MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba niishukuru Serikali kwa majibu mazuri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, Serikali ipo tayari sasa kuleta timu ya wataalam mara baada ya Mkutano huu wa Bunge?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Serikali ipo tayari kutumia sasa Mradi wa Bukene pamoja na Mradi wa Isemela ambao bado unatekelezwa kuweza kufikisha huduma ya maji katika Vijiji vya Zobogo, Tinde, Nuru pamoja na Igulamya? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kujibu swali la nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa Serikali iko tayari na kama nilivyojibu katika swali la msingi, Wizara inatarajia kuunda timu ambayo itaenda kule Itwangi na kwenda kufanya tathmini na kujiridhisha na hali halisi ya huduma ya upatikanaji wa maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika miradi 3,714 ambayo Serikali iligharimu takribani shilingi trilioni 1.8, ndani ya Itwangi kulikuwa na miradi tisa iliyokamilika yenye gharama ya shilingi bilioni 12.7. Ndani ya Jimbo hili tunayo miradi inayoendelea miwili ambayo ina gharama ya shilingi bilioni 8.9 ikiwemo na kuhakikisha kwamba vijiji vilivyobaki katika eneo hilo ni vijiji 14 tu ambavyo vimebaki bila kuwa na huduma ya maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, eneo la Tinde, pamoja na Didia, pamoja na Samuye yote yataingizwa katika utaratibu wa kupata huduma ya maji safi na salama. Ninakushukuru sana. (Makofi)