MHE. TIMOTH G. ANYOSISYE aliuliza:-
Je, lini Serikali itajenga kingo za zege za Mto Mbezi ili kuzuia kusombwa kwa nyumba na kusababisha maafa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI, Profesa Shemdoe. Ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Timoth Geofrey Anyosisye, Mbunge wa Kawe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Mto Mbezi ni mto muhimu Jijini Dar es Salaam. Wakati wa msimu wa mvua mto huu huongezeka kina na mara nyingi husababisha mafuriko yanayoathiri miundombinu na makazi ya watu yaliyo kando ya kingo zake.
Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali inakamilisha utaratibu wa kumpata mtaalam mshauri atakayefanya kazi ya usanifu wa kina kwa lengo la kujua gharama halisi za ujenzi wa mto huo. Baada ya gharama halisi kufahamika itatenga fedha kwa ajili ya kutekeleza ujenzi wa kingo za mto huo.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Serikali inatambua uwepo wa Mto Nyakasengwe pamoja na Mto IPTL. Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI namwelekeza Meneja wa TARURA, Mkoa wa Dar es Salaam, pamoja na Mratibu wa Mradi wa DMDP II, wapitie mito hiyo miwili iliyoongezeka kwenye swali la Mheshimiwa Mbunge waweze kuona uhalisia na sisi, kama Serikali, tuone namna ya Kwenda nalo.