MHE. EDIBILY K. KINYOMA aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwalipa fidia Wananchi wa Kitongoji cha Katoto waliopisha Mradi wa Kitalu cha Makere Forest Reserve?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Spika, maelekezo ya wananchi wa Kitongoji cha Katoto kuhama yalitolewa mwezi Oktoba, mwaka 2022 na Kamati ya Mawaziri Nane wa kisekta baada ya kubaini kuwa wananchi hao walikuwa nje ya mipaka ya Kijiji Mama cha Kagera. Serikali ilifanya tathmini ya kaya na makazi na kugawa eneo la ukubwa wa Hekta 4,446 katika Kitongoji cha Nyantuku, Kijiji cha Kagerankanda ambapo kila kaya ilipewa eneo la kujenga la ukubwa wa mita 32 kwa 64 na hekari tatu kwa ajili ya shughuli za kilimo.
Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia maelekezo ya Serikali kupitia Kamati ya kisekta ya Mawaziri Nane, wananchi wa Katoto waliohamishwa walishapatiwa fidia ambayo ni ardhi kwa ajili ya makazi, kilimo na mifugo ikiwa ni pamoja na Serikali kuwapatia usafiri wa mali zao kipindi walichokuwa wanahama. Hadi kufikia mwezi Oktoba, 2025 uongozi wa Mkoa wa Kigoma kwa kushirikiana na uongozi wa Wilaya ya Kasulu ulifanikiwa kuhamisha wananchi wote kutoka Kitongoji cha Katoto na kwenda Kitongoji cha Nyantuku, Kijiji cha Kagerankanda.