Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025
MHE. ZAINAB ABDALLAH ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Spika, wewe Naibu Spika, pamoja na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano Wa Tanzania kwa kuaminiwa na kwa kazi kubwa na nzuri ambayo mnaendelea kuifanya katika kututumikia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nichukue fursa hii kuwashukuru sana, vijana kutoka mkoa wa Kaskazini Pemba na pia Kamati ya Utekelezaji ya UVCCM Taifa kwa kunichagua, pia, Kamati Kuu kupitia Mwenyekiti wetu wa CCM ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kunithibitisha kuwa Mbunge wa Viti Maalum. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka niwaahidi vijana, nitaendelea kuwa msemaji wao, daraja lao na Serikali, lakini kuhakikisha changamoto zao tunazifikisha na zinapatiwa ufumbuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma Surah Ar-Rahman, Aya 55:60 inasema: “Hal jaza ul ihsan illal ihsan.” Je, kuna malipo ya wema kwa mtu anayekutendea mema zaidi ya wewe kumtendea mema. Ukisoma Zaburi 136:1 inasema, “Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema kwa maana Fadhili zake ni za milele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa kwa niaba ya vijana, kutoa shukrani zetu za dhati kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anayoifanya kwa mustakabali wa maendeleo ya Taifa letu, na kwa kasi kubwa ya miradi ya maendeleo katika Taifa letu. Leo sisi ni mashuhuda, hakuna kijiji, hakuna kata, na hakuna wilaya utakayoenda usikute miradi iliyoachwa kama alama na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, iwe kwenye elimu, iwe kwenye afya, iwe kwenye maji, iwe kwenye miundombinu ya umeme, barabara, mawasiliano, Uchumi wa Buluu, utalii, kila sekta kama hujakuta alama ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, basi wewe utakuwa hujaizunguka Tanzania na hujatembelea vijiji kuona hayo maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni mwanadiplomasia na nimekuwa nikifuatilia hotuba za viongozi mbalimbali ndani ya Afrika na hata nje ya Afrika. Ninataka niwathibitishie Wabunge kwamba hotuba ambayo ameiwasilisha Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 14 Novemba, 2025 ni kati ya hotuba bora kabisa kuwahi kutokea ndani ya Bara la Afrika. Mheshimiwa Rais ana mapenzi makubwa sana na Watanzania. Mheshimiwa Rais kupitia hotuba ile ameonesha uzalendo na utu wa kuwatumikia Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kama kijana ninapata faraja kwa sababu hii inaonesha kwamba Mheshimiwa Rais anatambua kwamba 76% ya Watanzania iko chini ya umri wa miaka 36 ambao ni vijana. Kupitia hotuba ile Mheshimiwa Rais ameonesha mahaba na mapenzi makubwa sana kwa vijana wa Kitanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia hotuba ile, kwa mara ya kwanza kwenye historia ya nchi yetu, Mheshimiwa Rais ameunda Wizara ambayo ipo chini ya Ofisi ya Rais inayohusika na Maendeleo ya Vijana. Kwa kweli leo tunaye Waziri wa Vijana Mheshimiwa Joel Nanauka, ninaomba nimpe maua yake, anafanya kazi kubwa na kazi nzuri sana kuwatumikia vijana wa Taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, Mheshimiwa Rais ameenda mbali kusema kwamba ataweka washauri chini ya Ofisi ya Rais watakaoshughulikia maendeleo ya vijana. Ninataka niseme jambo moja, katika maeneo ambayo kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais yamenigusa sana moyo wangu ni pale Mheshimiwa Rais alipoonesha kwamba anataka uwajibikaji, na uadilifu Serikalini. Anatamani kuona watendaji wetu wakiwa na nidhamu wakiwajibika na wakiwatumikia Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia hotuba ile, Mheshimiwa Rais amesema: “Ninawaelekeza Mawaziri hadi Maafisa Tarafa wawe karibu na wananchi waende kusikiliza na kutatua kero za wananchi,” na watakaposhindwa kufanya hivyo, yeye atachukua hatua.
Mheshimiwa Naibu Spika, hii inanikumbusha kauli ya Baba wa Taifa mwaka 1961 pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliwahi kusema yafuatayo: “Those of you who have received this privilege, therefore have the duty to repay sacrifices which others have made.” Ninyi ambao mmebahatika kupata fursa hii, mna jukumu la kuhakikisha mnawajibika ili kujitoa kwa wale ambao wamejinyima ili ninyi leo muwe hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka niwaambie viongozi na watendaji wenzangu, Watanzania tupo 60,000,000, lakini leo wewe umepata heshima ya kuwa Waziri, leo umepata heshima ya kuwa Mkuu wa Mkoa, leo umepata heshima ya kuwa Mkuu wa Wilaya, leo umepata heshima ya kuwa Mkurugenzi, Afisa Tarafa, au Mtendaji Kata, ninataka utambue dhamana ambayo umepewa, una wajibu wa kuhakikisha unarudisha fadhila kwa wale ambao wamejinyima ili wewe uwe hapo kwenye hiyo nafasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninampongeza sana Waziri Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, kupitia mabaraza ya kazi anayoyaendesha, ametoa mwelekeo wa namna Serikali itakavyojipambanua. Amesema siku ya leo hapa, watumishi wote wanaofanya kazi kwa mazoea, watumishi wote ambao hawatimizi wajibu wao, na watumishi wote ambao badala ya kuwa suluhu ya kutatua migogoro, wao ndio wanakuwa sehemu ya kuongoza migogoro. Hawa watumishi hawatavumiliwa na Serikali ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kwenda mbali zaidi na kutaka tu-review sheria zetu ili wale ambao wanadhani wakiharibu sehemu moja wana uwezo wa kupelekwa sehemu nyingine hao waweze kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria. Hao watu ndio wanaotia doa Serikali yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya kazi kubwa na nzuri sana, lakini baadhi ya watumishi, baadhi ya viongozi wasioitakia mema nchi yetu, wasiokuwa na utayari wa kulitumika Taifa letu, ndio wanaomhujumu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mawaziri ambao mmepewa dhamana, tunawaamini na hatuna mashaka na ninyi. Nendeni mkawasimamie watumishi ili waweze kufanya kazi kwa mujibu wa sheria, taratibu na kanuni za nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kama Mbunge ambaye ninawakilisha kundi la vijana, ninatambua ya kwamba changamoto kubwa ya vijana ni ajira, lakini ninataka niwaambie vijana wanaonisikiliza huko mitaani, hakuna nchi duniani ambayo imemaliza tatizo la ajira. Maendeleo ni hatua, Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imejipambanua leo Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameahidi kupitia hotuba yake kwamba atahakikisha kunakuwa na kongani za viwanda kwenye kila wilaya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia viwanda hivi, vijana watapata ajira, Serikali itakusanya mapato, na nchi yetu itapiga hatua kimaendeleo. Mheshimiwa Rais ameahidi kutoa shilingi 200,000,000,000 kwa ajili ya kuwawezesha vijana na wanawake. Mitaji hii itaenda kuwakwamua vijana kiuchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia, Mheshimiwa Rais ameahidi ujuzi kuhakikisha kwamba, kwa sasa tuna VETA 64 kwenye wilaya 64. Ahadi ya Mheshimiwa Rais ni kuhakikisha kila wilaya kwenye wilaya 139 nchini kutakuwa na Vyuo vya VETA na vijana watafungamanishwa na miradi ya kimkakati ili waweze kupata ujuzi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ameahidi kutakuwa na kampasi kila mkoa ili tunapokuwa na Vyuo Vikuu kwenye mikoa hii, vijana wetu waweze kupata elimu na ujuzi, lakini kuweza kuchagiza uchumi kwenye mikoa husika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, ninaomba nihitimishe kwa nukuu ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, alisema haya yafuatayo: “Kwa wanangu vijana wa Taifa la Tanzania, nchi hii imejengwa kwenye misingi ya amani na utulivu wa kisiasa; sisi wazazi wenu tungeshawishika kuyafanya mliyoyafanya wakati huu nchi hii isingekuwa na neema na maendeleo mnayoyaona hii leo. Hivyo, ninawasihi wanangu vijana, nchi hii ni yenu, kwa shida zozote zile zinazowakabili, msikubali hata siku moja kushawishiwa kuichoma nchi yenu wenyewe. Msikubali kukata tawi la mti ambalo mmeukalia. Msikubali kabisa. Ninyi ndio walimu na wajenzi wa Taifa hili, ninawasihi vijana, kamwe msiwe wabomoaji wa Taifa lenu.” Mwisho wa kunukuu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaunga mkono hoja, ninaomba kuwasilisha. (Makofi)