Supplementary Questions from Hon. Revocatus Chipando Clayton (3 total)
MHE. CLAYTON R. CHIPANDO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.
SPIKA: Mheshimiwa ni swali moja tu.
MHE. CLAYTON R. CHIPANDO: Mheshimiwa Spika, sawa. Ninaomba majibu kutoka kwa Serikali kuhusiana na Barabara ya Kasulu, barabara ambayo itakwenda kuwasaidia wananchi wa Kata za kama Machinjioni, Rubuga, Kagera pamoja na Kata ya Majengo. Barabara iliyopo sasa hivi inawalazimisha wananchi hawa wakitaka kwenda kwenye kata zao lazima wafike mjini halafu warudi nyuma. Ikijengwa Barabara hii ya Kasulu kuanzia pale Msimba kuelekea Ujiji itasaidia wananchi hawa wasiingie mjini wapate shortcut ya kwenda kwenye makazi yao. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ninaomba kumjibu Mheshimiwa Mbunge Baba Levo, Mbunge wa Kigoma Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, tuna wakala mbili za barabara, TANROADS na TARURA. Mheshimiwa Mbunge, Barabara tunazozijenga sisi ni kuanzia Ujiji hadi Kigoma Mjini, Mwanga kwenda Mwandiga, pale kwenye Sanamu ya Sokwe kwenda Simbo na Mwandiga. Hizi barabara nyingine tutahakikisha kwamba tunawasiliana na wenzetu wa TARURA ili kuhakikisha hizo barabara zinajengwa na wananchi wasipate changamoto kama alivyozielezea Mheshimiwa Mbunge. Ahsante. (Makofi)
MHE. CLAYTON R. CHIPANDO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu kutoka kwa Naibu Waziri wa Kilimo, mimi ninasikitishwa sana na hiki kinachoendelea katika huu mradi wa Bonde la Mto Luiche.
Mheshimiwa Naibu Spika, fedha zimekopwa Kuwait tangu mwaka 2018. Ukienda pale mpaka leo hii ninavyoongea na wewe, anavyosema Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba mradi umeanza, wako wanafyagia miaka nane. Miaka nane tangu tumekopa fedha mpaka leo hii wako wanafyagia tu, wanasema wanakusanya vifaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninamwomba sana Mheshimiwa Naibu Waziri, kama itampendeza, twende wote akajionee vituko vinavyoendelea pale katika Bonde la Mto Luiche. Fedha tumekopa, tumechukua Kuwait, tena fedha hizi alizipambania Mheshimiwa Zitto Kwabwe, alikuwa ndio Mbunge. Mheshimiwa Zitto kamaliza muda wake, mradi haujatekelezwa, kaja Mheshimiwa Ng’enda Kilumbe...
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mbunge, uliza swali la nyongeza.
MHE. CLAYTON R. CHIPANDO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la nyongeza, ninaomba Serikali, tufunge nayo safari kwenda kwenye Bonde la Mto Luiche wakaone kwa macho waache maneno ya kuhadithiwa. Twende naye Naibu Waziri aende pale akaone kwa macho yake nini kinachoendelea pale katika Bonde la Mto Luiche. Hilo ndilo ombi langu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru Mheshimiwa Baba Levo, Mbunge wa Kigoma Mjini kwa concern yake, na sisi kama Wizara tunaelewa hayo anayoyaeleza. Jambo moja tu nimthibitishie, tutaenda kabla hili Bunge halijaisha, tutaongozana, tutakwenda.
Mheshimiwa Naibu Spika, tutapanga moja ya weekend tutafika eneo la mradi, lakini kwa kifupi tu nieleze kwamba, kwa nini mradi huo umechelewa? Hayo anayoyaeleza ni kwamba changamoto ilikuwa ni upatikanaji wa fedha na ndiyo maana Tume ya Umwagiliaji mwaka 2025 ilifanya mapitio upya ya huu mradi, na sasa hivi mradi huu tunautekeleza sisi wenyewe kupitia fedha za ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyozungumza hivi sasa ni kwamba kuna kama shilingi bilioni 8.89 ambazo tutazitoa kwa mkandarasi kama sehemu ya malipo mengine ya awali ili kuhakikisha kwamba mradi huu unaenda kwa wakati. Matarajio yetu kabla mwaka 2030 mradi huu utakuwa umekamilika na Baba Levo atawaeleza wananchi kwamba moja ya jitihada zake kubwa alizozifanya Bungeni ni kuhakikisha mradi huu umekamilika kwa vitendo. (Makofi)
MHE. CLAYTON R. CHIPANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI, nilikuwa na maswali mawili ya nyongeza. Moja litakuwa swali, na lingine litakuwa ombi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza. Bwawa la Katubuka linazidi kuwaletea madhara makubwa sana wananchi wa Kata ya Katubuka na tayari kulikuwa na mkandarasi pale anaendelea na kazi ya kutoa maji yale kwa kutengeneza mtaro mkubwa ambao ulikuwa unayapeleka maji Ziwa Tanganyika. Sasa hivi ameondoa vifaa katika eneo la site. Serikali ina mpango gani wa kumlipa yule mkandarasi ili aweze kumaliza kazi ya kuyaondoa yale maji na kuwaacha wananchi katika makazi yao wakiwa na amani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi la pili, nilikuwa ninaiomba Serikali, sisi Wabunge pamoja na kufanya maendeleo, lakini tunafanya siasa pia. Tulikuwa tunaomba, pale ambapo wanaleta fedha ya ujenzi wa barabara, basi wataalamu wetu waambiwe waje washauriane na sisi, ni barabara gani ambazo zikienda kujengwa zitatusaidia, na pia ndiyo kilio cha wananchi wetu katika Majimbo yetu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani ukiwa uko huku Bungeni unaambiwa tu greda liko mtaani linafanya kazi, unaweza kukuta hiyo barabara inayojengwa ni barabara ambayo kwenye ahadi zako kwa wananchi wako haina umuhimu kama kuna barabara nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kwa ruhusa yako naomba nimtajie barabara tano ambazo hata nikifa leo ninaomba zijengwe katika Jimbo la Kigoma Mjini. Barabara ya kutokea Uwanja la Lake Tanganyika kupita Bezebazeba Sokoni – Rusimbi, Kata ya Majengo pamoja na Kata ya Machinjioni. Barabara ya kutokea Kata ya Mwanga Kaskazini inaitwa Barabara ya Serengeti inayounganisha Kata ya Mwanga Kaskazini na Kata ya Gungu; Barabara ambayo inaunganisha Kata ya Buhanda na Kata ya Businde; Barabara ambayo inaanzia Shini – Vamia – Bega; Barabara ambayo inaanzia Madukani…
MWENYEKITI: Mheshimiwa Clayton ahsante. Ameshakuelewa kwa sababu hilo ni ombi, siyo swali. Kwa hiyo, Mheshimiwa Naibu Waziri ameshakuelewa, tunashukuru…
MHE. CLAYTON R. CHIPANDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naomba sana Mheshimiwa Waziri abaki na hizi barabara kichwani hata nikifa leo hayo ndiyo maombi ya wananchi wa Kigoma Mjini. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, niaomba kwanza nikubaliane na Mheshimiwa Clayton Revocatus Chipando, Mbunge wa Kigoma Mjini kwamba Bwawa la Katubuka ambalo limekuwa likisababisha mafuriko ya mara kwa mara kwa wananchi wa Manispaa ya Kigoma Ujiji, Serikali inatambua kwamba kuna changamoto hiyo na ndiyo maana ilishapeleka mkandarasi pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeshafanya addendum kwenye mkataba kuhakikisha kwamba mkandarasi analiingiza suala la ujenzi wa mfereji mkubwa wa kutoa maji kwenye maeneo hayo yanayosababishwa na mafuriko ya Bwawa la Katubuka kupeleka Ziwa Tanganyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari tuko hatua za mwisho za kufanya malipo kwa mkandarasi ili arejee, aendelee na ujenzi na hatimaye kuondoa kero hiyo ya mafuriko ya mara kwa mara kwa wananchi wa Manispaa ya Kigoma Ujiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, ni kweli kwamba kuna fedha za ujenzi wa barabara ambazo zimeendelea kupelekwa kwenye Majimbo yote kote nchini likiwemo Jimbo la Kigoma Mjini. Hivi karibuni Jimbo la Kigoma Mjini limepelekewa jumla ya shilingi milioni 898 kwa ajili ya kujenga lami ya Baptists mita 800, lakini shilingi milioni 450 kwa ajili ya kujenga Barabara ya Zuru kiwango cha zege mita 420 na bajeti ya Kigoma Mjini imeongezeka kwa mwaka 2025/2026 kutoka bilioni 3.2 za mwaka uliopita mpaka shilingi bilioni 5.33.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali inathamini uboreshaji wa miundombinu ya barabara katika Mji wa Kigoma, lakini nitumie nafasi hii kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI kuwaelekeza Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kwamba ni maelekezo ya Serikali kwamba fedha zozote zinapoingia katika Majimbo yetu, lazima Waheshimiwa Wabunge wapewe taarifa rasmi ya mapokezi ya fedha hizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango ya utekelezaji iwe barabara au miundombinu mingine yoyote, lazima Waheshimiwa Wabunge ambao ni wawakilishi wa wananchi katika Majimbo hayo washirikishwe ili tuwe na uelewa wa pamoja na maamuzi ya pamoja ya utekelezaji wa miradi hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili limetolewa maelekezo mara kadhaa. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge kwamba tutafuatilia kwa karibu na tutachukua hatua kwa Wakurugenzi na Watendaji ambao hawatatekeleza maelekezo haya ya Serikali. (Makofi)