Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Musa Godfrey Mbuga (1 total)

MHE. MUSSA G. MBUGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mbinu gani mpya za kukabiliana na tembo vijiji vya Ng’hanga, Mwambongo, Matale, Longalonhinga, Sakata, Nyanza na Banhya?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuendelea kuboresha na kuibua mbinu mpya, Serikali imeendelea kutumia teknolojia mbalimbali ikiwemo uzio wa umeme kwa ajili ya kuimarisha udhibiti wa tembo wanaoingia kwenye makazi na mashamba ya wananchi. Aidha, Serikali kupitia wadau wa uhifadhi ina mpango wa kuweka uzio wa umeme kuzunguka mpaka wa Hifadhi ya Pori la Akiba Maswa kwa upande wa magharibi unaopakana na makazi ya wananchi utakaozuia tembo kutoka nje ya hifadhi na kuleta madhara kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua nyingine, Serikali imeandaa Mkakati mpya wa Kitaifa wa Kusimamia Utatuzi wa Migongano baina ya Binadamu na Wanyamapori wa miaka 10 kuanzia 2025/2026 hadi 2035/2036. Mkakati huu utatekelezwa kwa ushirikiano na Wizara za kisekta ikiwemo: TAMISEMI, Maliasili na Utalii, Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi chini ya uratibu wa Ofisi ya Waziri Mkuu ili kuhakikisha kuwa jitihada za kupunguza changamoto hii zinafanyika kwa pamoja na kwa ufanisi zaidi. Aidha, ushirikiano mpana wa Wizara mbalimbali unaifanya nchi kuwa na mfumo thabiti ulioratibiwa na unaozingatia maslahi ya watu na uchumi wa Taifa letu.