Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Neema Peter Majule (2 total)

Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025
MHE. DKT. NEEMA P. MAJULE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuongea tena mara ya pili katika siku ya leo. Nimefurahi sana kuongea leo ili nami pia niweze kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano. Siyo hivyo tu, kumpongeza kwa birthday yake leo na kweli hata kama hatupo huko, lakini tumemtakia birthday njema siku ya leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, ninampongeza sana Mheshimiwa Spika na wewe Mheshimiwa Naibu Spika kwa kuchaguliwa kuliongoza Bunge hili Tukufu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ninampongeza sana kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba kwa kuchaguliwa kuwa Waziri Mkuu wa nchi hii ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami nitoe shukrani nyingi kwa Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi ya kuingia Bungeni, nafasi ambayo niliipambania kwa miaka 10 bila kupata, lakini sasa nimefanikiwa kuingia Bungeni. Ninamshukuru Mwenyezi Mungu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawashukuru wanawake wa Dodoma kwa kuweza kuniamini na kunipa kura nyingi sana. Kati ya kura 1,581 niliweza kupata kura 1,524. Kwa hiyo, ninawashukuru sana wanawake wa Dodoma, wameniamini sana na mimi nitawawakilisha vyema Bungeni. Siyo hivyo tu, nitafanya utumishi uliotukuka kuweza kuwatumikia wanawake wa Dodoma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitamani sana kuchangia hotuba hii ya Mheshimiwa Rais, niliiona ni hotuba ya kiongozi tena iliyo thabiti kabisa, kiongozi mwenye madaraka, lakini upande wa pili ili-sound kama hotuba ya mama tena mama mlezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba niongee maeneo machache ambayo ninamsikia Rais wangu akiongea kama mama. Pale alipoingia tu na kuanza hotuba yake kwa kuonyesha masikitiko yake kwa matukio yaliyotokea Oktoba 29, hiyo ilikuwa ni sauti ya mama. Pia, alipoendelea kuwasamehe wale vijana ambao waliingia kwenye mkumbo hiyo pia ilikuwa ni sauti ya mama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, aliongea sasa kama mama, akasema, nikimaliza nafasi yangu sipendi kusemwa kwa majengo, miundombinu, barabara, maghorofa, lakini niache tabasamu kwa Watanzania. Hiyo niliona ni sauti ya mama ndani ya hotuba ya Rais wa nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ilikuwa ni dira yetu ya miaka mitano ambayo tutaifuata na inaenda sambamba kabisa na Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Niliona Rais ame-summarize Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwenye hotuba fupi aliyoitoa kwenye Bunge lako Tukufu hiyo tarehe 14, Novemba, 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nijikite kwenye hotuba hiyo na mawazo yangu niyatoe kwenye uchumi na uwekezaji wa wananchi. Amesema: “malengo yetu ya kiuchumi ni kupandisha kasi ya ukuaji wa uchumi kutoka 5.6% hadi zaidi ya 7%.” Kwa hiyo, alikuwa na maana kwamba economic growth yetu itaenda zaidi ya 7%. Pia, akasema kwamba itaongeza ukuaji wa huduma za kijamii ambazo ni muhimu sana, hata tuzo nyingi amepata kwa ajili ya huduma za kijamii, kujenga hospitali, kujenga zahanati mpaka vijijini, kujenga vituo vya afya na kujenga hospitali za rufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu hahitaji kutoka mkoa kwenda mkoa mwingine tayari hospitali za rufaa zimejengwa kwenye kila mkoa na hapo moja kwa moja ameokoa maisha ya mwanamke na mtoto. Hivyo, wanawake tumerefushiwa maisha yetu, hatufi mara nyingi kwa kujifungua au kwa njia ya uzazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Rais huyu mwanamke amejipambanua kwa kutujengea vituo vya afya na zahanati kuanzia chini vijijini, kwenye tarafa zetu, kwenye wilaya zetu na hospitali za rufaa zipo kwenye kila mikoa yetu. Hivyo, kongole nyingi sana kwa Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, amejikita katika kujenga miundombinu wezeshi ya kiuchumi. Hapo ndiyo tunaona barabara, madaraja yanajengwa, anafanya uwekezaji rafiki ili tuweze kufanya maendeleo ya kiuchumi. Nami ninampongeza tena Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano. Pia, anasema ataimarisha masoko na mitaji na kuhamasisha uwekezaji wa ndani, anatia moyo Watanzania kuwa wawekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zamani tulikuwa tunafikiri wawekezaji ni wazungu. Mzungu akija ndio anatetemekewa kuwekeza, lakini sasa hivi tunatiwa moyo wawekezaji wa ndani kuwekeza kwenye viwanda na shughuli mbalimbali za kiuchumi. Ana kitengo maalumu cha kuwatia moyo wawekezaji wa ndani, lakini akigusa moja kwa moja, ni kutia moyo shughuli zetu za madini, na pia kuwawezesha au kuwadhamini mikopo hao wawekezaji wa ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami niseme tu ukweli tumaini hili ni kubwa sana kwa wanawake na vijana pamoja na watu wa makundi maalum kwa sababu zile 10% za kila halmashauri bado zinaendelea. Alipotamka hivi tu, nafikiri wanawake na vijana wote tulifurahi. Hilo ni tumaini kubwa sana kwa wanawake wa Kitanzania kwamba tutaendelea kupata hizo 10% za mikopo, na bado ataendelea pia kufanya mifuko yote ya uwekezaji iliyo chini ya ofisi yake ya kiuchumi, yapata mifuko 74, nayo pia itaendelea kuwasaidia wanawake, vijana na makundi maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Dodoma sisi tumenufaika sana na hizi 10%. Kwa miaka minne tu wanawake wamepokea shilingi bilioni 1.6, kwa Dodoma Mjini peke yake. Siyo hivyo tu, tumeendelea kunufaika na mifuko kama TASAF na tumeenda kunufaika na mifumo mingine kama Women Development Funds. Kwa hiyo, sisi tunaendelea kunufaika na mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kutuwazia vizuri wanawake, vijana pamoja na makundi maalum kwenye jamii yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, ni hilo tumaini sasa la shilingi bilioni 200 ambazo nazo pia zinaenda kwa wajasiriamali wote, lakini wanufaika wakubwa watakuwa ni hao hao wanawake, vijana na makundi maalum pamoja na wazee wameongezwa hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapongeza sana hotuba hii, ina mashiko. Tunawaomba tu watendaji kwenye Wizara mbalimbali na sekta mbalimbali watumie vizuri maneno haya yaliyowekwa kwenye hii hotuba ili wanufaika wawe watu wote ikiwepo wanawake wote hasa wa vijijini. Tukiwa kwenye kampeni, tulipokwenda vijijini, wanawake wengine hawajawahi kusikia na kupata hii mikopo. Hivyo basi, yatengenezwe mazingira rafiki ambayo mikopo hii itaweza kuwafikia wanawake waliopo vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, elimu hiyo ya fedha ambayo tuliongea hata asubuhi iendelee kutolewa mpaka kule vijijini ili wanawake, vijana na makundi haya maalum yaweze kupata elimu ya fedha ili sasa waweze kurasimiwa biashara zao na waweze kukopesheka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaunga mkono sana hotuba ya Rais wangu mpendwa kabisa. Mungu ambariki, ampe maisha mema na leo ni birthday yake, tunamhitaji akiwa na afya njema aendelee kufanya majukumu yake, ahsante sana. (Makofi)
Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. DKT. NEEMA P. MAJULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa hii nafasi na nimefurahi sana kumfuata kijana kuongea, maana kijana amejikita kwenye mambo ya vijana mpaka wote tumefurahi na hii ndiyo sura ya Bunge lako lina wawakilishi wa kila sekta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, kwa ajili ya kutusaidia na kutuwezesha kutupa Mawaziri pamoja na Manaibu Waziri ambao wamekaa kwenye Wizara hizi na hata kuweza sasa kutoka na Mpango huu wa Maendeleo wa Miaka 25. Moja kwa moja niipongeze Wizara ya Mipango na niipongeze Wizara ya Fedha: Mpango uliopita wa miaka mitano ulikuwa mzuri umetusogeza mpaka tulipo na kweli maendeleo makubwa yamefanyika nchi za Kiafrika zinashangaa, dunia pia nayo inashangaa kwa maendeleo makubwa ambayo Tanzania imeweza kupiga kwa miaka mitano iliyopita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tumepata Mpango mwingine ambao kama wanavyosema wenzangu na walivyounga mkono ya kwamba Mpango huu ni wa Kisayansi na Kiteknolojia: Mpango ambao unaweza kutupaisha tukaenda mahali pazuri zaidi, lakini tuna Mpango huu wa muda mrefu sasa wa miaka 25 na huu Mpango wa miaka mitano, halafu tumepewa Mpango wa mwaka mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika uchambuzi wangu mimi nataka kuchangia nafasi sasa ya mwanamke katika Mpango huu. Nimeupitia Mpango na kuweza kuona nafasi ya mwanamke, Wabunge wengi wamechangia mambo mbalimbali na wamegusa kwa namna moja au nyingine mambo ya wanawake katika Mpango huu. Hata hivyo, ninataka niseme kwamba, wanawake tumepaishwa zaidi kipindi hiki cha kuwa na Rais, Mwanamke Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana Mpango huu ambao tumeletewa wa miaka 25, pia wanawake wamepewa nafasi kubwa sana. Lakini niseme tu kwa nini nimekuwa na interest hiyo, kwanza, kwa sababu mimi zaidi ya kuwa Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Dodoma, mimi pia ni Mwenyekiti wa UWT wa Mkoa wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanawake idadi yetu sisi ni 51% population ambayo tumehesabiwa mwaka jana 2025, lakini pia ndiyo wazalishaji wakubwa na ndio wanaoweza kuupeleka uchumi huu kutoka hatua hii kwenda hatua nyingine. Kwa sababu wanawake wamejikita zaidi kwenye kilimo, asilimia kubwa ya wakulima ni wanawake na pato la Taifa ambalo linachangia ni 54%, ambao watendaji wakubwa kwenye field ni wanawake. Hivyo basi, hatuwezi kutenga maendeleo makubwa ambayo tunayatarajia pasipo kuwahusisha na kuwaongelea wanawake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, wanawake wamejikita kwenye biashara ndogondogo ikiwepo biashara za kati (SME), kwa hiyo ni wanawake ndiyo waliofanya. Wanawake pia wamejikita kwenye kazi za huduma za jamii, hivyo basi niseme kwamba, Mpango huu ambao tunao, tutaenda vizuri tukiwa kwenye usawa wa kijinsia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipendekeze moja kwa moja nisije baadaye mwishoni nikashindwa vitu vya kupendekeza. Niseme basi Mpango huu kama tutaweza kuenenda ukiwa na mlengo wa usawa wa kijinsia viwekwe moja kwa moja viashiria mahususi vya kijinsia katika Mpango mzima, lakini pia kwenye bajeti, yaani kuwe na indicators ambazo ni mahususi kabisa za kijinsia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, ushiriki mzima wa wanawake kuanzia kwenye Mpango, lakini pia kwenye ufuatiliaji kwa maana ya monitoring, lakini pia kwenye tathmini. Kuwepo na ushiriki wa wanawake kwenye stage zote hizo kuanzia kwenye mipango; kwenye utekelezaji mpaka kwenye tathmini. Tukienda kwa pamoja hivyo, ninaamini kwamba tunaenda kufikia haya malengo vizuri kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda tu niseme kwamba, uchumi jumuishi ambao tumeamua kwenda nao kwa sasa hivi utaenda kuinua mapato yetu ya Taifa mpaka dola za Kimarekani trilioni moja, lakini pia pato la mtu mmoja mmoja linaenda kwenye dola za Kimarekani 7,000 ifikapo 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo haya yatatokea tu kama tutaongeza fursa za ajira kwa wanawake: wanawake ndiyo ambao ni wazalishaji, lakini siyo hivyo, tutaweza kujikwamua tu kwa kupunguza umaskini kuanzia ngazi ya kaya au kuanzia ngazi ya familia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umaskini ukiuongea kati ya mwanamke na mwanaume aliye masikini zaidi ni mwanamke kwa sababu ya mila zetu na desturi ya kwamba kwenye ngazi ya kaya mmiliki wa mali ni mwanaume na utaweza kuona haya mara mwanaume anapoondoka duniani yule mwanamke hawezi kuruhusiwa kumiliki ardhi aliyonayo pale inachukuliwa na familia ya mwanaume. Kule alipotoka kwenye familia yake hajapewa ardhi, huku alipoolewa nako hapewi ardhi, hivyo umaskini wa mwanamke ni mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukitaka kwenda kwa pamoja basi tulenge kuzikwamua kaya ambazo mara nyingi zinakuwa headed au zinakuwa zinaongozwa na wanawake, huko ndiko ulipo umaskini. Kama tutakuwa na Mpango mzuri wa kuwakwamua wanawake kwenye ngazi ya familia, moja kwa moja tutakuwa tumefanikiwa kulikwamua Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni mambo ya elimu; kama tutaweza kutoa elimu kwa wasichana vizuri kabisa, tunawapanua wasichana uwezo kama unavyoona Mheshimiwa Magreth ame-present pale, uwezo wake umepanuka, msichana huyu amepewa elimu. Hivyo basi tunaweza kumkwamua, tunaweza kuwakwamua wanawake kuanzia kuwapa elimu ya kutosha kuanzia wakiwa wadogo. Mpango huu umeonesha tunaongeza idadi ya shule za sekondari na ushiriki wa wasichana kwenye elimu ya sekondari na tunaongeza pia hata teacher-student ratio kutoka 105 kwa Mwalimu kwenda wanafunzi 40 kwa Mwalimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yote hiyo itasaidia kuongeza fursa ya elimu kwa wasichana na tutawaongezea wasichana sasa uwezo wa kushiriki kwenye biashara za ushindani. Siyo hivyo tu, tunapoenda kuangalia mambo haya moja kwa moja tunapoongelea mwanamke tunaongea juu ya mwanamke na mtoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli tumefanikiwa sana kupunguza vifo vya wanawake na Watoto wachanga. Mpaka sasa hivi ni vizazi 104 tu katika 1,000 wanawake wanaopoteza maisha. Mpango huu unaenda kupunguza vifo hivi mpaka vizazi 85 tu kati ya vizazi 1,000, lakini inapunguza vifo vya watoto kuanzia 33 hadi 27. (Makofi)

Mheshimiwa Mweyekiti, kwa nini sasa? Ni kuzidi kuwekeza zaidi katika sekta ya afya ili tuendelee kuboresha maisha ya wanawake na Watoto, lakini siyo hivyo huduma za dispensary zinapoanzishwa na vituo vya afya zilenge kuwapa ajira nyingi zaidi wanawake kwa maana ndiyo watoa huduma za kijamii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo tutaweza kufaulu sana kuwanufaisha wanawake kwenye huu Mpango wetu wa miaka 25, lakini Mpango wetu wa miaka mitano ambao moja kwa moja umejikita kupunguza umaskini. Pia tutaweza kufanikiwa kwa huu Mpango wetu wa mwaka mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nitoe mapendekezo yangu, zaidi ya kuongeza indicators kwenye kila Mpango na pia na bajeti, lakini pia fedha za mikopo za wanawake ziongezwe kwenye bajeti, ambayo itatengwa kwa ajili ya maendeleo ya wanawake…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa, muda wako umekwisha. Tunashukuru sana kwa mchango mzuri. Muda umekwisha malizia sentensi ya mwisho.

MHE. DKT. NEEMA P. MAJULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)