MHE. SHAFFIN A. SUMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri sana kwa majibu mazuri ambayo kwa kweli yanatia moyo. Ninaomba niulize swali la kwanza; Serikali imejipanga vipi kukabiliana na tatizo ambalo linaweza kutokea ya bei ya tumbaku kushuka na kwa kuzingatia kwamba wakulima tayari walishalima tumbaku yao, walishafulia mabedi na tayari walishaweka mbolea: mbolea ambazo ni NPK, CAN na UREA ambazo mpaka sasa hazijapewa ruzuku?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; je, Serikali itaweka lini mpango mzuri wa utaratibu rasmi wa ushirikishi na kuruhusu kampuni za tumbaku kwenda kujinadi kwa wakulima ili mkulima awe na haki ya kuchagua kampuni ambayo ana maslahi nayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Shaffin Ahmedali Sumar, Mbunge wa Uyui, ni moja ya Wabunge makini sana, ambaye anafanya kazi nzuri katika jimbo lake.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimthibitishie tu kwamba, moja, sisi kama Serikali katika kuhakikisha kwamba tunakabiliana na anguko la bei katika mazao yote nchini ikiwemo tumbaku. Moja ya jambo kubwa ambalo tunalifanya ili kutoa ruzuku ya pembejeo, maana yake ni kumpunguzia mkulima gharama ili azalishe kwa gharama ya chini na akishazalisha aweze kuuza katika bei inayohusika, hata panapotokea anguko la bei maana yake walau mkulima anaweza akapata faida.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, tunaendelea kujenga viwanda vya kuchakata haya mazao vikiwemo viwanda vya kuchakata tumbaku. Yote ile ni kuhakikisha kwamba tunapunguza gharama. Tuna viwanda ambavyo, AMCOS zinakaribia kujenga vile viwanda vya vifungashio. Lengo lote lile ni kutaka kumpunguzia mkulima bei ya zao lake. Kwa hiyo, kitu ambacho nikuthibitishie Mheshimiwa Mbunge ni kwamba moja ya mkakati wa Serikali ni kuhakikisha mazao yote yanaingia katika mpango wa ruzuku, lakini kwa awamu na kwa kuzingatia mahitaji ya kila wakati, ikiwemo hili eneo ambalo ameliaininisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mpango wa kampuni kwenda kujinadi, kwa sababu tumekuwa na kila mwaka tuna mkutano wa wadau wa tumbaku na jambo hili lilishakuwa linafanyika hapo nyuma kabla ya kubadilishwa mfumo wake, basi sisi kama Serikali tumelipokea na katika kikao kinachokuja kwa wadau tutalifikisha pale. Wadau watalijadili na yale watakayokubaliana, sisi Serikali tutakuwa tayari kuyatekeleza.
MHE. SHAFFIN A. SUMAR: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo. Kwa kuwa tatizo la mawasiliano ni la nchi nzima na katika Jimbo langu la Uyui tatizo kama hili lipo na linasumbua sana katika Kata ya Ibili, Ibelamirundi, Ndono, Makazi na Bukumbi. Je, ni lini Serikali itapeleka wataalam ili waangalie maeneo ambayo yanafaa kuweka mnara waweze kuweka haraka iwezekanavyo ili wananchi waache kupanda miti kutafuta mawasiliano? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Uyui kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ninaomba nichukue nafasi hii pia kumwelekeza tena Mkurugenzi Mkuu wa TCRA kutuma timu ya wataalam katika Jimbo la Uyui kuweza kufanya tathmini na kutambua changamoto zilizopo za mawasiliano katika jimbo hilo.