Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Devotha Daniel Mburarugaba (4 total)

MHE. DEVOTHA D. MBURARUGABA aliuliza:-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kurekebisha kigezo kinachowapunguzia fursa wanafunzi wa shule binafsi kupata mikopo ya elimu ya juu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako naomba nijibu swali la Mheshimiwa Devotha Daniel, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, upangaji na utoaji mikopo ya elimu ya juu unaongozwa na Sheria ya Bodi ya Mikopo (Sura 178) ambayo inabainisha sifa za msingi za mwombaji, zikiwepo sifa za kitaaluma za kujiunga na taasisi za elimu ya juu kwa waombaji waliothibitika kutokuwa na uwezo wa kumudu gharama za elimu ya juu.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutoa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu wanaotoka katika kaya maskini bila kujali mwombaji ametoka shule za Serikali au shule binafsi. Kwa msingi huo, Serikali kupitia Bodi ya Mikopo imeweka utaratibu wa kuzingatiwa kwa waombaji wote, bila kujali shule aliyosoma ilimradi mwombaji amekidhi vigezo vilivyowekwa ikiwemo ujazaji wa taarifa sahihi.
MHE. DEVOTHA D. MBURARUGABA aliuliza:-

Je, hatua gani inachukuliwa kuhakikisha usimamizi, utoaji, urejeshaji wa mikopo 10% ya halmashauri unakuwa wazi na unawafikia walengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. JAFAR R. SEIF) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Daniel Mburarugaba, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Kagera kuwa Serikali imeweka utaratibu wa kuhakikisha mchakato mzima wa usimamizi, utoaji na urejeshaji wa mikopo unakuwa wa uwazi na usawa. Utaraibu huo umeainishwa kwenye kanuni na katika mwongozo ambao halmashauri zote nchini zimepatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kanuni, mwongozo pamoja na vitini vya mafunzo vinaelekeza halmashauri baada ya kukusanya fedha kwa ajili ya mikopo zinapaswa kutoa tangazo kwa njia mbalimbali ili kuufahamisha umma. Sambamba na hilo Serikali imeunda mfumo wa kielektroniki wa utoaji na usimamizi wa mikopo ambapo kila mwombaji anautumia kuomba mkopo. Mfumo huu unatumika pia katika usimamizi wa shughuli za vikundi pamoja na kufuatilia marejesho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua hii imesaidia kuweka wazi uwajibikaji katika kila hatua ya utoaji wa mikopo, usimamizi na marejesho. Serikali itaendelea kuchukua hatua za kuhakikisha kuwa kunakuwa na uwazi katika uombaji na utoaji wa mikopo, kama kanuni na miongozo inavyoelekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. DEVOTHA D. MBURARUGABA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha Wabunge wa Viti Maalum wanashirikishwa katika utoaji wa mikopo ya 10% kwenye halmashauri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Daniel Mburarugaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatatanrmbua umuhimu wa kuwashirikisha Waheshimiwa Wabunge wote wakiwemo wa Viti Maalum, katika utoaji na usimamizi wa mikopo ya 10% katika halmashauri. Kufuatia maboresho ya sheria, kanuni na mwongozo wa utoaji na usimamizi wa mikopo hiyo wa mwaka 2024, Serikali imeweka utaratibu wa ushirikishwaji wa Waheshimiwa Wabunge kuhusu hatua za utoaji mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chini ya utaratibu huo, Waheshimiwa Wabunge wanatakiwa washirikishwe kikamilifu kupitia vikao vya kisheria vya halmashauri, hususani Baraza la Madiwani na Kamati ya Fedha, Uongozi na Mipango ambapo hupokea taarifa, kujadili na kutoa maoni kuhusu upangaji, ugawaji na usimamizi wa mikopo ya 10% kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

Aidha, Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI imewaelekeza Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuwataarifu na kuwaalika Waheshimiwa Wabunge kushiriki kwenye shughuli za utoaji mikopo katika halmshauri zao ili kuwapa fursa ya kuhamasisha, kuelimisha na kufuatilia shughuli za vikundi kutokana na mikopo hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inazisistiza halmashauri zote nchini kuendelea kuimarisha utaratibu wa mawasiliano na kuwapa taarifa kwa wakati Waheshimiwa Wabunge kuhusu ratiba za vikao, orodha ya wanufaika na mwenendo wa urejeshaji wa mikopo ili kuongeza uwazi na uwajibikaji. Ahsante.
MHE. DEVOTHA D. MBURARUGABA aliuliza:-

Je, Serikali ipo tayari kutenga dirisha maalumu la mikopo kwa sekta za kipaumbele za kilimo cha kahawa, ufugaji na biashara ndogo ndogo – Kagera?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Daniel Mburarugaba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wa Mkoa wa Kagera unategemea sana sekta za kilimo, mifugo, uvuvi na biashara ndogo ndogo. Serikali imekuwa ikitoa mikopo mbalimbali ili kuwawezesha wananchi wake. Mikopo hiyo ni pamoja na mikopo ya 10% inayotokana na mapato ya ndani ya halmashauri; mikopo ya kuwezesha shughuli za ufugaji wa mifugo na samaki kwa kutumia vizimba inayotolewa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi; mikopo kupitia Programu ya Jenga Kesho Iliyo Bora (Building a Better Tomorow – BBT) na Mfuko wa Pembejeo inayoratibiwa na Wizara ya Kilimo. Aidha, ipo mikopo inayotolewa na Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii kwa wajasiliamali wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, Serikali imeanzisha Benki ya Maendelo ya Kilimo na Ushirika ambayo imepewa jukumu mahsusi la kutoa mikopo kwa ajili ya kuwezesha sekta za kipaumbele za kilimo ikiwemo kilimo cha kahawa, ufugaji na biashara ndogo ndogo. Mwaka 2024/2025 Serikali imetoa mikopo ya shilingi milioni 742.67 kwa makundi mbalimbali ya Mkoa wa Kagera kupitia mikopo ya 10%.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kwa sasa Wizara ya Mifugo na Uvuvi imetoa matangazo ya kutoa mikopo ya shilingi bilioni 200 ambazo ni ahadi ya Mheshimiwa Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuwezesha wananchi kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kiuchumi zikiwemo kilimo, ufugaji wa mifugo na samaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutoa elimu na hamasa kwa jamii na makundi husika ili kunufaika na fursa za mikopo mbalimbali.