MHE. CHARLES M. NJAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi. Kwanza naanza kwa kumshukuru Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametuletea pesa wiki iliyopita shilingi bilioni 1.4, kwa ajili ya ukarabati wa Hospitali yetu ya Magunga. Hospitali ya Magunga imezeeka sana, imechakaa na ina umri karibu miaka 73 sasa. Je, Mheshimiwa Waziri yupo tayari twende pamoja katika hospitali ile, kwa ajili ya kufanya tathmini, ili ikiwezekana tufikirie kujenga majengo mapya badala ya kuendelea kuweka viraka katika hospitali ile, ambayo inakuwa ni gharama kubwa zaidi kwa Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. JAFAR R. SEIF): Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Charles, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi pamoja na timu ya wataalam tutaongozana pamoja na Mheshimiwa Mbunge kwenda kwenye hospitali hiyo kufanya tathmini na kuendelea kuboresha miundombinu ya hospitali hiyo. (Makofi)
MHE. CHARLES M. NJAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, Ninashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina swali moja la nyongeza. Je, kilomita 2.45 za kutoka Korogwe Girls – Stesheni zitafanyiwa upanuzi ili kuendana na ujenzi wa barabara mpya kutoka Old Korogwe – Kwamndolwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nimjibu Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, tunapoanza hii barabara ni kuanzia Old Korogwe – Kwamndolwa. Nimwelekeze Meneja wa Mkoa wa Tanga kwamba kwa kuwa hii barabara inaenda Korogwe Girls waende wakaiangalie na kuona kama imefanyiwa usanifu ama kama haijafanyiwa usanifu iweze kufanyiwa usanifu ili tuweze kuunga hizo kilometa 2.5 kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)