Supplementary Questions from Hon. Zuberi Yahya Mfaume (3 total)
MHE. ZUBERI Y. MFAUME: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona na kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Jimbo la Morogoro Kusini ni miongoni mwa majimbo ambayo yako katika hali mbaya sana ya miundombinu kwa sababu, sehemu kubwa ya jimbo hili ni milima, na hivyo, inaathiri hata performance yetu katika elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia takwimu za ufaulu, tuko chini na hali ya afya tuko hoi. Tuna changamoto ya Barabara ya Dakawa – Bwakila Juu, ambayo kwa kweli haipitiki kabisa. Tuna changamoto ya barabara ya Kolelo – Lukange...
MWENYEKITI: Mheshimiwa uliza swali moja kwa moja.
MHE. ZUBERI Y. MFAUME: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni kwamba, ni kwa kiasi gani tutapewa upendeleo maalumu kutokana na hali mbaya tuliyonayo, kwa ajili ya kuzikarabati barabara hizi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO): Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalipokea hili, na Serikali, tutalifanyia kazi kwa kadiri ya ambavyo tutapata taarifa za wataalamu wetu tukimshirikisha Mheshimiwa Mbunge. Pia ninampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kuchaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Sheria Ndogo.
MHE. ZUBERI Y. MFAUME: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa, shughuli hizi za madini ni shughuli zinazowaendeshea maisha wananchi wenzetu. Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa sasa elimu ya utunzaji wa mazingira ili wananchi wenzetu waendelee na shughuli zao za kujipatia kipato?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba shughuli za madini ni shughuli muhimu kwa uchumi wa nchi yetu na wananchi na sisi Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira kwa kushirikiana na Wizara ya Madini na Wizara zote zenye nasaba na masuala ya mazingira na madini tutaendelea, kwanza kuhakikisha kwamba tunatoa elimu kwa wananchi na wachimbaji wote wa madini kuzingatia sheria na taratibu za uhifadhi wa mazingira ili kuwa na uchimbaji wa madini na uhifadhi wa mazingira endelevu. Ahsante sana.
MHE. ZUBERI Y. MFAUME: Mheshimiwa Spika, ninaomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza kutokea katika swali langu la msingi.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; mpaka hivi sasa ninavyozungumza hapa bado kuna mifugo katika mashamba ya wakulima huko katika Jimbo la Morogoro Kusini. Nini kauli ya Mheshimiwa Naibu Waziri sasa hivi ili iweze kutekelezwa na mifugo hiyo iondolewe katika mashamba ya wakulima?
Mheshimiwa Spika, swali la pili; Wizara ina mpango gani sasa katika Jimbo la Morogoro Kusini kuongeza ujenzi wa majosho, malambo pamoja na kasi ya kuelimisha wafugaji juu ya ufugaji bora wa kisasa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. JAFAR R. SEIF): Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu maswali mawili madogo ya nyongeza ya Mheshimiwa Mfaume, Mbunge wa Morogoro Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze kwa maswali yanayogusa changamoto hizi za wakulima na wafugaji. Sisi Ofisi ya TAMISEMI tunashirikiana kwa karibu sana na Wizara ya Uvuvi na Mifugo na wameendelea kutoa elimu wenzetu Wizara ya Mifugo na pia wanatoa mbegu za ruzuku kwa ajili ya malisho ili kuondoa migogoro hii kabisa.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, tunaendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi na vyombo vingine vya ulinzi na usalama kuhakikisha mifugo inaondolewa katika maeneo ya wakulima wetu na baadae nitakaa na Mheshimiwa Mbunge pamoja na Mheshimiwa Waziri wa Mifugo ili tuweze kuyaangazia maeneo haya na kupata ufumbuzi wa kudumu.
Mheshimiwa Spika, vilevile, Serikali imeendelea kujenga majosho mengi nchini. Nimwombe Mheshimiwa Mbunge tuweze kuainisha eneo ambalo hasa amelizungumzia ambalo halijapata majosho mpaka sasa ili tuweze kujenga majosho hayo.