MHE. TIMOTH G. ANYOSISYE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tarehe 29 Oktoba, 2025 Jimboni Kawe vilichomwa Vituo vya Polisi vitatu. Kwetu sisi Wanakawe jambo hili tunalichukulia kama jambo la dharura. Je, ni lini Serikali itajenga vituo hivi ili kurejesha hali ya huduma ya kipolisi katika maeneo husika?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ruhusa yako na kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, ninaomba nimjibu swali lake Mheshimiwa Timoth kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tarehe 29 Oktoba, 2025 kulitokea uharibifu wa mali mbalimbali za Serikali ikiwepo baadhi ya Vituo vya Polisi katika baadhi ya maeneo. Ninaomba nimwambie Mheshimiwa Timothy kwamba Serikali inaendelea kukamilisha kazi ya tathmini na kuja na mpango wa dharura wa kuona namna gani ya kuweza kurejesha huduma kwenye maeneo husika. (Makofi)