MHE. SULEIMAN MOHAMED RASHID aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha maslahi na stahiki za Walimu wanaosahihisha Mitihani ya Taifa ya Kidato cha Nne na Sita?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako ninaomba nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuniteua na kuniamini katika nafasi hii ya kumsaidia Mheshimiwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia.
Mheshimiwa Spika, sasa ninaomba nijibu swali la Mheshimiwa Suleiman Mohamed Rashid, Mbunge wa Mwera. Mitihani ya Taifa ya Kidato cha Nne na Sita ni mitihani muhimu ambayo usahihishaji wake hufanyika kwa baadhi ya walimu kukusanywa katika vituo maalum kwa ajili ya jukumu hilo unaozingatia muda maalum, usalama, usiri, mazingira wezeshi na ubora wa kazi.
Mheshimiwa Spika, stahiki za Walimu wanaosahihisha Mitihani ya Taifa ya Kidato cha Nne na Sita hulipwa kwa kuzingatia miongozo ya usahihishaji wa Mitihani kwa kipindi husika. Ili kuleta ufanisi wa kazi hiyo, miongozo hiyo imeendelea kuboreshwa mara kwa mara. Serikali itaendelea kuboresha maslahi na stahiki za walimu katika usahihishaji wa mitihani ya Taifa ili kuimarisha na kuongeza ufanisi wa kazi hiyo.