Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. John John Nchimbi (1 total)

MHE. JOHN J. NCHIMBI aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Kiwanda cha kukoboa Kahawa Nyasa kama alivyoahidi Mheshimiwa Rais?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, ninaomba nijibu swali namba 79 la Mheshimiwa John John Nchimbi, Mbunge wa Nyasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Nyasa inazalisha kahawa aina ya Arabica kwa wastani wa tani 2193 kwa mwaka. Kutokana na uzalishaji huu, Mheshimiwa Rais aliona umuhimu wa kuwa na kiwanda katika eneo hili. Hivyo, Serikali kupitia Halmashauri ya Nyasa imetenga eneo lililopo Kitongoji cha Ndanda, Kijiji cha Kingirikiti Kata ya Kingirikiti kwa ajili ya ujenzi wa kiwanda cha kukoboa kahawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili lina ukubwa wa hekta nne na lina miundombinu wezeshi kama vile barabara, maji na umeme. Aidha, eneo hili linamilikiwa na Serikali na lipo tayari kwa ajili ya uwekezaji kwa kujenga kiwanda cha kukoboa kahawa. Serikali inaendelea kuhamasisha wawekezaji kwa ajili ya kujenga kiwanda cha kukoboa kahawa katika eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kuwasilisha.