Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Juma Ramadhani Mustafa (1 total)

MHE. JUMA R. MUSTAFA aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kutenga maeneo ya malisho katika Jimbo la Igalula ili kupunguza migogoro kati ya Wakulima na Wafugaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. RAJAB S. JAFAR) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Juma Mustafa Kawamba, Mbunge wa Jimbo la Igalula, Halmashauri ya Uyui, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI:-

Mheshimiwa Spika, eneo la Igalula limekuwa na migogoro midogo ya wakulima na wafugaji, hususan katika maeneo ya kulishia mifugo. Aidha, migogoro hii imekuwa ikitatuliwa kupitia maridhiano ya mtu na mtu na hata kuwahusisha viongozi wa Serikali, kwa ajili ya kusimamia taratibu za fidia kwa hasara inayojitokeza. Aidha, Serikali imetenga jumla ya hekta 6,226.92 katika vijiji 16 vilivyopo Igalula.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha, kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi wa Matumizi Bora ya Ardhi, ikiwa ni pamoja na kuainisha na kutenga maeneo maalum ya wakulima na wafugaji, kwa ajili ya ustawi wa wakazi wa Halmashauri ya Wilaya ya Uyui. Pia, Serikali inatoa wito kwa viongozi ngazi ya mkoa na halmashauri kote nchini kuhakikisha wanatatua migogoro ya wakulima na wafugaji kwa wakati na kuweka utaratibu mzuri wa matumizi bora ya ardhi.