MHE. DKT. NEEMA P. MAJULE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri yaliyotolewa na Naibu Waziri kijana kabisa. Nina maswali ya nyongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; kwa kutambua umuhimu wa sekta ya fedha, Serikali imeandaa au kusimamia miongozo ipi ya kuhakikisha wananchi hususan wanawake na vijana wanapata elimu ya fedha ili kuchochea jitihada za ukuaji wa kiuchumi? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili; Serikali imechukua gani sasa kwa hao watu ambao wamejinufaisha sana kwa mikopo hii yenye riba kubwa? Waingereza wanasema Predatory Loans, lakini sisi tumeitafsiri kama ‘Mikopo ya Kausha Damu’. Kwa maana kwa namna walivyofanya wameweza kabisa wenyewe kujinufaisha na kupunguza kabisa jitihada ya Serikali ya kuwakwamua wananchi kiuchumi hususan wanawake na vijana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA (MHE. LAURENT D. LUSWETULA): Mheshimiwa Spika, ahsante sana Mheshimiwa Dkt. Neema Peter. Kwanza ninakushukuru kwa maswali mawili ya nyongeza, maswali mazuri, lakini hii inamaanisha kwamba wanawake wa Dodoma hawakukosea kukuchagua. Kweli Ph.D kichwani ipo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya hayo sasa, niseme tu kwamba, Serikali imeendelea kuandaa na kusimamia miongozo na utekelezaji wa sekta ya fedha ili kuchochea uchumi wa wananchi, hasa vijana pamoja na wanawake. Serikali imekuja na mkakati maalum ambao unaitwa Programu ya Elimu ya fedha ya mwaka 2020/2021 – 2025/2026, ikiwa ni mpango maalum wa kutoa elimu kwa wananchi (wanawake wanaume na makundi mengine) ambayo inalenga zaidi kuwawezesha Watanzania kupata uelewa, maarifa na kuwajengea kujiamini katika kusimamia mapato na matumizi na kufanya maamuzi sahihi katika kutumia huduma rasmi za kifedha.
Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, ninyi mnaweza mkawa ni mashahidi ya kwamba kama Wizara ya Fedha tumekuwa kila mwaka tukiadhimisha maadhimisho ya Huduma ya Wiki ya Kifedha; ambapo tumeanza mwaka 2021 – 2026 (ambapo yamefanyika rasmi tarehe 21 mwezi huu, 2026). Mimi binafsi nikimwakilisha Waziri wa Fedha nimeenda kufungua rasmi maadhimisho hayo ambayo yamefanyikia nchini (Tanga) ili wananchi waweze kupata elimu ya kifedha. Kweli wananchi wa Tanga waliyapokea kwa hali ya juu, walikuwa ni wengi. Hii ni mikakati maalum ya Wizara ya Fedha kuhakikisha ya kwamba wananchi wanapata elimu ya fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, maadhimisho haya yameanza muda kidogo, tangu mwaka 2021. Mikoa ya Dar es Salaam, Mwanza, Arusha na mikoa mingine imeendelea kunufaika na elimu hii.
Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, zaidi ya mikoa 16 mpaka sasa hivi tumeweza kufikisha huduma hiyo ya fedha, kuwapa elimu ambapo zaidi ya wananchi 64,000 ikiwemo wanawake 40,000 na wanaume 24,000 wamepata elimu hii kuhusu elimu ya fedha. Vilevile, zaidi ya halmashauri 94 nazo tumepita kuhakikisha kwamba wanapata elimu ya fedha ili waweze kufanya maamuzi sahihi katika uwekezaji wao, katika uwekezaji na kuingia sasa kuwekeza kwenye mambo yetu ya kifedha ikiwemo uwekaji akiba, mikopo, uwekezaji, bima, Bima-amana, kodi, hati fungani na mengineyo mengi, kwa sababu sisi kama Wizara ya Fedha tumejipanga ipasavyo. (Makofi)
SPIKA: Ahsante!
NAIBU WAZIRI WA FEDHA (MHE. LAURENT D. LUSWETULA): Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili, lililenga zaidi kwamba sasa sisi kama Wizara ya Fedha tumejipanga kwa namna gani kuhakikisha kwamba wale wanaokiuka taratibu zilizowekwa sasa wanaweka riba kubwa ili kujinufaisha wao.
Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba, katika mkakati ambao tumesema kwamba tumeandaa rasimu ya kusimamia mikopo ya kidijiti ambayo inatarajiwa kuanza mwaka 2026 na 2027, sisi kama Wizara ya Fedha tumejipanga kuhakikisha ya kwamba taasisi zote zinazotoa mikopo zinafuata taratibu zote. Yeyote anayekiuka tayari tumeshaanza msako huo kuhakikisha kwamba tunasitisha leseni na kufunga kabisa, kwa sababu anakiuka taratibu ambazo Serikali imeziweka. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa nyongeza tu kwa niaba ya Waziri wa Fedha, tunaiagiza Benki Kuu ya Tanzania kuendelea kuongeza juhudi zaidi katika udhibiti wa mikopo hii, kuhakikisha kwamba wananchi hawa ambao sasa wanatuamini na Serikali yetu hii ya Awamu ya Sita wanapata mikopo ambayo sasa inawanufaisha na wala si ile wanayoiita ‘Kausha Damu’ na sisi tumejipanga kuhakikisha kwamba tuko pamoja kuwasaidia wananchi kwa sababu ndiyo wananchi wetu. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. NEEMA P. MAJULE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ya kwamba tathmini ilifanyika na bado kuna maboresho yamefanyika, lakini bado kumekuwa na malalamiko makubwa kwa wanawake wa Dodoma Vijijini kwamba mikopo hii haiwafikii na pia kumekuwa na mchakato mrefu sana wa upatikanaji wa mikopo hiyo. Je, ni lini Serikali itakuwa na njia mbadala kwa ajili ya wanawake wa vijijini kupata mikopo sawa na wanawake wa mijini ambao wapo karibu na hizo fursa?
Mheshimiwa Spika, lingine pia kumekuwa na huo mchakato mrefu...
SPIKA: Mheshimiwa hujauliza maswali mawili?
MHE. DKT. NEEMA P. MAJULE: Mheshimiwa Spika, hili ni swali la pili la nyongeza.
SPIKA: Sawa, endelea.
MHE. DKT. NEEMA P. MAJULE: Mheshimiwa Spika, kumekuwa na mchakato mrefu wa upatikanaji wa huduma hii ya mikopo, kwamba, wanawake wengine wamekata tamaa kabla hawajafikia kupata mikopo. Swali, je, ni lini Serikali itakuja sasa na one stop centre ambapo mwanamke huyu akienda atakuta na atapata pale pale katiba, cheti, tax clearance, service levy na huo mkopo ili kunusuru wanawake kukata tamaa ku-process mkopo huu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO): Mheshimiwa Spika, ninaomba niyajibu maswali yote mawili kwa pamoja kwa sababu yanaingiliana.
Mheshimiwa Spika, wote tutakumbuka kwamba mara baada ya kuanzisha utoaji wa mikopo awamu mpya, kwa maana ya baada ya kuachana na utaratibu wa zamani, Serikali ilizigawa halmashauri zetu katika makundi mawili. Kundi la kwanza likiwa na halmashauri 174 na kundi la pili, ikiwemo Dodoma, likiwa na halmashauri 10. Halmashauri 174 tumeendelea kutoa mikopo kupitia utaratibu ulioboreshwa, lakini halmashauri hizi 10 pia tulisema tutoe mikopo kupitia benki ili tuweze kuona kama tutafanikiwa, kama ambavyo Mheshimiwa Rais alikuwa ametamani ifanyike, hatimaye tuweze kufanya utaratibu wote utumike kwa nchi nzima.
Mheshimiwa Spika, sasa katika mikoa 10, maeneo 10 ambayo tulipanga kufanya kupitia benki ni pamoja na Jiji la Dar es Salaam, kwa maana ya Mkoa mzima wa Dar es Salaam, Dodoma, Songea Manispaa, Newala, Bumbuli, Siha, Mbulu pamoja na Itilima na Nkasi; huku kote tumeendelea kutoa kupitia utaratibu wa benki.
Mheshimiwa Spika, wiki mbili zilizopita tumekaa na benki hizi tatu ambazo tulikuwa tumezipa kazi hii; Benki za CRDB, NMB na Uchumi Commercial Bank; kwa ajili ya kufanya tathmini na kuona maeneo ambayo yamekuwa kikwazo kwa watu wetu.
Mheshimiwa Spika, msisitizo wetu na namna ambayo tumekubaliana na maelekezo ambayo tumepeana ni kwamba, mabenki ni sharti yazingatie kwamba wananchi ambao tunataka wakopeshwe mikopo hii, ni wananchi ambao hawawezi kukidhi masharti ya kibenki. Ndiyo maana tumesaini MoU ya kuhakikisha kuwa wanapewa kwa mazingira hayo hayo waliyonayo. Mheshimiwa Rais anataka watu wote wapate mikopo, hata wasiokopesheka kwenye benki. Kwa hiyo nisisitize tena kwamba tutayasimamia haya ili kuhakikisha hakuna ucheleweshwaji wa utoaji wa mikopo.
Mheshimiwa Spika, jana tumejibu swali hapa na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI amelitolea maelezo marefu na ya kina, kwamba Maafisa Maendeleo ya Jamii kwa kushirikiana na TAMISEMI wamewezeshwa. Kwanza pikipiki zaidi ya 98 ili waweze kuwafikia wananchi wetu kwenye vikundi vyao mahali walipo; na pia Serikali kupitia TAMISEMI tumekuwa tukitenga fedha kwenye OC zetu. Kila tunapopeleka OC tunapeleka na fungu kwa ajili ya Mafisa Maendeleo ya Jamii kuweza kuwafikia watu wetu. Niwaelekeze mikoa yote kupitia ma-RAS wetu wahakikishe kuwa hapawi na usumbufu wote kwa wananchi kupatiwa mikopo hii.