Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa nafasi na ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya njema. Ninawashukuru wananchi wangu wa Kiteto kwa heshima kubwa sana waliyonipa, kurudi Bungeni hapa. Ninawahakikishia nitaendelea kuwa sauti yao hapa Bungeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Ndiyo iliyotujengea heshima kule majimboni, ndiyo maana Watanzania wale wametuchagua kwa nguvu nyingi sana. Kwa kweli, kwa miradi ya maendeleo iliyofanyika kwa kipindi cha miaka mitano kwa Kiteto tu peke yake ni kazi kubwa sana na kila Mwanakiteto popote alipo akitoka kwenye kata yake, kijiji chake, ataona mradi ambao umejengwa kwa kipindi cha miaka mitano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa ziara zake anazozifanya na anasikiliza wananchi sana. Tunamwomba aendelee na nguvu hiyo hiyo ya kuwasikiliza Watanzania hawa. Amekuja Kiteto, leo timu ya matumizi bora ya ardhi iko Kiteto kwa ajili ya vijiji karibu 20 kwa sababu ya ziara yake, lakini vilevile kero za wananchi zimeanza kusikilizwa, karibu kero 300 wakati wa ziara hiyo. Ziara hizi za viongozi wetu ni nzuri sana, zinawagusa Watanzania walio wengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza Mheshimiwa Profesa Shemdoe na timu yote ya TAMISEMI. Ninamfahamu Profesa, ni mtu mwema sana, humble. Aendelee hivyo hivyo na timu yake yote, na Mawaziri walioko Wizara hii, kwa kweli, wanafanya kazi nzuri. Tunawaombea Mwenyezi Mungu awape nguvu ili waendelee kumsaidia Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wana-Kiteto safari hii wamenituma nizungumzie barabara peke yake. Barabara tu. Jimbo la Kiteto ni kubwa kidogo, ni square kilometa karibu 17,000. Ukitoka mwanzo wa Kiteto mpaka mwisho ni karibu kilometa 500, jimbo moja, na wako wakulima na wafugaji wanachapa kazi sana; wanalima vizuri, wanafuga vizuri, lakini miundombinu ya barabara imekuwa tabu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mtandao wa barabara. Barabara za TARURA ni kilometa 1,291 halafu zenye lami ni kilometa nne tu peke yake. Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuja Kiteto alipita kwenye Barabara ya Kongwa – Kiteto – Simanjiro, ambayo ni muhimu sana kwa sababu, kwanza magari karibu 533,995 yanapita kwa mwaka. Ni barabara inayounganisha Mikoa ya Dodoma – Manyara – Arusha na Kilimanjaro. Kwa kuwa, sera yetu ni kuweka kipaumbele kwa barabara hizi ambazo zinaunganisha mikoa na kufungua uchumi, barabara hii haikwepeki, yaani haikwepeki sasa!
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema tu, nitawakera sana kipindi hiki kuhusu barabara. Wananchi wa Kiteto wamenituma, in fact wameniambia kila nikipata nafasi hapa nianze kuzungumza kuhusu barabara. Hata nikipata nafasi ya kuuliza swali kwenye Wizara ya Maendeleo ya Jamii, nizungumze barabara hapa. Namna ya ku-frame i-fit, hiyo mniachie mimi, lakini kwa kweli, Wanakiteto sasa wanataka barabara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ilikuwa kwenye mradi ule wa EPC+F, tumesaini mikataba hapa, Wanakiteto walikuja. Tuliambiwa kuna shida imetokea kwenye EPC+F, tunafahamu, lakini kupitia Wizara ya Ujenzi mlisema kwamba, mmehuisha tena mikataba. Kwa hiyo, kwa kweli, kama mnataka kujenga heshima ya wananchi hawa wa Kiteto, Barabara hii ya Kongwa – Kiteto – Simanjiro – Arusha ni muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa ziara, Mwenyezi Mungu alitusaidia, mvua ikanyesha sana na Waziri Mkuu akapita barabara yote hiyo mpaka Arusha. Mwenyezi Mungu alisaidia naye aone. Kwa hiyo, kwa kweli, umuhimu wa barabara hii ni mkubwa sana. Kwa hiyo, tungependa sana majawabu na Serikali ijipange kuleta fedha, kwa ajili ya barabara hii. Barabara hii ni muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya kutoka Handeni – Kibirashi – Kiteto inakwenda Chemba mpaka Singida, ni barabara nyingine muhimu inayounganisha Mikoa minne ya Tanga – Manyara – Dodoma mpaka Singida. Ni barabara ya wakulima na wafugaji, ni barabara ya kilimo, barabara ya mifugo, Itafungua sana uchumi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu umuhimu wa bomba la mafuta na Bandari ya Tanga. Barabara hii itakuwa ni muhimu sana na magari karibu mia tano na themanini na ngapi yanapita kwa mwaka. Kwa hiyo, ni barabara muhimu sana. Ni vizuri Serikali ikajipanga kwa kweli, tupate barabara za lami zitakazofungua uchumi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni ajira kwa vijana. Tumejenga shule nyingi sana, na ni kitu kizuri sana. Tumetoka kwenye shule za kata, sasa tunakwenda vijijini na vijana wasomi wamekuwa wengi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna siku nilikuwa naangalia kipindi fulani hivi kinaitwa sijui, Watu-Back Jobs; kijana mmoja anazungumza anasema, siku hizi GPA ambayo tulikuwa tunafahamu kwamba, ni "Grade Point Average", siku hizi inaitwa ni "Gambling People Association", ile GPA kwa sababu ya frustration, ambayo vijana wanaipata kwa sababu ya kukosekana kwa ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona fedha nyingi hapa, zile shilingi bilioni 200 za Mheshimiwa Rais. Nia ya Mheshimiwa Rais ni kwamba, ifike kwenye majimbo yote, na vijana wengi sana wa Kiteto wameomba hizi fedha. Tunachoomba ni hizi fedha tuone kila kijana ameguswa kutoka kila mahali, siyo kutuletea namba tu kwamba, wameajiriwa vijana kadhaa, hapana. Nchi yetu ni ya ujamaa, ni lazima kazi hizi na fursa zinapojitokeza kila mahali tusikie mkono huu wa Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawaomba sana Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kweli, mratibu wote walioomba kwenye sekta hizi. Tunachotamani ni kuona kwamba, kuna Vijana wa Kiteto, Vijana wa Simanjiro, Kilindi, Chemba huko, majirani zangu wote. Tukiwagusa itaendelea kuwapa courage vijana kwamba, yes, elimu yetu siyo Gambling People’s Association, ile GPA. It matters bado na kwamba, Taifa hili linajali elimu na fursa zipo; lakini lazima tuongeze uwazi katika utekelezaji wa ajira hizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemwambia Profesa, ni kilometa 1,291 mnatuletea shilingi bilioni mbili tu, haiwezekani. Mtuongezee bajeti kwenye TARURA, the minimum ni shilingi bilioni sita. Tungetaka yote, ni shilingi bilioni 11, lakini sisi tunafahamu uchumi wa nchi yetu, angalau sasa ile bajeti itoke shilingi bilioni mbili, twende shilingi bilioni sita angalau, lakini shule za sekondari kidato cha tano na cha sita tunazo mbili tu; Shereta, Maombi, Lesoit, Dongo, Sunya, Dosidosi, Ndedo na Kibaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo haimshindi Profesa. Tumeleta maombi kwa ajili ya mabweni, kwa sababu ya mazingira ya shule zetu. Huko kwetu huko mazingira ya shule zetu lazima yawe bora, ili yawe motisha kwa watu wetu kusoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kazi kubwa sana ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Miaka 50. Hii dira wataalamu wanasema ni "ambitious" lakini ni "achievable." Ni achievable peke yake tukifanya mambo kama haya, kwa sababu, sisi kuandika document nzuri, tuko vizuri sana na hata baada ya dira kwisha tukiambiwa tuandike, kwa nini hatukufanikiwa? Tutaandika document nyingine nzuri sana. Sasa tabu yetu ni utekelezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Hotuba ya Mheshimiwa Rais inasema hivi, ili kutimiza Dira ya Maendeleo ya 2050 ni lazima tujenge utamaduni wa utekelezaji na uwajibikaji, kwa hiyo, hapa lazima mchakamchaka uwepo kidogo. Utekelezaji uko kwa Ofisi ya Waziri Mkuu, tukimbizane wazee, tutoke huko sasa kwamba, sisi tunaambiwa tunaandika document nzuri, na tusipopata matokeo, tunaandika nyingine nzuri ya kusema kwa nini hatukupata? Hebu twende kwenye utekelezaji sasa, dira ni nzuri, itahitaji nguvu kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tumesema private sector. Private sector ni 70% tunatarajia, lakini wanachotaka private sector ni lazima tu-expand tax base, siyo tax burden. Watu wachache lazima tufungue tax na informal sector, lazima waingie, lakini wakati mwingine tunafikiri wawekezaji ni kuomba tu waje nchini. Wawekezaji waliopo nchini, kila mmoja akija hapa anataka aweke kwanza mtaji kidogo halafu jinsi unavyo-behave ndiyo ataongeza zaidi na zaidi na hao ndio wanaongea na watu wengine wote duniani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuache zile sheria ambazo ni unpredictable, zinabadilikabadilika tu, tuache bureaucracy, tuwe ni watu wa vitendo. Tukifanya hivyo, tuta-attract hiyo 7%0 ya private sector. Baada ya kusema hayo machache, nakushukuru na ninaunga mkono hoja. Ahsanteni sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi. Ninampongeza Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu nzima ya Wizara ya Kilimo kwa kazi kubwa ambayo wanafanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Waheshimiwa Wabunge waliotangulia kuwapongeza wakulima wote nchi nzima. Wakulima wanafanya kazi kubwa, ukisikia Taifa lina chakula cha kutosheleza, kazi hii inafanywa na wakulima wa Tanzania nzima hii. Kwa hiyo, tunawapongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo ni maisha, ni zaidi ya biashara, ni zaidi ya uti wa mgongo, ni zaidi ya mgongo wenyewe, ni maisha. Sifa ya kilimo, sifa nyingi sana zimeshatajwa kwamba Watanzania 65% mpaka 75% wanategemea kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nami ninadhani hata hizi data, unajua kutokutegemea kilimo maana yake kuna mtu hali kabisa. Kwa hiyo, ni more than 75%. Kama hulimi, si unauza; kama huuzi, si unakula; sasa si unategemea kilimo. Kwa hiyo, kwa kweli tumpongeze Mheshimiwa Dkt. Samia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama walivyosema wengine, bajeti ya kilimo kuongezeka mara tatu, mara nne kwa kipindi cha miaka mitano ni kazi kubwa sana. Kazi nyingine kubwa aliyofanya ni kumchagua Katibu Mkuu Mstaafu wa Chama cha Mapinduzi, rafiki yangu Mheshimiwa Chongolo. Yeye ni zaidi ya Waziri. Sio Waziri tu, ni Waziri halafu ni Katibu Mkuu Mstaafu wa CCM. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake nini? Yeye anajua nchi hii yote, ameizunguka. Anajua kila mahali, kila kona ya nchi hii. Kwa sababu Chama cha Mapinduzi kinatunza misingi, sisi kazi yetu ni kuisimamia misingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tungependa kwa kweli wakulima kama unavyosikia kwa Wabunge hawa, kila Mbunge amependa kuchangia kilimo kwa sababu kinawagusa Watanzania wote na misingi ya kilimo ni kuzungumza na wananchi wenyewe na kusikiliiza Watanzania wanasema nini kuhusu kilimo. Huo ni msingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi mwingine ni Serikali kuendelea kuwekeza na kuweka mazingira mazuri kwa wakulima nchi hii. Tuwe na sheria nzuri, tuwe na masoko mazuri, tuwe na mbegu bora, nzuri na mbolea na zifike kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa ninasoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri hapa ukurasa wa 148 ninanukuu sehemu ndogo tu: “Nawasihi wakulima wa nchi hii kuwa macho na kuhakikisha wananunua mbegu bora kutoka kwa mawakala waliosajiliwa na kukagua kwa makini nembo za udhibiti ubora na kwenye vifungashio na siyo vinginevyo.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi mkulima leo wa kule Emarti kule Kiteto ama Makame ama Longido huko, yuko kijijini kabisa kule atajuaje kwamba kuna nembo, kuna kifungashio? Unajua Wizara ya Kilimo lazima tuongee lugha ambayo Watanzania wa kawaida wanafahamu. Kuna Watanzania wengine wanakutana na hizi mbegu, imenunuliwa na mtu mwingine, kaileta kijijini. Kwanza atajuaje kwamba huyu kasajaliwa; na nani? Ataona wapi? Kwa hiyo, ninadhani Wizara ya Kilimo iongee lugha ya wakulima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Wizara ifanyeni hiyo kazi ya kupambana na wale wanaoleta mbegu. Tusilete jukumu hili kwa wakulima, ni kazi ya Serikali. Tutasaidiana ndiyo, lakini isifanywe kwamba sisi ndio tukague, halafu tukishindwa tuseme sijui nini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwaambia wakulima wangu, kesho ninachangia, yaani leo sasa; nikawaomba mawazo yao. Kwa kuwa Wizara ya Kilimo ni kuangalia misingi, wasikilize wakulima wa Kiteto wanasema nini, tunaomba magari yale ya Mama Samia Suluhu tukachimbe maji mashambani. Maeneo tunayo, tupate kilimo cha uhakika, ndicho wanachosema wakulima. Mwingine anamwambia mwenzake, anasema Waziri yuko sahihi sana, kilimo cha mara moja kwa mwaka cha kutegemea mvua ni mtihani. Ndicho wanachosema wakulima wale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwingine anasema tupatiwe mbegu bora, lakini changamoto kubwa ni bei. Tunomba Serikali iendelee kupambana, iendelee kufikiria mbegu hizi ni ghali, ishuke ili wakulima wapate motisha ya kwenda mashambani. Vilevile, wanaomba na wanasema masoko yawepo na waunganishwe na masoko ya nje. Huyu ni mkulima mdogo sana wa Kiteto. Ndicho wanachosema. Kwa hiyo, tunataka Serikali iweke mazingira mazuri kwa ajili ya wakulima hawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa ninaangalia mazao ya chakula tunayaagiza kutoka nje ngano na maziwa. Nimekutana na maziwa sasa nikawa ninawaza, sasa hata maziwa yako kwako huku, sasa rafiki yako wa mifugo utakuwa umemwachia nini? Nyama tu. Anyway, lakini kama tunaagiza maziwa, ngano na mafuta ya alizeti, na tuna ardhi ya kutosha, kweli itatuchukua miaka mingi sana kwenda mwezini which is fine. Angalau huku chini basi na sisi tuwe giants kwenye maeneo haya, na tumepata experience wakati wa UVIKO. Mipaka ilipofungwa hakuna mafuta ya kula. Sasa kwa sababu hatuna namna ya ku-control majanga haya yanayotokea huko duniani, ni afadhali tuwekeze kwenye kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli kama alivyosema Mheshimiwa Prof. Muhongo, commitment tuliyofanya ya Malabo ya…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)