Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon Tamima Haji Abass (3 total)

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. TAMIMA HAJI ABASS: Mheshimiwa Spika, awali ya yote naanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kila jambo, pia aniwezeshe kutoa mchango wangu kwa ufasaha.

Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru wewe pamoja na kukupongeza kwa namna unavyoliongoza Bunge letu tukufu, hakika wewe ni Spika wa viwango, Mwengezi Mungu azidi kukumulikia mwanga wa mafanikio, wewe ni hazina kubwa ya nchi yetu. Hakika Mungu amekuibua kwa sababu, kwani Taifa linahitaji mtu kama wewe wakati huu. Pia nampongeza Naibu Spika pamoja na Wenyeviti wa Bunge kwa namna wanavyoliongoza Bunge letu tukufu.

Mheshimiwa Spika, nikiendelea, nachukua fursa hii kwa dhati ya nafsi yangu kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, pia nampongeza kwa namna ambavyo anaiendesha nchi hii.

Mheshimiwa Spika, nampongeza Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa anavyotuongoza. Pia nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa uongozi wake na moyo wake wa kuwatumikia wananchi. Nampongeza Mheshimiwa Mwigulu Nchemba - Waziri wa Fedha na Mipango pamoja na Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara na viongozi wote wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata nafasi ya kutoa mchango wangu kwa njia ya maandishi kwenye hoja hii ya Bajeti Kuu ya Serikali. Naipongeza Serikali kwa bajeti nzuri ambayo inatoa faraja na matumaini mema kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwa kuendelea nauelekeza mchango wangu kwenye madawati ya jinsia; naipongeza Serikali kwa kuona umuhimu wa kuweka madawati ya jinsia nchini. Madawati haya lengo lake kubwa ni kuwasogezea huduma karibu wananchi wanaopata changamoto za kifamilia zikiwemo, udhalilishaji, ubakaji, ukatili, utelekezaji wa watoto pamoja na wanaokinzana na sheria.

Mheshimiwa Spika, madawati haya kama yalivyoundwa ipo haja ya kuyafanya yaweze kufanyakazi kama ikivyokusudiwa, kwani kinyume chake itakuwa ni kuzidisha changamoto badala ya kupunguza. Baadhi ya madawati haya yanakabiliwa na ukosefu wa vitendea kazi kama vile usafiri, kompyuta, karatasi, vifaa kwa ajili ya kuchezea na kutuliza akili za watoto wakati wa kuhojiwa na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, kukosekana kwa vitendea kazi hivyo vinachelewesha au kukwamisha kushughulikia mashauri yanayopelekwa na kupelekea wananchi kuona hakuna haja ya kwenda kwenye dawati, pia hupelekea wananchi kuchoka wakati mwingine wanakosa hata nauli pale inapotokea kuitwa mara nyingi.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali kuweka mkakati maalum wa kuyawezesha madawati haya kwani ni mkombozi wa wananchi wanyonge wanaopata unyanyasaji hasa vijijini.

Mheshimiwa Spika, naipongeza sana Serikali kwa kazi kubwa inayofanya, pamoja na kazi kubwa inayofanywa wapo watu wanambeza na kumsema vibaya Rais wetu, hii sio sawa kabisa hasa kutumia ukabila, udini au anakotoka. Rais wetu hana ubaguzi kwa nini yeye abaguliwe. Naiomba sana Serikali kutunga sheria ya kumlinda Rais dhidi ya watakaomsema vibaya.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo machache naunga mkono hoja.
Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2023 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. TAMIMA HAJI ABASS: Mheshimiwa Spika, naomba kuchukua nafasi hii kutoa mchango wangu kwa njia ya maandishi katika Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2024/2025 iliyowasilishwa mbele ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, naishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada kubwa inayochukua katika kuleta maendeleo kwa wananchi wake.

Mheshimiwa Spika, pia nampongeza Waziri wa Mipango na Uwekezaji kwa kuja na mpango wa maendeleo pamoja na Waziri wa Fedha kwa kuwasilisha bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2024/2025, bajeti ambayo ni nzuri na mkombozi wa mwananchi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na uzuri wa bajeti hiyo haitakuwa na thamani yoyote iwapo utekelezaji wake hautapewa umuhimu kwa maana ya watendaji ambao ndio watekelezaji wafanye kazi kwa bidii kuhakikisha wanakamilisha kazi walizopangiwa.

Mheshimiwa Spika, vilevile Wizara ya Fedha ina wajibu wa kuzipatia fedha walioomba Wizara za Kisekta ili waweze kukamilisha shughuli walizozipanga, iwapo Wizara hazikupatiwa fedha zote na kwa wakati ni wazi kwamba malengo hayatoweza kufanikiwa.

Mheshimiwa Spika, naendelea na mchango wangu kwenye eneo la kuchangia pato la Serikali na nazungumzia eneo la mazingira. Serikali ijenge viwanda vikubwa vya kuchakata taka na kuzalisha mbolea ambayo tutatumia nchini pia tutauza nje na kupata fedha za kigeni.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tunazalisha taka nyingi ambazo zimekuwa kero kwa kuchafua mazingira na kusababisha maradhi ya mllipuko, tukumbuke kuwa kila kiumbe nchini kinazalisha taka, hivyo changamoto hiyo tuigeuze kuwa fursa.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu; kwanza, kupitia halmashauri zetu uwekwe mkakati maalumu wa kukusanya taka kwenye masoko yote; pili, kuwa na mkakati maalumu wa kukusanya taka majumbani; tatu, kuwa na mkakati maalumu wa kusafisha mitaro ya maji machafu; nne, kuwa na utaratibu maalumu wa kusafisha fukwe; tano, kitengo cha kukusanya taka kwenye halmashauri zetu kiimarishwe kwa kupatiwa vifaa vya kisasa na sita, wawepo wakaguzi wa kila siku kukagua usafi wa masoko. Hii itasaidia maeneo yetu kuwa safi, pia kupata malighafi ya kutengeneza mbolea.

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2024 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026
MHE. TAMIMA HAJI ABASS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi mchana huu wa leo kuchangia hotuba ya bajeti na hoja zilizoletwa hapa mbele ya Wizara ya Fedha pamoja na Mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kila kitu aliyenijaalia uhai, afya, nguvu katika muda huu wote wa maisha yangu. Pia ninawashukuru wote wale walioniunga mkono na kunisaidia katika kuniongoza mpaka nikaingia ndani ya Bunge hili Tukufu, vilevile Waheshimiwa Wabunge wenzangu walionipokea mwaka 2022, wakanifundisha, wakanielekeza mpaka muda huu ninawashukuru Wabunge wenzangu nyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ninampongeza Dkt. Mwigulu Nchemba, ninampongeza kwa hotuba hii aliyoiwasilisha hapa ambayo inatuonesha kwamba nchi yetu itakwenda kuwa na mafanikio makubwa baada ya utekelezaji wa bajeti hii. Vilevile ninampongeza Profesa Kitila Mkumbo kwa kutuwekea mpango madhubuti ambao utakwenda kutekelezwa sambamba na bajeti hii katika kipindi hiki cha mwaka wa fedha 2025/2026.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawapongeza pia wasaidizi wenu Mheshimiwa Chande, ninampongeza pia Mheshimiwa Nyongo, wote hawa kwa umoja wao wameweza kushirikiana wakaweza kutuletea mpango na bajeti hii ambayo ni mkombozi wa wananchi, hakika itakwenda kuwakomboa wananchi wetu kwa kipindi chote cha miaka mitano ijayo, nawapongezeni sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana vilevile Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Mheshimiwa Dkt. Hussein Ally Mwingi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kusimamia vyema Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi tunayoimalizia 2020 - 2025. Hakika wamezitendea haki sekta zao walizozisimamia na hata sasa tumeona Tanzania nzima imekuwa ikiwataja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija Tanzania Bara, Dkt Samia amekuwa akitajwa kila sehemu, ukienda Zanzibar Dkt. Hussein Ally Mwinyi amekuwa akitajwa kila sehemu. Hii yote ni kutokana na utekelezaji wa Ilani waliyoifanya na kusikiliza kwa sababu kila Mkoa ameonesha hapa viongozi wote waliosimama wa Waheshimiwa Wabunge wameeleza katika maeneo yao kazi zilizofanyika. Hakika kazi walizozifanya ni za kutukuka na Insha Allah Mwenyezi atawajaalia, atawalipa mema kwa kile ambacho wamekitekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiendelea na shukrani zangu, ninatoka Mkoa wa Kaskazini Unguja nikiwawakilisha wanawake wa Mkoa wa Kaskazini Unguja ambao kwa hakika wamefarijika na jitihada za Marais wetu hawa na viongozi wetu hawa waliomo ndani ya Serikali na zaidi viongozi hawa wametokana na Chama Cha Mapinduzi. Chama Cha Mapinduzi kimetuwekea misingi imara ya kuwapata viongozi wazuri ambao watatuletea maendeleo sisi wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa hapo nianze kwa kusema ndani ya Mkoa wa Kaskazini hususan wanawake wa Mkoa wa Kaskazini tutajitahidi kadri ya uwezo wetu kuhakikisha viongozi hawa wanarudi madarakani ili waweze kuendeleza yale waliyoyapanga wananchi waweze kupata manufaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru tena Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan alikuja kutufungulia kituo chetu cha ujasiriamali pale Mkoa wa Kaskazini Unguja cha wanawake na alipokuja akatuasa mambo mengi na alitoa kauli pale akasema kwamba viongozi watapimwa kutokana na utendaji wa kazi waliyoifanya. Akatushajihisha akatuambia kwamba katika kituo kile cha ujasiriamali ambacho kitakuwa kinafundisha ushoni, akatuahidi kutoa vyereheni vitano, lakini kwa uzalendo wake mama huyu alitupa vyerehani 10.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ni kuonesha kwamba anawiwa na changamoto za wananchi kukosa ajira, kwa sababu kituo kile kinapokea vijana wengi ambao wanakuja kujifunza pale, wakitoka kujifunza watakwenda katika maeneo yao kwenda kuyaendeleza na hatimaye watapata kipato. Sasa kwa hilo ninampongeza sana, ninamshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutupatia vyerehani vile, tunamshukuru na tunamwahidi tutazifanyia kazi kwa kadri ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaendelea vilevile kumshukuru tena Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika ziara zangu nilizokuwa ninatembelea nilikuwa nimepitia katika dawati la jinsia pale Mahonda, wakanieleza changamoto nyingi wanazopambana nazo, lakini mwisho wa siku wakasema wanashukuru sana kwa sababu kuna watoto ambao walikuwa wanapatikana na shida kidogo, basi walikuwa wanapeleka kituo cha polisi na nikaona bora nitembelee, nikatembelea kituo cha polisi na nikatembela Kituo cha Polisi cha Mkokotoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Polisi Mkokotoni kimejengwa upya, kilijengwa tangu miaka ya ukoloni lakini Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akawapelekea pesa kikajengwa upya kituo kile kipo vizuri na makamanda wa pale waliniambia niwaletee shukrani zao kwa Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa hili ninaomba amwambie Mheshimiwa Rais kwamba zile pesa alizopeleka wakajengewa kituo kile cha polisi, basi wanamshukuru sana sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo ni kizuri, kituo kina miundombinu ya kisasa kwa sababu hapo mwanzo ilikuwa hata wale watoto wanaokinzana na sheria walikuwa wanawekwa pamoja na mahabusu watu wazima, lakini kwa sasa kituo kimejengwa, kina miundombinu mizuri hata mahabusu ya watoto ipo nimeiona ipo vizuri. Kwa hiyo ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri ampe salamu hizi Mheshimiwa Rais kwamba makamanda wa Kituo cha Polisi Mkokotoni wanamshukuru sana kwa lile alilowafanyia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuendelea mbele, ninashukuru tena kwa Mheshimiwa Rais ametupatia majiko ya gesi kwa ajili ya wananchi wetu, kwa hiyo na kwa Mkoa wa Kaskazini ninashukuru wamepata, ametupa mashuka mama, tumekwenda kupeleka kwenye hospitali zetu, pia na hilo tunashukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna hiyo Mkoa wa Kaskazini tutajitahidi kadri ya uwezo wetu kuzisaka kura tuhakikishe tunamrudisha tena mama huyu na pamoja na Mheshimiwa Dkt. Mwinyi wapate kura za kishindo. Tunashukuru sana kwa kazi zote walizotufanyia pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye hii bajeti ya Serikali pia naishukuru kwa sababu ukiiangalia hata vile vipaumbele vyake vilivyowekwa pale vinamlenga mwananchi wa kawaida moja kwa moja atanufaika. Vipaumbele hivi vitawasaidia wananchi kupata ajira, kwa sababu kuna kuwastawisha wananchi kwa miradi yote na mipango na ajira, kila kitu. Sasa haya yote wananchi wananufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye sehemu ile ya ajira, watafaidika wananchi, tukiangalia bajeti iliyokwisha ya 2025/2026 tuliona kwamba ajira kwa mujibu wa Ilani yetu ya Uchaguzi kipindi kile walikuwa wamesema ajira 8,000 wananchi watapatiwa, lakini utekelezaji wa Ilani ile umevuka kwa sababu kuna ajira zimetoka 8,000 na nukta nane. Sasa kwa sababu hiyo tunashukuru sana Serikali, tunashukuru sana kwa kazi zote zilizofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hayo kila nikiendelea mimi nitakuwa ninashukuru tu, lakini yote ni kwa sababu kazi kubwa imefanyika ya kuleta maendeleo ndani ya nchi yetu. Ninashukuru sana uongozi wa Chama changu Cha Mapinduzi kwa muda wote unijaalia nikaingia humu ndani ya Bunge hili Tukufu, ninawashukuru sana uongozi wa Kaskazini Unguja, wanawake wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, UWT kwa pamoja, mama yetu Mama Mary Chatanda anatusimamia vyema, tunashukuru tunaendelea mpaka muda huu tunapokamilisha bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaunga mkono hoja. (Makofi)