Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Eng. Amosy William Maganga (2 total)

MHE. ENG. AMOSY W. MAGANGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Barabara ya Ipole – Rungwa na Sikonge – Kipili kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Amos William Maganga, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami wa Barabara ya Ipole – Rungwa inayounganisha Mikoa ya Tabora na Mbeya umekamilika. Kwa sasa Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Barabara ya Sikonge – Kipili Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Baada ya Usanifu kukamilika, Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi. Ahsante.
MHE. ENG. AMOSY W. MAGANGA aliuliza: -

Je, lini maji ya Ziwa Victoria yataanza kusambazwa katika Kata za Pangale, Mpombwe, Igigwa, Kisanga, Tutuo, Mkolye, Chabutwa na Ipoje?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maji ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Mhandisi Amosy William Maganga, Mbunge wa Jimbo la Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na utekelezaji wa Mradi wa Maji wa Miji 28 kwa kutumia maji ya Ziwa Victoria kutoka Tabora kwenda katika Wilaya za Sikonge, Urambo na Kaliua mkoani Tabora kwa gharama ya shilingi bilioni 143.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa kazi zinazotekelezwa kupitia mradi huo ni pamoja na ulazaji wa mabomba umbali wa kilometa 253 sambamba na ujenzi wa matanki tano yenye jumla ya ujazo wa lita milioni nane yakiwemo matanki mawili yenye ujazo wa lita milioni tatu yaliyojengwa katika maeneo ya Tumbili na Misheni, wilayani Sikonge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huo umefikia wastani wa 76.5% za utekelezaji na umeanza kutoa huduma kwenye baadhi ya maeneo ya Mji wa Sikonge wakati utekelezaji ukiendelea. Mradi huo unatarajiwa kukamilika mwezi Julai, 2026 ambapo Serikali itafanya usanifu wa kufikisha huduma ya maji kupitia mradi huo kwenye maeneo ya pembezoni umbali wa kilometa 12 kutoka bomba kuu ikiwemo Kata za Pangale, Mpombwe, Igigwa, Kisanga, Tutuo, Mkolye, Chabutwa na Ipoje.