kata hiyo, Vijiji vya Kazamoyo na Imani vimejumuishwa katika mradi wa mawasiliano vijijini, awamu ya tisa unaotekelezwa na Wizara. Usanifu wa minara katika vijiji hivyo umekamilika na ujenzi unatarajiwa kuanza mapema Februari, 2026 na kukamilika mwishoni mwa Mei, 2026, ambapo wananchi wataanza kunufaika na huduma za mawasiliano.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kijiji cha Kilimani kitapata mawasiliano kupitia mnara wa Kazamoyo mara utakapokamilika. (Makofi)
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA aliuliza:-
Je, lini changamoto ya Mawasiliano Jimbo la Tabora Mjini Kata za Ikomwa, Ndevelwa, Ntalikwa, Kabila, Kalunde na Itetemia itamalizika?
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Subira Mwaifunga, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kwa kupitia UCSAF na watoa huduma wa Mawasiliano ilifikisha huduma za mawasiliano katika Kata husika kama ifuatavyo: Kata ya Ikomwa (Airtel, Vodacom na Halotel), Kata ya Ndevelwa (Halotel), Kata ya Ntalikwa (Airtel), Kata ya Kabila (Honora, Airtel na Halotel), Kata ya Kalunde (Honora, Vodacom, Airtel na Halotel) na Kata ya Itetemia (Halotel).
Mheshimiwa Spika, Kata zote sita zimefikiwa na watoa huduma za mawasiliano kama nilivyotangulia kuwataja kwa kuzijengea minara ambayo imekamilika na inafanya kazi. Kwa kuwa Mheshimiwa Mbunge ameuliza swali lake kwa kuonyesha kuna tatizo la Mawasiliano, Wizara kwa kushirikiana na UCSAF na Watoa Huduma wa Mawasiliano itatuma wataalam katika Jimbo la Tabora Mjini ili kufanya tathmini ya kina ya hali ya mawasiliano kwa lengo la kujua tatizo lililopo.
Mheshimiwa Spika, upo uwezekano wa kutokea tatizo la kupatikana kwa mawasiliano ya uhakika katika baadhi ya maeneo hata kama minara ya mawasiliano ilishajengwa katika maeneo hayo kwa sababu kama vile ongezeko la watu, kukua kwa shughuli za kiuchumi pamoja na jiografia ya eneo husika. Pia, sababu nyingine ni kuanzishwa kwa makazi mapya katika maeneo ambayo awali hayakuwa na wakazi, hivyo kuongeza uhitaji wa kujengwa minara zaidi au kuboreshwa kwa minara iliyopo.
Mheshimiwa Spika, tathmini itakayofanyika itatoa suluhisho sahihi, kama ni kuongeza nguvu ya mitambo katika minara iliyopo au kujenga minara mipya. Iwapo suluhisho ni ujenzi wa minara mipya, Kata husika zitajumuishwa katika miradi itakayotekelezwa kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Aidha, kupitia Mradi wa Awamu ya 11 utakaotangazwa mwishoni mwa mwezi Februari, Kata ya Ndevelwa, Kijiji cha Itulu utajengwa mnara wa mawasiliano.