Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Cornel Lucas Magembe (1 total)

MHE. CORNEL L. MAGEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nina swali moja la nyongeza. Kuna vijiji takribani vitano katika Jimbo la Chato Kaskazini, ambavyo ni Vijiji vya Mkungo, Nyakato, Buzirayombo, Itale na sehemu kubwa ya Ilyamchele. Vijiji hivi havipati mawasiliano kwa sababu hakuna mtandao na hii husababisha utoaji wa elimu hasa kwenye shule za msingi na Sekondari ambako sasa wanatumia TEHAMA wanafunzi wanashindwa kupata haki yao kama wanafunzi wengine. Je, Wizara ina mpango gani wa kwenda kuweka mtandao katika maeneo hayo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kujibu swali la ndugu Mheshimiwa Magembe, Mbunge wa Chato Kaskazini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoeleza katika jibu la swali la msingi, tunatambua changamoto ya mawasiliano nchi nzima na ninaamini kila Mbunge aliyemo katika jengo hili ana changamoto ya mawasiliano katika Jimbo lake kwenye sehemu moja au nyingine. Ndiyo maana sisi kama Wizara tunaandaa mkakati wa miaka mitano wa kuyafikia maeneo yote yenye changamo ya mawasiliano na tunaamini katika kipindi hiki cha miaka mitano, tutafika kila eneo kule ambako hakuna minara, tutajenga minara mipya, kule ambako minara imezidiwa, tutaiongezea nguvu ili kuhakikisha kwamba ifikapo mwaka 2030 changamoto ya mawasiliano katika Majimbo mbalimbali na hapa nchini iwe imepungua kwa kiasi kikubwa au tumeimaliza kabisa. (Makofi)