Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Zainab Abdallah Issa (4 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. ZAINAB ABDALLAH ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Ukisoma maandiko yanasema, mshukuruni Mungu kwa kila jambo, maana moyo usiokuwa na shukurani hukausha mema yote, lakini ukisoma Quran Surat Sabayi aya ya 13 inasema, "Wa Qalilun Min 'Ibadiya sh-Shakuru" (na wachache ni miongoni mwa wale wenye shukrani).

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa kutoa shukrani zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaendelea kuifanya, na ndani ya siku 100 za uongozi wake ahadi ambazo ameziahidi ameweza kuzitekeleza ikiwemo ahadi ya uzinduzi wa bima ya afya kwa wote ambapo tayari imeshaanza kwa awamu ya kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ameahidi shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kuwawezesha wajasiriamali wadogo. Fedha hizo tayari zimekwishatolewa, lakini ameahidi mpango wa pamoja wa mafunzo kati ya waajiri, VETA pamoja na vyuo vikuu. Jambo hili tayari limeshafanyika pamoja na gridi ya Taifa ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tunasema tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, na juzi tumeshuhudia Wizara ya Kazi, Ajira na Mahusiano ikisaini mikataba mitano mikubwa kwa ajili ya kuwawezesha vijana kupata ajira nje ya nchi. Hili ni jambo kubwa sana, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, sisi wote ni mashuhuda, amekuwa akifanya ziara mkoa kwa mkoa, wilaya kwa wilaya, jimbo kwa jimbo, na kote alipopita ametekeleza majukumu yake ipasavyo, na amejenga matumaini makubwa sana kwa Watanzania. Kwa hiyo, sisi tunampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee tunawapongeza Wizara ambazo zipo ndani ya ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu: Wizara ya TAMISEMI; Kazi, Ajira na Mahusiano; Sera, Bunge na Uratibu, wanafanya kazi kubwa na kazi nzuri sana, hongereni sana viongozi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunavyofahamu, sasa hivi tunatekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050, na kwa sasa tunatekeleza Dira ya 2025/2026 kwenda 2030/2031 na msingi wa miaka hii mitano ni ujengaji wa uchumi shindani pamoja na kuzalisha ajira kwa maana ya tunaenda kufanya transformation, economic growth and job creation.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama tunaenda kwenye uchumi shindani, imani yangu kubwa ni kwamba TAMISEMI ni moyo wa Serikali. TAMISEMI iki-paralyse, Serikali ina-paralyse; TAMISEMI ikifanya vizuri, Serikali inafanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaongea hivyo kwa uzoefu. Alhamdulillah nilipata heshima ya kuhudumu kama Mkuu wa Wilaya kwa miaka tisa na nusu. Ninajua kwamba Wizara ya TAMISEMI ni Wizara ambayo inashughulika na sekta zote za maendeleo. Ukienda kwenye mikoa na wilaya, niwapongeze sana Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa, Ma-RAS, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi, Ma-DAS, na Maafisa Tarafa, wanafanya kazi kubwa na nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya, maji ya kwake, umeme wa kwake, barabara za kwake, afya ya kwake, na elimu ya kwake. Ndiyo maana nikasema TAMISEMI ni moyo wa Serikali. Kwa hiyo, ninapongeza kazi kubwa na nzuri ambayo imefanyika, lakini yapo maeneo ambayo ninatamani nishauri yaweze kuboreshwa na kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la kwanza ni eneo la uwajibikaji. Hayati Mzee Benjamini William Mkapa alisema uwajibikaji ndiyo msingi wa maendeleo. Wengi waliozungumza, wameelezea ziara ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, na yapo mambo ambayo yalipaswa kushughulikiwa chini, lakini yameenda kwake. Tuna haja ya kufanya reforms kwenye halmashauri zetu. Kama ambavyo tunataka economic reforms katika nchi, ipo haja ya kufanya reforms kwenye halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu ametuhakikishia kwamba hakutakuwa na business as usual, kutakuwa na business unusual; ili twende kwenye business unusual ni lazima watu waache kufanya kazi kwa mazoea. Watendaji wa Vijiji, Watendaji wa Kata, na Maafisa Tarafa, hawa watu chini huku wakitimiza wajibu wao vizuri Mkuu wa Wilaya, DAS, Mkurugenzi, Mkuu wa Mkoa, na RAS watakuwa na kazi nyepesi sana ya kufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni lazima TAMISEMI sasa ishuke chini kule kwa watendaji kuhakikisha wanawabana kama ni kwa mujibu wa sheria, haiwezekani mtu aharibu hapa apelekwe pale. Watu wanafanya kazi kwa urasimu, jambo la kufanyika kwa siku moja linaweza likachukua miezi mitatu. Haya mambo ni lazima tukubali kuyabadilisha ili tuweze kupiga hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni eneo la ukusanyaji wa mapato. Ninadhani ndiyo focus kubwa ya Rais, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha kwamba halmashauri zetu zinakusanya mapato. Kwa bahati mbaya sana, ukiangalia ile Idara ya Mapato kwanza watumishi ni wachache, lakini professionalism ni changamoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, unakuta unazungumza na Afisa Mapato wa Halmashauri, hata vipaumbele vyake vitano vya mapato havifahamu. Unamwambia nioneshe Ledger Book, nioneshe Cash Book hana. Unamwuliza, vyanzo hivi vya mapato mara ya mwisho vimekusanywa lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna wafanyabiashara wamekaa miaka mpaka 10 hawajawahi kutozwa baadhi ya tozo ambazo ziko kwa mujibu wa sheria za halmashauri. Kwa hiyo, tunaona kabisa hii Idara ya Mapato ifanye reforms, tufanye mageuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunaweza kufanya mabadiliko zaidi kuhakikisha kwamba aidha tunaunda kampuni ambayo itakuwa specific kwa ajili ya kubeba ajenda za kiuchumi, kwa sababu leo hii tunasema tunataka uchumi shindani lakini hatuna blue print ya uwekezaji kwenye wilaya zetu. Ukienda kwa Mkurugenzi, ukimwambia nioneshe maeneo ya uwekezaji, atakutajia kwa mdomo, lakini hatuna blueprint ya uwekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ambayo yametengwa kwa ajili ya kongani za viwanda, maeneo ambayo yametengwa kwa ajili ya kujenga hoteli, maeneo ambayo yametengwa kwa ajili ya kilimo kikubwa cha kisasa, hayo mambo digitalized hayapo. Kwa hiyo, ni muhimu sana kuangalia jinsi gani tunaweza kuimarisha Idara ya Fedha ili tubebe ile ajenda ya Mheshimiwa Rais ya kusema kila wilaya tuwe na viwanda vya kimkakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaamini huku chini tukiweka vizuri, tutakuwa na viwanda kwenye kila wilaya, na bidhaa ambazo zinaweza kuzalishwa ndani, tutazizalisha sisi wenyewe. Hatuna sababu ya kuagiza vitu nje ya nchi ilhali sisi kama Watanzania ndani ya nchi tuna uwezo wa kuvizalisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ameahidi ajira 8,000,000 kama tukiwa na business mind tukawa strategically located. Ninawahakikishieni, tuna uwezo wa kukusanya fedha nyingi sana kupitia Serikali za Mitaa. Shilingi trilioni moja hii ni ndogo kulingana na uhalisia wa vyanzo vilivyopo, mipango miji wakifanya kazi yao vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii tuna issue ya (PPP) Public Private Partnership. Tukishirikisha wadau wa sekta binafsi kuwekeza kwenye miradi mbalimbali ya kimkakati ndani ya halmshauri zetu, tuna uwezo wa kukusanya mapato makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, John F. Kennedy aliwahi kusema: “Don’t ask what America has done for you? Ask how much you have done for the Americans?” Nami ninairudisha kwetu Watanzania, tusiulize Tanzania imetufanyia nini? Hebu sisi tujiulize tumeifanyia nini Tanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaunga mkono, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. ZAINAB ABDALLAH ISSA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami nichangie bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nami ninakushukuru kwa kunipa nafasi hii kuchangia bajeti ya Wizara ya Ulinzi. Ninachukua fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uhai na uzima, lakini kwa namna ya kipekee kabisa ninachukua fursa hii kumpongeza na kumshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuimarisha ulinzi na usalama wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee kabisa tunampongeza Mheshimiwa Rais, mwaka huu Februari kwa kuzindua Makao Makuu ya Usalama wa Taifa, kwa ajili ya kuhakikisha kwamba viongozi wetu na wafanyakazi na taasisi za Wizara hii wanakuwa na mazingira bora ya kiutendaji na ya kufanyia kazi kwa ufanisi. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa sababu mradi ule wa makao makuu umeweza kugharimu zaidi ya shilingi bilioni 120. Haya ni maendeleo makubwa sana ndani ya Wizara hii. Tunampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee tunampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kutuamini vijana na kutupa nafasi za juu kabisa za uongozi wa Taifa letu. Leo tunashuhudia kwenye historia ya Wizara hii tumepata Waziri kijana, mnyenyekevu, mchapa kazi, Mheshimiwa Dkt. Rhimo Nyansaho ambaye huyu ni mbobezi na mzamivu wa masuala ya uchumi. Tunampongeza sana kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais kuwa Mbunge, lakini pia kuwa Waziri wa Wizara hii ya Ulinzi. Hakika anaitendea haki Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi kama Mjumbe wa Kamati ninataka niwaambie Wabunge wenzangu, mara ya kwanza Mheshimiwa Waziri alipokuja kwenye Kamati alikuwa anaweza kuitafsiri Wizara hii kichwani mwake bila kusoma popote. Kwa hiyo, tumeona kabisa jicho la mama limemwona huyu kijana mwenzetu, mchapakazi, mnyenyekevu, na ninaamini kwa weledi aliokuwa nao, na kwa namna anavyoishi na watu, na uwezo wa kusikiliza na kupambanua mambo, hakika atafika mbali. Tunamwombea sana kwa Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunampongeza sana Katibu Mkuu wa Wizara hii, yeye ndiyo encyclopedia ya Wizara hii. Kijana mnyenyekevu, mchapakazi, kwa kweli anafanya kazi kubwa sana na kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa namna ya kipekee ninaomba tumpongeze sana Mkuu wa Majeshi yetu, CDF Jenerali Jacob John Mkunda pamoja na Kamandi zote za vikosi vyetu vya ulinzi na usalama kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaendelea kuifanya kuhakikisha nchi yetu inaendelea kuwa salama.

Mheshimiwa Spika, pia bila ya kumsahau mnadhimu wa jeshi ndugu yetu luteni jenerali Salum Haji Othumani, wanafanya kazi kubwa na kazi nzuri sana kumsaidia CDF, tunakupongeza sana, lakini pia tunampongeza Mkuu wetu wa JKT, Meja Jenerali Rajabu Mabele pamoja na Mkuu wa SUMA-JKT wanafanya kazi kubwa na kazi nzuri sana, tunawapongezeni sana.

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizo tunaomba tuwatie moyo wanajeshi wote na vikosi vyote vya usalama, kwamba kazi wanayoifanya ya kulinda amani na usalama wa nchi yetu, sisi kama Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tunawapongeza sana na tunawatia moyo na tunathamini kwamba sisi muda tukiwa tunalala wao wapo macho kupambania usalama wa Taifa letu. Tunawapongezeni sana na Mwenyezi Mungu azidi kuwalinda na kuwabariki kwa kuendelea kuimarisha usalama wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ninaomba nitume salamu kwa Wizara ya Fedha. Suala la amani halina compromise, tunaweza ku-compromise mambo mengine yote, lakini siyo suala la usalama wan chi yetu. Ninaiomba sana Wizara ya Fedha itusaidie kwenye suala zima la kutoa bajeti ya kutosha kwenye Wizara hii ili Wizara hii waendelee kufanya kazi kwa ufanisi wa hali ya juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano Fungu 57 la Wizara, fedha ambazo zimetoka ni 43.6% lakini pia kwenye fedha za miradi ya maendeleo, kwenye fedha shilingi bilioni 318, fedha zilizotoka ni shilingi bilioni 110 sawa na 34.6%, lakini pia Shirika la Nyumbu fedha ambazo zimetoka ni 32%, Shirika la Mzinga fedha zilizotoka ni 33%.

Mheshimiwa Spika, tunaomba sana Wizara ya Fedha, kuhakikisha kwamba wanatoa fedha hizi ili taasisi hizi zilizopo chini ya Wizara ziweze kufanya kazi kwa ufanisi wa hali ya juu sana, kwa sababu bila ya kuwawezesha, maana yake tunawafanya wafanye kazi katika mazingira magumu ya kulinda amani na usalama wa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, la pili, niipongeze sana JKT (Jeshi la Kujenga Taifa), wamefanya kazi kubwa na kazi nzuri sana na kupitia SUMA-JKT mwaka huu tumeona wametoa gaio la shilingi bilioni moja kwenye Mfuko wa Hazina, haya ni mafanikio makubwa sana na mimi niungane na Mbunge mwenzangu Mheshimiwa Fadhili Liwaka, kuwaomba sana waone uwezekano wa vijana wetu wanaohitimu kidato cha sita kuhakikisha kwamba hawa vijana wanapata fursa ya kwenda kupata mafunzo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sasa hivi capacity ya JKT wanauwezo wa kuchukua vijana 60,000 lakini vijana wanaohitimu kidato cha sita ni 125,000. Niiombe sana Wizara ya Fedha iwape ushirikiano wenzetu wa Wizara ya Ulinzi kupitia JKT, kwa sababu tunaandaa Taifa la kesho na bila kuwaandaa vijana ambao ni wazalendo, tutakuwa tunatwanga maji kwenye kinu, hatuwezi kupata matokeo tunayoyatarajia. Ninajua mpango wa Wizara ni kuhakikisha mpaka ifikapo mwaka 2031 wanaweza kuwa na capacity ya vijana 120,000; lakini niwaombe Wizara kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha kupitia SUMA-JKT wauone uwezekano wa kimkakati kabisa kuwezesha hili shirika letu la SUMA-JKT kuweza kufanya miradi ya kimkakati.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tunaona SUMA-JKT wanafanya shughuli za ulinzi kwenye makampuni mbalimbali na kwenye miradi ya kimkakati ikiwemo SGR, wanafanya kazi kubwa sana kwenye Bwawa la Hydropower la Mwalimu Julius Nyerere, wanafanya kazi nzuri sana kwenye miradi ya kimkakati. Tunaomba sana pamoja na hii kazi nzuri wanayoifanya kwenye ulinzi, lakini pia kwenye ujenzi wa miradi mbalimbali tuone uwezekano wa kutanua wigo kwenye sekta za kimkakati kwa mfano uwezekano wa kuwa na kongani za viwanda, lakini pia kwenye sekta ya madini ili tuendelee kulinda rasilimali za Taifa letu lakini kupitia wao tuweze kupata fedha zakuwezesha JKT iweze kuendesha mafunzo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tunatambua sasa hivi kupitia JKT kuna skimu mbalimbali za umwagiliaji kama pale Chita kuna skimu ya umwagiliaji. Pale Chita tuna hekari 12,000 lakini tuna kilimo cha umwagiliaji hekari 2,500. Niiombe sana Wizara ya Kilimo...

(hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa muda wako umekwisha.

MHE. ZAINAB ABDALLAH ISSA: Mheshimiwa Spika, niiombe sana Wizara ya Kilimo iweze kuwa-support wenzetu...

SPIKA: Nikuombe ...

MHE. ZAINAB ABDALLAH ISSA: Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo ninaunga mkono hoja, ahsante sana.
Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025
MHE. ZAINAB ABDALLAH ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Spika, wewe Naibu Spika, pamoja na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano Wa Tanzania kwa kuaminiwa na kwa kazi kubwa na nzuri ambayo mnaendelea kuifanya katika kututumikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nichukue fursa hii kuwashukuru sana, vijana kutoka mkoa wa Kaskazini Pemba na pia Kamati ya Utekelezaji ya UVCCM Taifa kwa kunichagua, pia, Kamati Kuu kupitia Mwenyekiti wetu wa CCM ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kunithibitisha kuwa Mbunge wa Viti Maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka niwaahidi vijana, nitaendelea kuwa msemaji wao, daraja lao na Serikali, lakini kuhakikisha changamoto zao tunazifikisha na zinapatiwa ufumbuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma Surah Ar-Rahman, Aya 55:60 inasema: “Hal jaza ul ihsan illal ihsan.” Je, kuna malipo ya wema kwa mtu anayekutendea mema zaidi ya wewe kumtendea mema. Ukisoma Zaburi 136:1 inasema, “Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema kwa maana Fadhili zake ni za milele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa kwa niaba ya vijana, kutoa shukrani zetu za dhati kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anayoifanya kwa mustakabali wa maendeleo ya Taifa letu, na kwa kasi kubwa ya miradi ya maendeleo katika Taifa letu. Leo sisi ni mashuhuda, hakuna kijiji, hakuna kata, na hakuna wilaya utakayoenda usikute miradi iliyoachwa kama alama na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, iwe kwenye elimu, iwe kwenye afya, iwe kwenye maji, iwe kwenye miundombinu ya umeme, barabara, mawasiliano, Uchumi wa Buluu, utalii, kila sekta kama hujakuta alama ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, basi wewe utakuwa hujaizunguka Tanzania na hujatembelea vijiji kuona hayo maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni mwanadiplomasia na nimekuwa nikifuatilia hotuba za viongozi mbalimbali ndani ya Afrika na hata nje ya Afrika. Ninataka niwathibitishie Wabunge kwamba hotuba ambayo ameiwasilisha Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 14 Novemba, 2025 ni kati ya hotuba bora kabisa kuwahi kutokea ndani ya Bara la Afrika. Mheshimiwa Rais ana mapenzi makubwa sana na Watanzania. Mheshimiwa Rais kupitia hotuba ile ameonesha uzalendo na utu wa kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kama kijana ninapata faraja kwa sababu hii inaonesha kwamba Mheshimiwa Rais anatambua kwamba 76% ya Watanzania iko chini ya umri wa miaka 36 ambao ni vijana. Kupitia hotuba ile Mheshimiwa Rais ameonesha mahaba na mapenzi makubwa sana kwa vijana wa Kitanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia hotuba ile, kwa mara ya kwanza kwenye historia ya nchi yetu, Mheshimiwa Rais ameunda Wizara ambayo ipo chini ya Ofisi ya Rais inayohusika na Maendeleo ya Vijana. Kwa kweli leo tunaye Waziri wa Vijana Mheshimiwa Joel Nanauka, ninaomba nimpe maua yake, anafanya kazi kubwa na kazi nzuri sana kuwatumikia vijana wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, Mheshimiwa Rais ameenda mbali kusema kwamba ataweka washauri chini ya Ofisi ya Rais watakaoshughulikia maendeleo ya vijana. Ninataka niseme jambo moja, katika maeneo ambayo kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais yamenigusa sana moyo wangu ni pale Mheshimiwa Rais alipoonesha kwamba anataka uwajibikaji, na uadilifu Serikalini. Anatamani kuona watendaji wetu wakiwa na nidhamu wakiwajibika na wakiwatumikia Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia hotuba ile, Mheshimiwa Rais amesema: “Ninawaelekeza Mawaziri hadi Maafisa Tarafa wawe karibu na wananchi waende kusikiliza na kutatua kero za wananchi,” na watakaposhindwa kufanya hivyo, yeye atachukua hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii inanikumbusha kauli ya Baba wa Taifa mwaka 1961 pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliwahi kusema yafuatayo: “Those of you who have received this privilege, therefore have the duty to repay sacrifices which others have made.” Ninyi ambao mmebahatika kupata fursa hii, mna jukumu la kuhakikisha mnawajibika ili kujitoa kwa wale ambao wamejinyima ili ninyi leo muwe hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka niwaambie viongozi na watendaji wenzangu, Watanzania tupo 60,000,000, lakini leo wewe umepata heshima ya kuwa Waziri, leo umepata heshima ya kuwa Mkuu wa Mkoa, leo umepata heshima ya kuwa Mkuu wa Wilaya, leo umepata heshima ya kuwa Mkurugenzi, Afisa Tarafa, au Mtendaji Kata, ninataka utambue dhamana ambayo umepewa, una wajibu wa kuhakikisha unarudisha fadhila kwa wale ambao wamejinyima ili wewe uwe hapo kwenye hiyo nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninampongeza sana Waziri Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, kupitia mabaraza ya kazi anayoyaendesha, ametoa mwelekeo wa namna Serikali itakavyojipambanua. Amesema siku ya leo hapa, watumishi wote wanaofanya kazi kwa mazoea, watumishi wote ambao hawatimizi wajibu wao, na watumishi wote ambao badala ya kuwa suluhu ya kutatua migogoro, wao ndio wanakuwa sehemu ya kuongoza migogoro. Hawa watumishi hawatavumiliwa na Serikali ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kwenda mbali zaidi na kutaka tu-review sheria zetu ili wale ambao wanadhani wakiharibu sehemu moja wana uwezo wa kupelekwa sehemu nyingine hao waweze kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria. Hao watu ndio wanaotia doa Serikali yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya kazi kubwa na nzuri sana, lakini baadhi ya watumishi, baadhi ya viongozi wasioitakia mema nchi yetu, wasiokuwa na utayari wa kulitumika Taifa letu, ndio wanaomhujumu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mawaziri ambao mmepewa dhamana, tunawaamini na hatuna mashaka na ninyi. Nendeni mkawasimamie watumishi ili waweze kufanya kazi kwa mujibu wa sheria, taratibu na kanuni za nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kama Mbunge ambaye ninawakilisha kundi la vijana, ninatambua ya kwamba changamoto kubwa ya vijana ni ajira, lakini ninataka niwaambie vijana wanaonisikiliza huko mitaani, hakuna nchi duniani ambayo imemaliza tatizo la ajira. Maendeleo ni hatua, Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imejipambanua leo Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameahidi kupitia hotuba yake kwamba atahakikisha kunakuwa na kongani za viwanda kwenye kila wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia viwanda hivi, vijana watapata ajira, Serikali itakusanya mapato, na nchi yetu itapiga hatua kimaendeleo. Mheshimiwa Rais ameahidi kutoa shilingi 200,000,000,000 kwa ajili ya kuwawezesha vijana na wanawake. Mitaji hii itaenda kuwakwamua vijana kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, Mheshimiwa Rais ameahidi ujuzi kuhakikisha kwamba, kwa sasa tuna VETA 64 kwenye wilaya 64. Ahadi ya Mheshimiwa Rais ni kuhakikisha kila wilaya kwenye wilaya 139 nchini kutakuwa na Vyuo vya VETA na vijana watafungamanishwa na miradi ya kimkakati ili waweze kupata ujuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ameahidi kutakuwa na kampasi kila mkoa ili tunapokuwa na Vyuo Vikuu kwenye mikoa hii, vijana wetu waweze kupata elimu na ujuzi, lakini kuweza kuchagiza uchumi kwenye mikoa husika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, ninaomba nihitimishe kwa nukuu ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, alisema haya yafuatayo: “Kwa wanangu vijana wa Taifa la Tanzania, nchi hii imejengwa kwenye misingi ya amani na utulivu wa kisiasa; sisi wazazi wenu tungeshawishika kuyafanya mliyoyafanya wakati huu nchi hii isingekuwa na neema na maendeleo mnayoyaona hii leo. Hivyo, ninawasihi wanangu vijana, nchi hii ni yenu, kwa shida zozote zile zinazowakabili, msikubali hata siku moja kushawishiwa kuichoma nchi yenu wenyewe. Msikubali kukata tawi la mti ambalo mmeukalia. Msikubali kabisa. Ninyi ndio walimu na wajenzi wa Taifa hili, ninawasihi vijana, kamwe msiwe wabomoaji wa Taifa lenu.” Mwisho wa kunukuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaunga mkono hoja, ninaomba kuwasilisha. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. ZAINAB ABDALLAH ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi nami nichangie hoja ya Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana. Leo nimesimama hapa kuwasilisha sauti za vijana wote wa Kitanzania, vijana wanaotaka mabadiliko ya kweli. Hatma ya Taifa hili iko mikononi mwetu sisi vijana, na hii ni kwa sababu zaidi ya 76% ya nguvu kazi ya Taifa hili ni vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ninukuu kauli ya Nelson Mandela ambaye aliwahi kusema, "The development of any nation cannot prosper if the generation of young people is left behind." Maendeleo ya nchi yoyote hayawezi kupiga hatua kama kundi kubwa la vijana litaachwa nyuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee ninaomba nichukue fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwanza, kwa mapenzi makubwa aliyokuwa nayo kwa vijana wa Taifa hili na kwa kuona umuhimu kwenye historia ya nchi hii kwa mara ya kwanza kuanzisha Wizara mahususi inayohusu maendeleo ya vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais ameenda mbali zaidi kwa kutoa fedha shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kuwawezesha vijana kiuchumi. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. Kwa niaba ya vijana wenzangu, tunataka kumhakikishia kwamba, sisi vijana hatutamwangusha. Tunatambua kwamba tuna wajibu wa kuhakikisha kuwa tunalinda amani na utulivu wa Taifa letu ili nchi yetu iweze kupiga hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaamini, kama ambavyo nchi yetu imerithishwa hivi leo ikiwa kwenye mikono salama, sisi vijana tuna wajibu wa kuhakikisha tunaendeleza amani na utulivu wa Taifa hili ili nchi hii iendelee kubaki kuwa salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee ninampongeza sana Waziri wetu wa vijana Mheshimiwa Joel Nanauka, pamoja na menejimenti nzima ya Wizara, kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaendelea kuifanya, na kwa ubunifu mkubwa ambao wameuonesha ndani ya muda mfupi tangu wamekabidhiwa jukumu hili na Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi vijana tumeona uanzishwaji wa Vijana Platform, platform ambayo yeye binafsi, Mheshimiwa Waziri amezunguka mkoa kwa mkoa kwenda kusikiliza na kutatua kero za vijana. Pongezi sana kwa Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wa Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninampongeza kwa kuanzisha vijana call centre, mfumo ambao unatoa uhuru wa vijana kuwasiliana moja kwa moja na watendaji wa Wizara, ikiwemo Mheshimiwa Waziri. Hili ni jambo la kupongezwa na la kuungwa mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninampongeza kwa kuja na Vijana Uchumi Challenge kwa ajili ya kuibua vipaji vya vijana wenye mawazo kwa ajili ya kujikwamua kiuchumi. Kwa hiyo, ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na timu nzima ya Wizara kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo, ushauri wangu kwenye Wizara hii, moja, kwa kuwa tuko katika utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050, na kwa kuwa malengo ya dira hii ni kwamba tuhakikishe sekta binafsi inachangia 70% ya uchumi wa Taifa letu, na kwa kuwa nguvu kazi ya Taifa hili ni 76% ambayo kundi kubwa ni vijana, ipo haja ya Serikali kuanza kupitia upya sheria, sera, na kanuni zetu ili kuhakikisha zinafungamanishwa na ushiriki wa sekta binafsi, pia kuhakikisha kuwa vijana wanapewa nafasi na kwamba wanatambulika katika kushiriki kwenye marekebisho ya sera, kanuni pamoja na sheria zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, leo tuna Sheria ya Public Private Partnership ya Mwaka 2023, lakini ukiitazama ile PPP Act na ukija kutazama Sheria ya Procurement Act unaona kabisa hatuwezi kufungamanisha vitu hivi viwili na tukapata tija kama inavyotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, ukiangalia PPP Act inatoa fursa kwa mwekezaji mwenye wazo la kuendeleza miradi kupata hiyo fursa ya kuweza kuendeleza miradi, lakini ukija kwenye Procurement Act inataka utaratibu na mmlolongo mzima wa Serikali uweze kufuatwa ili mtu aweze kupatikana wa kufanya shughuli mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unakuta Procurement Act mchakato unaweza kuchukua zaidi ya siku 90, lakini mbaya zaidi waombaji wanakuwa wengi pengine hata yule ambaye alikuja na lile wazo asibahatike kuweza kushiriki kufanya lile wazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna haja ya sheria zetu kufanyiwa mapitio, na sheria ambazo zimekaa kwa zaidi ya miaka 10 zifanyiwe maboresho ili ziendane na masuala ya Public Private Partnership pamoja na ushirikishaji wa vijana. Hili ni jambo kubwa na ni jambo muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, sasa hivi tuna Wizara hii, lakini tunahitaji instruments za kuweza kuisimamia Wizara hii. Leo hii maafisa vijana wapo chini ya halmashauri chini ya Afisa Maendeleo ya Jamii. Ipo haja ya maafisa vijana kwenye halmashauri waripoti moja kwa moja Wizara ya vijana ili waweze kuwa na dhana ya uwajibikaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona mabadiliko hayo yamefanyika kwenye Wizara mbalimbali wakati halmashauri kipindi cha nyuma maafisa hawa, ma-engineer wa maji walikuwa chini ya halmashauri, lakini sasa hivi hawa Wakurugenzi, Maafisa wa Idara ya Maji wanaripoti moja kwa moja Wizara ya Maji na wanajibishwa na Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hawa maafisa wa vijana hawatakuwa chini ya Wizara ya Mheshimiwa Waziri, ni ngumu sana kuwawajibisha kwa sababu watakuwa chini ya halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna maafisa vijana ambao ni wazee, uwezo wao wa kufanya kazi ni mdogo, uwezo wao wa kubuni ni mdogo. Hili jambo la kuwa na watendaji wanaoendana na kasi ya vijana ni muhimu sana kuzingatiwa katika kuwapata hawa watendaji wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia sasa hivi tuna Sera ya Maendeleo ya Vijana ambayo imekuwa reviewed 2024. Pia tuna mkakati wa utekelezaji wa sera hii wa miaka kumi, 2024 hadi 2034, lakini hatuna mpango kazi wa muda mfupi na muda mrefu ambao utatupatia majibu, mpango kazi kuhusiana na umuhimu wa kupata masoko ya uhakika kwa vijana, mpango kazi utakaoonyesha mkakati wa kupata elimu ya ujuzi kwa vijana, mpango kazi utakaoonyesha miundombinu wezeshi kwa ajili ya kukuza ujasiriamali na uwekezaji, mpango kazi ambao utaonyesha ushiriki wa sekta binafsi katika kukuza maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ipo haja ya kuwa na mpango kazi ambao utatupa direction kwa ndani ya miaka hii 10, nini tunaenda kukifanya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni hili la benki ya vijana. Ninapongeza kwa kuwa na wazo hili na kuanza kulichakata. Ipo haja ya kuwa na benki ya maendeleo ya vijana. Kama tumeweza kuwa na Benki ya Maendeleo ya ya Kilimo tunashindwaje kuwa na benki ya maendeleo ya vijana ilhali 76% ya nguvu kazi ya Taifa hili ni vijana?

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tuna programu na mifuko 74 ya uwezeshaji wananchi kiuchumi, lakini pengine vijana wanafahamu mifuko miwili tu. Wanafahamu mfuko wa 10% na wanafahamu na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana, lakini leo tuna mfuko wa Small and Medium Enterprises Fund, tuna Mfuko wa Maendeleo ya Wajasiriamali, tuna Mfuko wa Kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi, tuna mifuko 74.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatamani mifuko hii iratibiwe na benki ya maendeleo ya vijana ili vijana sehemu zote ndani ya nchi yetu waweze kupata fursa ya mitaji kwa sababu changamoto kubwa ya vijana ni suala zima la mitaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa 10% kipindi cha nyuma mchakato ulikuwa unawa-favour baadhi ya watu na kuwanyima baadhi ya watu nafasi. Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan alisimamisha mchakato huu, na baadhi ya maeneo sasa hivi pilot imefanyika kwa ajili ya hizi fedha za 10% kupitia benki zetu. Hata hivyo taarifa iliyopo benki nyingi mpaka sasa hawajatoa fedha hizi za 10% kwa vijana, lakini pia kuna urasimu mkubwa wa utolewaji wa fedha hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, tangu maelekezo yametoka ni takribani mwaka mmoja sasa hivi. Tunatamani tupate tathmini ya uhakika, je, kupitia mfumo huu wa benki pilot study inakuja na majibu gani? Kuna haja ya kuendeleanao au hatuna haja ya kuendeleanao ili vijana huko kwenye halmashauri zetu waweze kupata fedha hizi?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. ZAINAB ABDALLAH ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuhitimisha, ninataka niwaambie vijana wenzangu, tumekuwa na ulalamikaji kwamba hatushikwi mikono. Serikali imeanza kutushika mikono, tuache kulalamika vijana wenzangu, tutumie fursa hizi zilizopo ili tuweze kujikwamua kiuchumi. Tanzania itajengwa na sisi sote, tushikamane kwa pamoja kuleta maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja. Ninakushukuru sana.