Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Kija Limbu Ntemi (1 total)

Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. KIJA L. NTEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ili niweze kuchangia. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa sababu ndiye aliyetufanya na kutupa uhai mpaka kufika siku ya leo tuko hapa tumesimama tunazungumza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nataka nisome kidogo maandiko Matakatifu. Warumi 13:1 ili kuonesha kwamba Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa nini yupo amekaa pale kwenye kile kiti, Biblia yangu inasema kwamba, “Kila mtu na atii mamlaka iliyo kuu, kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu, na ile iliyopo imeamriwa na Mungu.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dkt. Samia Suluhu Hassan ni chaguo la Mwenyezi Mungu, ndiyo maana amemuweka pale. Hata sisi ambao tumefika humu siku ya leo, nasi pia tumepitishwa na Mwenyezi Mungu kupitia vyama vyetu, ndiyo maana tumefika humu na tunazungumza katika Bunge hili Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza Makamu wa Rais Emmanuel Nchimbi kwa kuchaguliwa kupitia Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye alikuwa mgombea naye kuwa Makamu wa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninampongeza Spika wa Bunge, ninakupongeza na wewe Naibu Spika Daniel Sillo kwa kuchaguliwa kuwa Naibu Spika katika Bunge hili kwa kura nyingi 100% nadhani zote zilipatikana. Ninampongeza pia Dkt. Mwigulu Nchemba kwa kuchaguliwa kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama hapa pia kuwapongeza wananchi wa Katoro walionichagua kuwa Mbunge au mwakilishi wao walionipigia kura nyingi za kutosha ili niwe Mbunge wao katika Jimbo la Katoro. Mimi ni Mbunge wa Jimbo la Katoro ninayeongoza wananchi wote, wawe wa upinzani wawe wa chama gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ndiye Mbunge wao na mimi niko tayari kufanya nao kazi kwa namna yoyote ambayo tutaongozwa na kwa sababu tuna Rais jemedari kabisa, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan tutawatumikia wananchi wote wa Katoro wa vyama vyote na wa itikadi zote ambazo zipo katika Jimbo la Katoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze kwenye mambo machache. Jambo la kwanza nizungumzie suala la madini. Ninaomba kupendekeza jambo moja kwa Wizara ya Madini, kama itawapendeza, tufike hatua basi turuhusu wachimbaji wetu ambao wapo wa kati na wadogo, kama inawezekana kutunza mali zao katika Benki ya BoT au benki ny,ingine watunze na kuweza kupata mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, sasa ungekuwa umetunza mali kuanzia mwezi wa Kwanza au mwezi wa 12, leo mchimbaji mdogo angeuza kwa fedha nyingi sana kwa soko ambalo lipo kwa siku ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napendekeza benki zetu zitoe nafasi au fursa ya kutunza mali katika benki zetu. Kama mtu anao mtaji wa kutosha na hahitaji kuuza mali yake kwa siku hiyo, aweze kuitunza iwe akiba na akihitaji kuchukua fedha benki, apatiwe nafasi ya kuchukua fedha benki kwa dhamana ya mali aliyoiweka benki katika benki zetu ili imsaidie kufanya maendeleo na kupiga hatua nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawapongeza Wizara ya Nishati ambao hata mimi ni mnufaika wa umeme ambao sasa nitakwenda kupata kaya 4,151 zinakwenda kuwashiwa umeme. Ninawapongeza Waziri wa Nishati pamoja na Naibu wake ambao wamekubali hata kwenye nyumba za matope wanakwenda kuwasha umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwetu kule Katoro kuna nyumba nyingi. Nimemwambia Naibu Waziri Salome Makamba aje atuwashie umeme kwenye zile nyumba ambazo ni za matope kwa sababu ni haki ya wananchi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwashiwa umeme katika maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ametujengea shule nzuri nyingi na mahiri Katoro. Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Profesa Shemdoe alifika akashuhudia shule nyingi za kisasa ambazo zimejengwa Katoro kwa fedha za Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Wale ambao hawajaona shule nzuri, njooni mshuhudie Katoro, kuna shule nzuri ambazo amejenga Rais ambazo ni bora na imara zinazotoa mafunzo kwa wanafunzi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe tu jambo moja, tunapoelekea katika mipango hii na kusaidia vijana wetu, kuna vijana ambao wako mtaani, wengine wamemaliza shule, lakini baadhi ya vijana hao hawajapata vyeti vyao, vipo chuoni mpaka leo, lakini wapo wanazurura mtaani. Wengine wameanza kujiajiri. Mmoja nimemkuta anafanya kazi ya car wash, lakini amemaliza chuo ni kijana mzuri na ni mwalimu, anakwambia sina cheti cha form four na cha chuo viko wapi? Viko chuo vimeshikiliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sijui Wizara imejipangaje kusaidia hawa vijana ili wapatiwe vyeti vyao. Wanapoomba ajira wanaambiwa mpaka uende na cheti original, anakitoa wapi cheti original? Cheti original kiko chuoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoenda na mipango hii tukumbuke kuna vijana ambao vyeti vyao hawana, lakini wanataka ajira. Ndiyo hawa ambao tunawaona kila siku huenda wanatangatanga kutafuta ajira, lakini ajira hawapatiwi kwa sababu hawana vyeti katika maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea tu kupongeza na kusema kwamba, tunapoendelea kujipanga na huu mpango wetu niwakumbushe Wizara ya Fedha pamoja na Waziri wa Mipango, sisi Katoro tuna uvuvi mkubwa sana, tunahitaji tungepata viwanda vya kuchakata Samaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile viwanda vinavyochakata samaki ili kuwasaidia wananchi wetu wanapovua samaki, maana tuna samaki wengi sana. Katika Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi imeeleza, kupata kiwanda kimoja cha samaki, mtusaidie ili wananchi wetu waweze kufanya biashara nzuri wanapokwenda kuuza bidhaa zao katika maeneo hayo ya viwanda ili waweze kusaidiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo ninapenda kulizungumzia ni hili jambo ambalo ni kama tu la kupongeza sasa. Tunamshukuru Rais mambo ambayo ameyafanya; ukisikia mtu anayesema Mheshimiwa Dkt. Samia hajafanya; Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan alipatiwa hii nchi na mtangulizi wake Mheshimiwa Hayati Dkt. Magufuli akiwa ameacha Daraja la Busisi kwa asilimia ndogo sana kukamilika, lakini leo sisi tunaotoka Katoro, tunaotoka Geita, tunapita pale kwa dakika tatu tu, na huyu ndiye Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyekamilisha daraja hili. Leo tunavuka kwa kishindo kikubwa tukitokea Geita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tunakaa masaa matatu, mpaka manne, mama huyu aliachiwa daraja hili likiwa lina asilimia kama 20, leo limekamilika. Tumpongeze, tumtie moyo, tumtie shime, tumuunge mkono, tushirikiane naye ili aweze kutuongezea, aweze kutusaidia kutuvusha mpaka kufika 2030, tuweze kupata maendeleo makubwa katika sehemu zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)