Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Jamal Ramadhan Mwinyi (1 total)

MHE. MWINYI JAMAL RAMADHAN: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa ruksa ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa katika Mkoa wa Kaskazini Unguja katika Jimbo la Bumbwini, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imewekeza nguvu kubwa sana katika uchumi wa nchi na maeneo mengine; je, haioni sasa kuna haja ya kujengwa kituo kikubwa cha polisi katika jimbo hilo kutokana na uchumi wa nchi ulivyokuwa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ruhusa yako na kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, ninaomba kumjibu Mheshimiwa Mwinyi Jamal swali lake la nyongeza kuhusiana na jimbo lake la Bumbwini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiri kwamba Bumbwini kwa sasa ni eneo la kimkakati hasa kwa uchumi wa Zanzibar, kwani Bumbwini inaenda kuelekea kujengwa uwekezaji wa bandari kubwa mpya; Bandari ambayo itakuwa na maeneo karibu matano. Katika bandari ile kwa bahati nzuri wakati nilipokuwa Mkuu wa Mkoa wa mkoa ule, niliwahi kupata fursa ya ushiriki kidogo wa maandalizi ya bandari hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mpango ulioandaliwa wa eneo lile la Bumbwini kumeandaliwa kujengwa miundombinu yenyewe ya bandari, miundombinu ya barabara za kisasa lakini pia kujengwa mji mdogo. Katika mpango uliowekwa wa mji mdogo ndani yake kuna ujenzi wa kituo kikubwa cha polisi ambacho kitaweza kusaidia kuimarisha eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuwasilisha. (Makofi)