Contributions by Hon. Eng. Amosy William Maganga (5 total)
Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025
MHE. ENG. AMOSY W. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nami ninaanza kwa kushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kutoa mchango wa Wanasikonge, kwenye hotuba hii nzuri ya Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ningeomba kabla sijaendelea, uniruhusu niweze kutoa tathmin ndogo sana ambayo niliiona kwenye jimbo langu nilipotembelea wakati ninawashukuru wananchi kwa kazi kubwa waliyoifanya tarehe 29 Oktoba, 2025. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Sikonge lina jumla ya kata 20, vijiji 71, vitongoji 287 na kwa sasa lina wakazi 372,800 na hii ni kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2022 pamoja na projection rate ya asilimia 3.1 Kwa hiyo, kwa hivi sasa tuko 372,800. Katika jimbo langu hilo niliweza kutembelea kata zote na nilibahatika kufanya mikutano zaidi ya 46. Ninafurahi kusema kwamba idadi ya watu walioongea wao wenyewe kwenye mikutano hiyo walifika 678. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninasema kwamba kati ya hao watu 678 watu 230, sawa na 34%, waliongelea changamoto ya barabara katika maeneo yao. Vilevile, watu 142 sawa na 21%, waliongelea ufinyu au upatikanaji wa maeneo ya shughuli za kiuchumi katika wilaya yetu ya Sikonge.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, watu 88 waliongelea changamoto ya maji ambao ni sawa na 13%. Pia 12% sawa na watu 81, waliongelea changamoto ya ujenzi wa zahanati, vituo vya afya pamoja na upatikanaji wa madawa. Hali kadhalika, watu 54 sawa na asilimia nane, waliongelea sekta ya elimu na hasa waliongelea juu ya umaliziaji wa majengo ya shule, uchakavu wa madarasa pamoja na upungufu wa walimu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wengine watu 34 waliongelea mambo mengine ikiwemo utawala bora, athari za wanyamapori, upatikanaji wa mbolea na hususan ya ruzuku, vilevile mawasiliano na hasa ujenzi wa minara ya simu, hicho ndicho nilichokiona huko jimboni kwangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikija sasa kuchangia hoja. Kwanza kabisa, wananchi wa Jimbo la Sikonge wanampongeza sana na wanamshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa mambo makubwa aliyowafanyia Wanasikonge. Sisi Wanasikonge ni wakulima, Mheshimiwa Rais amefanya jambo kubwa ambalo hatukulitarajia wala halikuwa katika ndoto zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa na shida ya mbolea, lakini Mheshimiwa Rais ametumwagia mbolea ya kutosha na isitoshe mbolea yenyewe kwa bei ya ruzuku, tunamshukuru sana. Kama haitoshi, sisi ni wakulima wa zao la tumbaku, kuna kipindi tumbaku iliyumba kwa sababu tulikosa masoko, lakini Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa. Ametutafutia masoko na sasa hivi tunauza tumbaku yetu kwa uhakika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, mliopo niwaambie tu msimu uliopita, zaidi ya shilingi bilioni 110 zimeweza kuingia pale Sikonge, tufanye nini sasa Wanasikonge? Kweli tarehe 29 Wanasikonge walijitoa kwa wingi na Mheshimiwa Rais amepata zaidi ya 98% kwenye Jimbo la Sikonge. Hizi 98% hazijaja kwa bahati nzuri, wala bahati mbaya, hapana. Ni kwamba yeye mwenyewe alizitafuta kwa sababu alifanya makubwa ndani ya Jimbo la Sikonge. Tunamshukuru sana na Wanasikonge wanampongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukija katika suala la maji, leo hii sisi kule Sikonge maji ya kutoka Ziwa Victoria yameingia. Bado kuna changamoto ndogo ndogo, lakini wataalam wanasema kwamba ifikapo Februari Wana-Sikonge wanapata maji ya uhakika kutoka Ziwa Victoria. Sasa Wanasikonge tuseme nini? Hivi tungeenda tukampe nani hizo kura kwa mambo haya mazuri aliyotufanyia? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala la umeme ndiyo usiseme, wachangiaji wamesema. Leo hii Mheshimiwa Rais anamalizia vitongoji vilivyobaki. Leo katika Jimbo langu la Sikonge nikichukua na hivi ambavyo ametupa sasa hivi siyo zaidi ya vitongoji 50, ndiyo vimebaki ambavyo havina umeme, na ninaamini hata kabla ya 2030 tayari vitongoji vyote vitakuwa vimepata umeme. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninarudia kusema tena, 98% aliyoipata haikuwa kwa bahati mbaya wala bahati nzuri isipokuwa alizitafuta yeye mwenyewe kwa kazi kubwa aliyoifanya. Tunamshukuru na tunampongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikija sasa kwenye tathmini hii. Kimsingi kinachoonekana hapa kwa wananchi wa Sikonge, changamoto kubwa namba moja waliyonayo ni barabara katika maeneo yao. Hata hivyo, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais, katika hotuba yake ukurasa wa 28 amesema waziwazi kabisa kwamba anaenda kuongeza bajeti na uwezo wa TARURA. Kwa hali hiyo, sisi Wanasikonge imetupa faraja kubwa sana kwa sababu hii ni changamoto kubwa sana katika eneo letu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu ni kwamba Jimbo la Sikonge ni kubwa, ni kubwa sana. Kuna kutoka Makao Makuu ya kata kwenda vijijini, kwa mfano, kutoka pale Sikonge uende Kijiji cha Igalula, ni zaidi ya kilometa 26 kwenda kwenye kijiji. Ni kubwa mno. Kimsingi ni kwamba Jimbo la Sikonge linalingana na baadhi ya nchi jirani. Hivyo tunaomba sasa, TARURA watakapokuja na Wizara, waje na formula, kanuni nzuri ambayo kwa kweli ile bajeti ita-reflect ule ukubwa wa jimbo na mtandao wa barabara.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana, ninawaomba sana ndugu zangu wa TARURA, ndugu zangu wa Wizara, hebu mjaribu kuliangalia hilo, mje na formula nzuri ili kusudi tuweze kupata ile bajeti kulingana na mtandao wa barabara jinsi ulivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo vilevile limewagusa sana Wana-Sikonge ni ufinyu wa maeneo ya shughuli za kiuchumi ikiwemo kilimo, ufugaji pamoja na urinaji wa asali. Ninamshukuru sana leo hii Mheshimiwa Naibu Spika pamoja na wizara kwa jibu lake zuri la Serikali kwamba Kamati ya Mawaziri imeshapewa hiyo kazi na imeshaifanya hiyo kazi, kinachosubiriwa sasa ni taarifa ili kusudi hawa wananchi waweze kuongezewa maeneo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninakuomba sana, Mheshimiwa Waziri Mkuu uko hapa, ninaomba sana ile kamati sasa itoe hiyo taarifa ili kusudi hawa wananchi waweze kupata hayo maeneo na hii migogoro midogo midogo ambayo inajitokeza iweze kwisha na watu waendelee na shughuli zao za kiuchumi. Tunaomba sana hilo kwa kweli, wafanye namna hiyo. Wakifanya namna hiyo, kwa kweli sisi hizi changamoto ndogo ndogo watakuwa wametuondolea kwa kiasi kikubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni jambo la maji. Kama nilivyosema hapo awali, tayari hivi sasa tunayo maji ya Ziwa Victoria. Ninawaomba tu ndugu zangu wataalamu na Serikali kwamba ijaribu sasa kuangalia kwa sababu tunaenda kwenye gridi ya Taifa ya Maji na kwa hivi sasa kuna kata tisa za awali katika Jimbo la Sikonge ambazo ndizo zitafaidika na huo mradi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba, kwa vile sasa zinakuja kuingia kwenye mfumo uliopo, kwenye mtandao wa maji uliopo, kwa kweli tunaamini kuna kata tatu zinaenda kufaidika, na yale maji ni mengi na yana pressure ya kutosha na miundombinu ipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninaamini kwamba Kata ya Usunga na yenyewe itafaidika, Kata ya Kiloleli na yenyewe itafaidika lakini vilevile na Kata ya Kipanga nayo itafaidika kutokana na huo mradi kwa sababu miundombinu ipo tayari. Maji yakishafika pale ni kuingia tu kwenye ile miundombinu, yanafika na kwenye hizo kata. Kwa hiyo, ni imani yangu kwamba badala ya kuwa na kata zile tisa, sasa tutakuwa na kata 12 na katika zile kata 20, tutabakiwa na kata nane ambazo sasa kwa bajeti ya kuchimba visima, ninaamini wananchi wa Sikonge tutawafikia kwa 100% hata kabla ya 2030.
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.
MHE. ENG. AMOSY W. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Madini kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. ENG. AMOSY W. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza nichukue nafasi hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia. Awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye ameendelea kutupa uzima na afya, hatimaye umefika muda na mimi niweze kutoa mchango wangu katika sekta hii ya madini.
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote niungane na Wabunge wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Madini pamoja na Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote ambao kwa kweli tumeona kazi kubwa wanayoifanya na kimsingi hakika wanaitendea haki hii Wizara ya Madini. Niseme tu wazi wazi kabisa kwamba Watanzania wanaona kazi wanayoifanya na macho ya Watanzania ndiyo macho ya Mungu. Kwa hiyo, Mungu anawaona jinsi wanavyofanya, waendelee kufanya kazi hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba Mheshimiwa Waziri, kwa kweli hotuba yak ni nzuri, ameeleza mambo mengi sana. Niombe tu Serikali iendelee kuwaunga mkono ili kusudi haya mambo mazuri tuliyoyaona, basi tuweze kuyaona kwa vitendo na hawa wachimbaji wetu wadogo basi wanaendelea kufaidika.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan alisema kwamba ametoa maelekezo kwamba, ifikapo mwaka 2034 angalau 80% ya Watanzania basi wawe wanatumia nishati safi ya kupikia. Kweli Wizara ya Madini hawajabaki nyuma, Wizara ya Madini wamelichukua hilo na leo hii tunaona kuna viwanda vinne vimejengwa vya kutengeneza mkaa unaotokana na makaa ya mawe. Viwanda hivi wamejenga Mbeya, Kisarawe, hapa Dodoma na vilevile kule Tabora. Sisi Wanatabora tumefarijika sana na ujenzi wa kiwanda hiki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wanatabora ni wakulima wa zao la tumbaku, tunakausha tumbaku yetu kwa moto. Tulikuwa na mashaka, Wanatabora walianza kuwa na mashaka kwamba je, miaka 10, 15 inayokuja itakuwaje? Tukizingatia kwamba miti iliyopo kule Tabora na hususan Sikonge, basi wana Sikonge ni kama supplier wa mkaa katika nchi hii, miti ilikuwa inakwisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunamshukuru Mheshimiwa Rais kumbe yeye alishaliona tayari na akatoa maelekezo kwa Wizara ya Madini kwamba waende wakajenge kiwanda pale Tabora. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa juhudi hizi ambazo wamezifanya. Hata hivyo, kiwanda kimekamilika na tayari kimeshazinduliwa, lakini mpaka hivi sasa bado hakijaanza kufanya kazi. Tunamwomba sana Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake, hebu kiwanda hiki kianze kufanya kazi basi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika msimu unaokuja tungependa kuona kwamba wakulima wa tumbaku katika Mkoa wa Tabora basi wanaanza kukausha tumbaku yao kwa kutumia haya makaa ya mawe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, ninaona elimu bado haijafika. Hebu wafike kule waende wakatoe elimu. Bado kuna wakulima wana mashaka mashaka kwamba yawezekana makaa ya mawe labda yanaenda kuwaongezea gharama ya uzalishaji. Wafike kule watoe elimu, wawaelimishe wananchi waweze kufahamu, ili kusudi huo mkaa uweze kupokelewa na wakulima wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe tu, ninaamini kwamba wameshafanya research ya kutosha, wameshafanya utafiti wa kutosha na wameshajua gharama za wakulima wa tumbaku wanatumia kiasi gani katika kuni na je, sasa gharama zenu wanazokuja nazo zinakuwaje? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe, suala la kutumia mkaa wa makaa ya mawe, ni suala la kimazingira. Niwaombe sana Wizara watumie lugha yoyote wanayoweza, ili kusudi wadau wa mazingira, wadau wa mazingira waweze kuingia pale na ikiwezekana basi kuwe na ruzuku ili kusudi gharama ya kutumia makaa ya mawe iwe ni chini zaidi ukilinganisha na gharama ya kuni wanazotumia. Hakika si kwamba tutasaidia mazingira, lakini vilevile kwa hawa wakulima wa tumbaku watakuwa wameongeza kipato. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwaombe sana ndugu zangu, hebu watufanyie hayo Wanatabora ili kusudi tuweze kuona kwamba kwa kweli Serikali ya Mama Samia imefanya kazi kubwa na imetusaidia sisi Wanatabora kwa ujumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikija kwenye upande wa madini, sisi watu wa Sikonge kweli hatuna madini mengi, lakini madini tunayo. Ukienda katika Kata ya Kitunda, tunayo dhahabu, lakini ukija jirani yake hapa panaitwa Kururu, madini ya dhahabu yamegundulika mahali hapo, lakini changamoto aliyoipata msemaji aliyetangulia pale mbele kwamba bado kuna changamoto kati ya TFS…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
NAIBU SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa Maganga muda wako umekwisha.
MHE. ENG. AMOSY W. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sana TFS na TAWA wamalize changamoto zao ili kusudi tuweze kufaidika na hayo madini.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. ENG. AMOSY W. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye sekta hii muhimu sana katika uchumi wa Taifa letu, ambayo ni Sekta ya Nishati. Ninaendelea pia kuipongeza sana Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambayo inaongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa jinsi ambavyo kwa ujasiri na uthabiti mkubwa, amejitoa kikweli kweli kabisa kuona kwamba, tunakuwa na mageuzi katika Taifa letu hili la Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi nchi yetu inaenda katika uchumi wa kati, uchumi wa viwanda. Ni uchumi ambao unahitaji sana sekta ya nishati kuwa imara, ndiyo hapo kwa hakika tutaweza kufika katika uchumi wa kati wa daraja la juu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawapongeza sana Wizara ya Nishati kwa kweli, wameleta mageuzi makubwa kweli kweli, kwenye sekta hii ya umeme. Ndugu zangu tukitaka kujua kwamba, hao watu wamefanya kazi kubwa hebu tuangalie tumetoka wapi, tuko wapi na then tuweze ku-project kuona kwamba, hao watu wanataka kutupeleka wapi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakumbuka mpaka mwaka 2007, takribani miaka 43 toka TANESCO imeanza, Mheshimiwa Prof. Muhongo amesema TANESCO imeanza mwaka 1964; nchi hii vijiji vyenye umeme vilikuwa 506 tu sawa na 4.1% ya vijiji vyote 12,318. Leo hii tunavyoongea vijiji vyote 12,318 tayari vina umeme na zaidi ya 61% ya vitongoji vyote 64,359 vina umeme. Leo tunaona mabadiliko makubwa ya kiuchumi na vilevile ya kijamii kule vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wakati tukiwa shuleni, nimesoma hapa Dodoma, tulikuwa tunasoma kwa kutumia vibatari, tena vibatari vyenyewe vya made by mimi, leo hii mpaka kule vijijini hawa vijana wetu wanasoma kwa kutumia umeme wa TANESCO. Kwa kweli, ni jambo ambalo inabidi tuwapongeze sana na huu umeme vijijini tunaona umeleta mabadiliko makubwa. Leo hii vijana wana shughuli za kiuchumi wanaziendesha kulekule vijijini, tunawapongeza sana kwa kazi kubwa hii mliyoifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke inawezekana miaka miwili, mitatu, hapo nyuma nikisema kero ninaona labda, kama hili neno ni dogo, tulikuwa na janga kubwa sana ndugu zangu Watanzania. Tulikuwa na kitu kinachoitwa mgao wa umeme, mgao wa umeme umetusumbua sana. Ulifanya hata uzalishaji wetu ukawa na changamoto nyingi kwelikweli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vyote vilijiendesha kwa shida na kufanya gharama za uendeshaji kuwa kubwa kwa sababu, walikuwa wanatumia umeme wa majenereta yanayoendeshwa kwa dizeli. Changamoto tulizopata zilikuwa ni kero kubwa kweli kweli, lakini leo hii ndugu zangu, binadamu tumeumbwa yale mambo mabaya huwa tunayasahau, habari ya mgao wa umeme tumeanza kuisahau tayari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haitoshi, tutakumbuka kwamba, uunganishaji wa umeme miaka mitano, mingapi kule nyuma, ilikuwa ni changamoto kubwa kwelikweli. Unakuta mwananchi amejenga nyumba yake vizuri, lakini kuunganisha umeme ilikuwa ni kazi, afadhali hata kujenga nyumba kuliko kuunganisha umeme; unaomba umeme inachukua miezi sita mpaka mwaka mzima bado hujaunganisha umeme. Leo hii ndani ya siku 10 mpaka 30 ukishaomba unaunganishiwa umeme, sisi wote hapa ni mashahidi. Haya ni mageuzi makubwa na ni mabadiliko makubwa kwelikweli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haitoshi, hata kazi za dharura unaenda kuripoti; miaka mitano iliyopita kule nyuma, unaripoti hapa kwangu, kwenye bomba kuna cheche zinatoka. Ilikuwa inachukua saa 24 mpaka 48 na wakati mwingine uzalendo unakutoka, unawatafuta vishoka wanakuja wanagongagonga pale, ili kuondoa tatizo uweze kuendelea na maisha, lakini leo hii ukiripoti ndani ya saa nne, sisi wote hapa ni mashahidi, tayari unaona vijana wamefika wamefanya kazi yako, maisha yanaendelea. Kwa kweli, ni jambo ambalo linahitaji kupongezwa kwelikweli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo tunajua TANESCO ilikotoka, walikuwa wanajiendesha kwa hasara, lakini mpaka hivi sasa TANESCO wanaenda kwa faida, tumeona wamerekodi faida ya takribani shilingi bilioni 500, jamani, hayo ni mageuzi makubwa, ndiyo. Waheshimiwa Mawaziri wanastahili pongezi na washikilie palepale kuona kwamba, Watanzania wanazidi kusonga mbele. Kubwa kabisa ndugu zangu Watanzania tusingependa sasa kuona tunarudi kule tulikotoka, tuhakikishe kwamba, haya mafanikio tuliyoyafikia tunayasimamia vizuri, ili kuona kwamba, haturudi tena kwenye mgao wa umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kusudi tusiweze kurudi kwenye mgao wa umeme tuhakikishe kwamba, Serikali inaendelea kufanya uwekezaji wa uhakika na hususani, kwanza kwenye matengenezo ya mitambo tuliyonayo. Lazima tuhakikishe kwamba, matengenezo yetu yanatengenezwa kulingana na specifications ambazo wataalam wametuwekea. Tukikosa hapo kuna uwezekano tukarudi kule nyuma, kitu ambacho kwa kweli, kitakuwa hakifai na hatutarajii kabisa kuona tunarudi huko. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo Mheshimiwa Profesa Muhongo amesema tuendelee katika uzalishaji wa umeme na sina sababu ya kurudia kwa sababu, Profesa ameeleza vizuri kwelikweli, lakini tuhakikishe kwamba, hizi megawatt 4,000, katika Taifa la Watanzania zaidi ya milioni 60 bado hazitoshi. Hata hizo megawatt 8000 kufika mwaka 2030 juhudi iendelee, bado haitoshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ameelezea mambo ya energy per capital. Energy per capital wenzetu wako mbali, sisi leo hii bado tuko chini ya kilowatt 300 kwa kila Mtanzania, ni kidogo sana hiyo. Kwa hiyo, tuhakikishe uzalishaji wetu unaendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo, ninarudi sasa upande upande wa REA. Ninaungana na wenzangu wote kupongeza sana taasisi yetu ya REA kwa kweli, wameendelea kufanya kazi nzuri. Leo hii tunaongelea kwamba, vijiji vyote 12,318 vimekwisha, 61% ya vitongoji vyote 64,359 vimekwisha na bado tunaendelea, kufikia mwaka 2030 tutakuwa na 100%, lakini hili linaweza vilevile likatu-take by surprise tukasema kwamba, labda yawezekana kazi ya REA inakwisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema hivi kama ni kazi ya REA sasa ndiyo inaanza kwa sababu, wahenga wetu walituambia, walitufundisha kwamba, kuzaa mtoto siyo kazi, kazi kubwa ni kumlea. REA wametuzalia mtoto; sasa je, huyu mtoto apate kwashakoo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa ninaangalia katika kipindi hiki kifupi katika ule mtandao wa umeme wa msongo wa kilovoti 33 ambao TANESCO wanaumiliki, takriban kilomita 80,000 REA wamechangia zaidi ya kilomita 38,000. Huu mtandao si kitu chepesi ni kitu kikubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tumeona njia za umeme za three phases zimekuwa ni kubwa sana. Mradi wa gridi imara tunaomba kwa kweli, usimamiwe kwa nguvu zote kwa sababu, kweli pamoja na mambo mazuri haya, lakini bado kuna changamoto ya kukatika kwa umeme kwa sababu, mtandao wa three phases umekuwa mrefu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo kuwa na mtandao wa kilomita 80,000 na kwa REA pekee yake 38,000 kwa kipindi kifupi hiki maana yake ni nini? Maana yake mtandao wa kilomita 38,000 ni zaidi ya nguzo 400,000 zimeweza kuingia kwenye system kwa muda huu mmoja. Maana yake ni kwamba, hizi nguzo zimetengenezwa kwa teknolojia moja, kwa spec moja. Maana yake ni kwamba, zitazeeka pamoja na kuna uwezekano zitakufa pamoja. Sasa ni lazima hilo tulione kwamba, ok, sasa tunaenda wapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, yanaweza yakatokea majanga kwamba, leo umekaa hapo unasikia kwa watani zangu kule Pwani nguzo 800 zimeanguka, hujakaa sawa unaambiwa hapa Dodoma zimeanguka 600, hujakaa sawa unaambiwa kule Kagera zimeanguka 200. Hilo litakuwa ni janga, tuanze kuliangalia na kuona tunaenda namna gani na ndiyo maana nimesema kwamba, kama ni kazi ya REA, sasa kazi yake ndiyo inaanza. Hakika tufanye kila linalowezekana, kama kuna uwezekano tuwaongezee hata bajeti, ili waanze kazi ya kumlea huyu mtoto kusudi aweze kuwa na faida katika Taifa la Tanzania.
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Mheshimiwa Engineer Amosy William.
MHE. ENG. AMOSY W. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na ninaomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. ENG. AMOSY W. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kwanza nichukue nafasi hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuwa mmoja wa wachangiaji katika Wizara hii muhimu sana Wizara ya Kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna mashaka na wala hakuna wasiwasi wowote kwamba ni kweli tunapokwenda ni kuzuri na tukizingatia kwamba kweli Wizara yetu ya Kilimo imepata watu shupavu ambao tunaona kwa kweli wanatupeleka kule ambako Watanzania tunakutaka.
Mheshimiwa Naibu Waziri, hivyo nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, lakini nimpongeze sana Naibu Waziri wa Kilimo, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu pamoja na Watendaji wote kwa kazi nzuri wanazozifanya. Kazi wanayoifanya inaonekana Watanzania tunaiona, wanafanya kazi mbalimbali hasa tunaona wanavyohangaika katika utafutaji wa masoko, tunawapongeza sana. Sisi wakulima wa tumbaku soko letu liliyumba, lakini chini ya uongozi wa Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan tunaona masoko ya tumbaku yanapatikana, hivyo tunawapongeza sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaona kazi nzuri za tafiti wanazofanya, wanafanya tafiti kwenye mbegu, viuatilifu pia kwenye afya ya udongo. Niseme kwamba waongeze kasi katika afya ya udongo. Tuna matatizo makubwa sana katika maeneo mbalimbali ya nchi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kule kwetu Sikonge Waziri ni vigumu sana sasa hivi kupata angalau magunia 10 ya mahindi kwa ekari moja ni kazi kubwa kwelikweli. Pamoja na kwamba utatumia input zote, utatumia mbolea zote, mbolea ya kupandia, mbolea ya kukuzia pamoja na kuzalishia na taratibu zote za kilimo umezifuata, lakini imekuwa changamoto kwelikweli kupata hata gunia 10. Tunaomba hili kwa kweli lifanyiwe kazi kubwa ili kusudi suluhu ya afya ya udongo iweze kupatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi zote hizi kwa Wizara ya Kilimo, lakini nilete sauti ya wakulima wa tumbaku hapa Tanzania hususani wakulima wa zao la tumbaku Wilayani Sikonge. Kwa kweli kitendo cha bei ya tumbaku kushuka na wakati uleule bei ya mbolea kupanda kimeleta mkanganyiko mkubwa sana kwa wakulima wa zao la tumbaku hapa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, msimu uliopita bei ya tumbaku kwa wastani ilikuwa ni dola 2.559. Hii siyo kwamba wastani huu ulipatikana Sikonge, hapana ni kwa nchi, hii ni kwa taarifa ya Wizara. Ukienda kwenye randama ukurasa wa 44, tani zilizouzwa zilikuwa tani 185,772 na fedha zilizopatikana zilikuwa milioni 475 plus. Ukichukua hiyo ukagawa unapata wastani wa dola 2.559, wakati huo mfuko wa mbolea ya NPK tunayoitumia ilikuwa ni dola 60.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa msimu huu mfuko wa mbolea umekwenda mpaka dola 63.89 wakati bei ya tumbaku kwa wastani ni dola 1.95, hili ni anguko kubwa sana kwa wakulima wa tumbaku.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimependa sana dhima ya Wizara katika mambo mengi ambayo yamewekwa kwenye hiyo dhima, lakini kuna sentensi moja inasema kuboresha maisha ya Watanzania. Kweli tuendee kuyaboresha maisha ya Watanzania, lakini huu msukosuko wa bei kupanda na kushuka ninadhani ni vizuri tuangalie kama tunataka kuona kwamba kweli tunaboresha maisha ya wakulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa najaribu kuangalia kwa nini bei ya mbolea imepanda namna hii. Nimejaribu kupitia maandiko mbalimbali, nikaja kuona kwamba bei ya kuzalisha kilo moja ya NPK ya mbolea pale Zambia ni wastani wa Kwacha 17,500 kwa tani. Kwacha moja ni sawa na dola 0.053, ukizidisha 0.053 kwa hiyo 17,500 unapata wastani wa kuzalisha tani moja ya mbolea ya NPK kule Zambia ni takribani dola 972 na point. Sasa ukizigawanya zile kwa mifuko 20 ambayo ndiyo tani moja unapata wastani wa dola 46.375.
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Maganga, ahsante sana, malizia sentensi ya mwisho.
MHE. ENG. AMOSY W. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sana kwamba, Serikali iangalie namna ya kupunguza hizo tozo ambazo ni nyingi sana, kwa sababu toka 46 mpaka 63 ni hela nyingi sana. Tunaomba wapunguze ili kusudi wananchi waweze kupata tija.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. ENG. AMOSY W. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Kabla sijaanza mchango wangu ninaomba, kwanza nilete salamu za wananchi wa Mji wa Sikonge wenye kata mbili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi hawa kupitia kwa Madiwani wao, Mheshimiwa Joyce Ng'amba wa Kata ya Mishen na Mheshimiwa Hamisi Saidi Kumba wa Kata ya Sikonge, wanaleta shukrani zao za dhati na za upendo kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kazi kubwa aliyoifanya ya kuwaondolea kero ya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi hawa sasa wanapata maji ya uhakika kutoka Ziwa Victoria. Wanachokiomba sasa ni Mheshimiwa Rais aweze kufika kule Sikonge, ili yeye mwenyewe aweze kuuzindua huo mradi. Mwisho wa shukrani hizo kutoka kwa wananchi wa Sikonge, ninaomba sasa ili niweze kutoa mchango wangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, ninaanza kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya. Leo tunavyoongea wananchi wa Sikonge takribani 68% tayari wana miundombinu na vilevile wana maji. Kuna changamoto ndogondogo ambazo zipo kule, wakati mwingine maji hayatoki kama jinsi ambavyo wanavyotaka, lakini tunasema safari ni hatua. Ninaamini kuna siku wananchi wote wa Skonge watapata maji ya uhakika, saa 24 kwa siku saba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza sana vilevile Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri. Ninakushukuru sana Mheshimiwa Waziri amefika kule Sikonge akashuhudia tone la kwanza la maji yaliyotoka Ziwa Victoria, ambayo ndiyo mwanzo wa Gridi ya Taifa. Ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri na Watendaji wote wa Wizara ya Maji, ninawapongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huu Mradi wa Maji kutoka Ziwa Victoria umepita, lakini ninamwambia Mheshimiwa Waziri kwamba, kuna kata takribani tisa ambazo ziko ndani ya kilometa 12. Nilipopita wakati ninamwombea kura Mheshimiwa Rais, pamoja na mimi mwenyewe na Madiwani, niliwaambia kwa uthabiti na kwa ujasiri kwamba, wasiwe na wasiwasi Mheshimiwa Mama Samia atawaletea maji kwa sababu, bomba linapita hapo katikati yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata hizo ni pamoja na: Pangale, Mpombwe, Igigwa, Kisanga, Tutuo, Mole, Mkolye, Chabutwa pamoja na Kata ya Ipole, hawa wananchi toka juzi wananipigia simu, tena wengine kwa machozi kabisa na nikawaambia machozi yenu ninayabeba na nitayafikisha kwa Mheshimiwa Aweso na ninaamini Waziri atakapokuwa ana-wind up atakuwa na jambo la kuwaambia wananchi hao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, …
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. ENG. AMOSY W. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nimeshachangia kwa maandishi utayaona, basi ninaunga mkono hoja. (Makofi)