Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Esther Nicholas Matiko (3 total)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Mji wa Tarime ni miongoni mwa maeneo ambayo yanapata mvua ya mara kwa mara, na hivyo kusababisha barabara kuharibika na kuathiri shughuli za maendeleo na uchumi za Mji wa Tarime.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka kujua, nini mkakati wa Serikali wa kulingana na mazingira ya Halmashauri ya Mji wa Tarime ya mvua ya mara kwa mara, kujenga barabara ambazo zitastahamili hali ya hewa ya Mji wa Tarime ili wananchi wa pale waweze kupita muda wote kwenye barabara zao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO): Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya Barabara za Tarime ni kama ilivyo hali ya Barabara za Mji wa Morogoro. Mpango ambao tumeuweka kwenye Mkoa wa Morogoro, vivyo hivyo tutau-extend kwenda Tarime. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, Barabara ambayo inaanzia keep left inakwenda mpaka Mogabiri yenye kipande cha takriban kilometa 9.3 iliyopo Tarime Mjini imeharibika sana kiasi cha kupelekea ajali mbaya sana na wakati mwingine vifo. Hata hivyo, kwa sababu tayari mkandarasi yupo na yupo tayari kuanza kazi anasubiri tu malipo ya awali, Serikali haioni kwamba kuna umuhimu wa kupeleka fedha hizi ambazo ni takriban shilingi bilioni 7.9 ili barabara hii iweze kutengenezwa na kuunganishwa na ile barabara inayoenda mpaka Nyamwaga ambayo tayari imeshakamilika? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ninaomba nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge kwamba kipande hicho ni kweli kimeharibika, kilikuwa na lami, lakini barabara ilitangazwa yote. Ilibidi tuanze mbele ili baadaye tuweze kufumua kipande hiki ambacho amekiongelea Mheshimiwa Mbunge. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tunajua kwamba hatuwezi tukatoka na barabara ya vumbi kutoka Tarime halafu tukaenda kuipata lami mbele. Kwa hiyo, nimhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali tunaandaa malipo ili mkandarasi aweze kulipwa na kuanza kuikarabati, ambayo ni sawa na kuijenga upya hiyo barabara ambayo ina zaidi ya kilometa tisa. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Tarime una Miradi mitatu ya TACTIC, ambayo ni Stendi ya Kimange, barabara za lami ikiwepo Barabara kutoka Lebu – Kebaga mpaka Biyambu, ambayo ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa Tarime pamoja na Mradi wa Dampo. Ninataka kujua ni lini sasa miradi hii itaanza na kukamilika kwa manufaa mapana ya wananchi wa Tarime Mji? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO): Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Tarime ni miongoni mwa miji inayokua kwa haraka. Nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa namna anavyoupambania huu Mji wa Tarime; tupo katika mpango wetu wa kutekeleza huu Mradi wa TACTIC Awamu ya Tatu na ngazi ya usanifu wa dhana, pamoja na usanifu wa awali tuko mwishoni kuukamilisha. Tutakwenda kutangaza zabuni, kuanza ujenzi mara moja. (Makofi)