Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Denis Lazaro Londo (2 total)

MHE. JOHN J. NCHIMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza baada ya kupata majibu haya mazuri. Swali la kwanza; Mheshimiwa Naibu Waziri atakubaliana nami kwamba Mheshimiwa Rais anapokuwa ametoa ahadi na pia ahadi hiyo inapokuwa imewekwa katika Ilani ya chama ni ahadi ambayo inatakiwa itekelezwe na Serikali na siyo kuwasubiri Private Sectors ambao wanaweza wakaja muda wanaopenda wao na ikapita hata miaka mitano inayotarajiwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; je Serikali haioni umuhimu wa kukusanya wataalam wake waende kuwasaidia wananchi wa wilaya yangu kuwezeshwa kusaidiwa kupata mikopo ambayo ni ya riba nafuu kutoka maeneo ya Serikali kama Agricultural Bank, TIB na Benki ya Ushirika?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nimshukuru Mheshimiwa John John Nchimbi kwa maswali yake mawili ya nyongeza. Ni kweli ninaungana naye Mheshimiwa Rais anapotoa ahadi jukumu letu sisi kama Serikali ni utekelezaji wa ahadi hiyo. Kimsingi Serikali imeshaanza utekelezaji wa ahadi hiyo na ndiyo maana Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa imeshatoa miche 2,000,000 kwa wakulima wa kahawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo wameshanunua eneo kwa ajili ya ujenzi wa kiwanda, uzalishaji wa kahawa Nyasa umeongezeka na ndiyo maana kuna umuhimu wa ujenzi wa kiwanda. Ukisoma Dira ya 2050 inazungumzia ushirikishwaji kwa maana tunazungumzia Uchumi Jumuishi na Sekta Binafsi ina mchango wa 70%. Ndiyo maana Serikali kupitia taasisi za fedha, kupitia wadau kama Vyama vya Ushirika tunaendelea kuhamasisha kuwekeza katika viwanda vya kati ili kushiriki kikamilifu katika dhana ya Uchumi Jumuishi kama nguzo ya Dira ya 2050 inavyosema.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala la uwezeshaji wa Serikali ninaungana na Mheshimiwa Mbunge. Ndiyo maana sisi kama Serikali tumeshatoa mwongozo kwa halmashauri kuona kwamba mazao ambayo yanatokana na maeneo husika tunaenda kuyajengea uwezo Vyama vya Ushirika. Pia kuomba fedha maalum kupitia bajeti ya Serikali kuona uwezeshaji wa ujenzi wa viwanda hivyo ili kuongeza mnyororo wa thamani, kuongeza thamani ya mazao, kupunguza gharama ya uzalishaji na kuchochea uzalishaji katika maeneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuwasilisha.
MHE. IBRAHIM M. SHAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mheshimiwa Naibu Waziri, Moshi ni Mji ambao ulikuwa na viwanda vingi sana, lakini viwanda vile sasa hivi vimekufa na vimechukuliwa na wawekezaji na wale wawekezaji hawawekezi wamevichukua tu kama magofu. Ni lini Serikali itaweza kuwanyang’anya viwanda vile na kuvifanyia kazi?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilivitoa viwanda hivi kwa wawekezaji kwa nia ya uzalishaji. Mkataba wa makabidhiano wa viwanda hivi kwa hao wawekezaji unawataka wauheshimu kwa maana ya kuendelea na shughuli za uzalishaji. Ndiyo maana kwa Moshi kuna Kiwanda cha Kilimanjaro Machine Tools ambacho mimi mwenyewe nilikuwa pale wiki mbili zilizopita kazi za uzalishaji inaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maeneo mengine ambayo wawekezaji wamepewa viwanda hivi na havizalishi, rai yetu ni moja tu kuwaambia kwamba, aidha warudi kwenye uzalishaji ama Serikali itachukua hatua ya kuwapatia viwanda hivyo wawekezaji ambao wana nia ya dhati ya kushiriki katika ujenzi wa Dira ya 2050 kwenye Uchumi wa Viwanda na Uzalishaji kwa ajili ya shughuli ya kuongeza mnyororo wa thamani wa mazao yetu.