MHE. JOHN F. NZILANYINGI: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi nyingine ili niweze kupata kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, ni nini mpango wa Serikali wa kupambana na uvuvi haramu ambao unatajwa ndicho chanzo cha uhaba wa samaki na hivyo kupelekea viwanda vingi vifungwe?
Mheshimiwa Spika, swali la pili; katika majibu ya Serikali, pamoja na jitihada ambazo inafanya za kuhamasisha ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba, Serikali bado haioni kwamba tutaendelea kuwa na changamoto ya upungufu wa samaki kwa sababu viwanda vyetu havitumii samaki aina ya sato ambaye ndiye hasa anafugwa kwenye vizimba vya samaki?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ninampongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa maswali mazuri. Katika swali la kwanza, Serikali inatambua uzito wa changamoto ya uvuvi usiozingatia sheria na athari kubwa ambazo uvuvi huu umeleta katika uchumi wetu na ndiyo maana mpaka sasa tunaendelea na jitihada mbalimbali na mipango ya kupambana na uvuvi huu haramu ikiwemo kuunda Mamlaka ya Uvuvi ambayo iko katika hatua mbalimbali na Mamlaka hii itapewa nguvu ya kisheria na kikanuni ya kupambana na uvuvi huu haramu.
Mheshimiwa Spika, Serikali pia inaendelea na doria mbalimbali za ulinzi kwa kushirikiana na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama ikiwemo Jeshi la Polisi na Jeshi letu la Ulinzi wa Wananchi ili kuhakikisha tunaendelea kupambana na uvuvi huu usiozingatia sheria. Serikali pia inaendelea kushirikisha jamii zetu katika kulinda rasilimali hizi za uvuvi kupitia BMU zetu ambazo tunazo katika mialo yote nchi nzima.
Mheshimiwa Spika, tunaendelea kutoa elimu kwa wavuvi wetu lakini pia tunaendelea kudhibiti uingizwaji na uuzwaji wa zana mbalimbali ambazo zinachochea au kuchangia katika uvuvi haramu.
Mheshimiwa Spika, katika swali la pili, tunatambua pamoja na kwamba Serikali na kwa jitihada za Mheshimiwa Rais, tunaendeleza programu mbalimbali za kuwezesha Watanzania yakiwemo makundi mbalimbali ya vijana, wanawake na vyama vya ushirika kushiriki katika uvuvi kupitia uvuvi wa vizimba. Hata hivyo bado tunatambua kwamba uvuvi huu hauwezi kuwa mbadala wa uvuvi wa asili.
Mheshimiwa Spika, kwa misingi hiyo, ndiyo maana tunaendelea na jitihada mbalimbali za kupambana na uvuvi usiozingatia sheria, kuu zaidi ikiwa ni uundwaji wa Mamlaka hii ya Uvuvi ambayo utaratibu wake katika Mpango wetu wa Serikali unaendelea vizuri. Tunawaomba tu Waheshimiwa Wabunge kwamba pindi tutakapokamilisha taratibu zetu za kiserikali na kuleta mpango huu wa uundwaji wa Mamlaka hii, basi watuunge mkono ili tuweze kuipa nguvu hii ya kisheria na kikanuni kupambana na uvuvi huu usiozingatia sheria. Ninashukuru sana. (Makofi)
MHE. JOHN F. NZILANYINGI: Mheshimiwa Spika, ninashukuru sana kwa majibu ya Serikali, lakini ninaomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; ninaomba kufahamu, huo upembuzi yakinifu unahusisha kitu gani na utakamilika lini? Kwa sababu tarehe 28 Machi, 2024, Serikali ilisaini mkataba na mkandarasi anayeitwa Taifa Civil Mining Limited, mkataba ambao ulikuwa na zaidi ya thamani ya bilioni 29.
Mheshimiwa Spika, kwa maelezo ya Serikali, wananchi wa Nyamagana, nikiwemo mimi mwenyewe kama mwakilishi wao, ninapata mkanganyiko wa nini ambacho kinaendelea kufanyiwa upembuzi yakinifu, ilhali Serikali tayari imekwishasaini mkataba.
Mheshimiwa Spika, swali la pili; toka Serikali isaini mkataba huo, haijawahi kupeleka hata senti tano. Hivi ninavyozungumza, kwa taarifa nilizonazo, mkandarasi ameanza kuondoa vifaa vyake site. Ni lini sasa Serikali itapeleka fedha ili mkandarasi aweze kuendelea na kazi ya ujenzi wa uwanja? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, kwanza ninampongeza sana Mheshimiwa Nzilanyingi kwa ufuatiliaji wake wa karibu kwenye uwanja wetu huo wa Mwanza, lakini yeye Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote wa Mkoa wa Mwanza na Kanda ya Ziwa kwa ujumla, wanachama wa Chama Cha Mapinduzi na wananchi kwa ujumla. Kiko kilio kimoja ambacho wamekuwa wakikitoa kwa muda mrefu, ni lini uwanja wa Mwanza utapewa hadhi ya kimataifa.
Mheshimiwa Spika, kufuatia maombi hayo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dr. Samia Suluhu Hassan, amepokea kilio hicho na amefanya usanifu, ametuelekeza kama sekta chini ya Waziri wetu Mheshimiwa Mbarawa tumefanya tathmini ya kina na kubaini kuwa, iko haja kubwa ya kuufanya uwanja kuwa wa kimataifa.
Mheshimiwa Spika, sasa mambo mazuri yanahitaji pia subira, nini kinafanyika kama nilivyosema? Mambo matatu; la kwanza Jengo lilopo kwa sasa, linatosha abiria karibu 400,000 – 500,000. Tunataka tufanye usanifu ili tuweze kujenga jengo kubwa litakaloweza kubeba abiria zaidi ya milioni mbili na laki tano. Ili ndani ya jengo, tuweze kuweka taasisi zote muhimu ambazo ni sifa na takwa muhimu kwenye uwanja wa kimataifa; Uhamiaji, Afya, pamoja na Maliasili na vitu vingine vingine. Mbili, runway; ili uwanja uweze kuwa wa kimataifa, ule upana wake hautoshi. Tunaongeza kutoka meta 45 mpaka meta 60 na ku-maintain urefu uliopo wa takribani meta 3,800.
Mheshimiwa Spika, la tatu, ni taa. Ule uwanja uliopo awali tulifikiri pengine zile taa zingetosha, lakini baada ya tathmini ya kina, inaonekana kabisa kwamba zile taa hazitatosha kwa sababu zilijengwa miaka ya 1970. Hivyo basi, tunataka tubadilishe taa zilizopo na kuweka za kisasa. Kwa sababu hiyo nimwombe Mheshimiwa Mbunge pamoja na Wabunge wote waweze kuwa na subira.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, ameuliza kwamba Serikali haikupeleka fedha ni kweli na jengo lililopo linafanya nini? Jengo lililopo sasa ambalo tulikuwa tumeshaanza ujenzi ambao tunashirikisha sekta binafsi tutalitumia kwa ajili ya general aviation. ndege ndogo, wale watu wa premium, ukiwa na ndege yako, utatumia jengo hilo. Lengo ni jema tu, kuhakikisha kwamba tunaupa hadhi ya kimataifa na inayostahili uwanja huo ambao unasafirisha bidhaa mbalimbali kutoka nchini kwetu minofu ya samaki, maliasili pamoja na utalii, kwa maana ya utalii kwa ujumla na kadhalika. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa nafasi. Hitaji la Uwanja wa Ndege wa Njombe ni kubwa sana kutokana na uchumi wa Njombe, lakini ni mradi wa kimkakati, pia ni ahadi Rais, ni lini sasa ujenzi wa uwanja huu utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mwanyika kwa ufuatiliaji wake wa karibu sana juu ya Uwanja wa Ndege wa Njombe. Yeye na Wabunge wenzake wa Mkoa wa Njombe wanafanya kazi nzuri. Serikali imetambua na kuthamini umuhimu wa uwanja wa Njombe kama nilivyosema kwenye kubebea mazao kama vile parachichi na kadhalika na kwa sababu hiyo, Serikali inakwenda kujenga uwanja mkubwa. Ni hatua gani tuko mpaka sasa hivi?
Mheshimiwa Spika, tayari tulikuwa kwenye hatua ya kwanza ya kutafuta eneo, kwa sababu eneo la pale mjini halitoshi. Tayari viongozi wa mkoa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege wanashirikiana. Hatua ya pili tunayokwenda sasa ni kwa ajili ya kufanya usanifu ili tuweze kujua kiasi gani kinachohitajika uwanja utakaojengwa uweze kwenda sawasawa na hadhi ya Mkoa wa Njombe.