Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Ado Shaibu Ado (2 total)

MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kuniona. Kwa vile tatizo hili la tembo kuvamia vijiji na kuharibu mazao, kuuwa binadamu ni tatizo kubwa sana katika Jimbo la Tunduru Kaskazini na Wilaya ya Tunduru kwa ujumla wake. Ambapo kwa msimu wa kilimo wa 2025/2026 peke yake jumla ya waathirika 1791 wameharibiwa mazao yao na askari wa vijiji mpaka sasa wako 23 tu. Je, ni lini Serikali italipa fidia kwa waathirika wote na kuongeza idadi ya askari wanyamapori wa vijiji (VGS)?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tayari Serikali imeshaweka fedha na zimeshaingia na sasa tunafanya utaratibu wa kulipa kupitia mfumo. Kilichochelewesha ilikuwa tunalipa manual, unaenda kijijini unaenda kulipa, pengine unaenda kulipa milioni tano unatumia gharama ya milioni nne, lakini kwa sasa tunatumia mfumo na mfumo huu umetuwezesha. Nimwombe tu Mheshimiwa Mbunge awe na subira hawa watu wetu watapata malipo yao.
MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona ili niulize swali dogo la nyongeza. Mbunge wa Tunduru Kusini Mhandisi Fadhili Chilombe, ninafahamu kwamba ameleta hoja na kufuatilia mara nyingi Wizara ya TAMISEMI juu ya haja ya kuigawanya Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru kupata Halmashauri mbili na mchakato wetu ulifika mpaka RCC, tuna watu zaidi 400,000 na tuna kilometa za mraba 18,000.

Mheshimiwa Spika, tunataka kauli ya TAMISEMI ili Watanzania wanaoishi Tunduru wapate kauli ya Serikali ndani ya Bunge. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO): Mheshimiwa Spika, kama nilivyotangulia kujibu kwenye jibu la msingi, uanzishwaji wa mamlaka za kiutawala ikiwemo hili analoliongelea Mheshimiwa Mbunge, Ado Shaibu, Mwenyekiti wetu wa Kamati ya LAAC unazingatia Sheria ile ya Uanzishwaji ya Mamlaka za Wilaya, Sura Na. 287 pamoja na Sheria ya Uanzishwaji wa Mamlaka za Miji, Sura 288.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetoa maelekezo na ushauri kwa Halmashauri ya Kibaha, vivyo hivyo wananchi wa Tunduru wafuate utaratibu huo na TAMISEMI kazi yetu ni moja tu kufanya tathmini na mapitio kama vigezo vimezingatiwa. (Makofi)