Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Jafari Wambura Chege (2 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipatia nafasi. Kwanza, nami nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipatia nafasi ya kuchangia Wizara ya Ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili; kipekee kabisa nichukue nafasi kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mambo kadhaa, lakini nitataja matatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati ninaingia kwenye Bunge hili mara ya kwanza nilikuwa ni Mjumbe wa Kamati ya Maliasili na Utalii. Nje ya hivyo nimekuwa niki-declare interest mara zote ambazo ninachangia kwenye wizara hii kwamba, mimi ni mdau wa sekta ya ardhi, pia ndiyo professional yangu ambayo imenikuza kwa miaka yote.
Mheshimiwa Naibu Spika, mambo makubwa matatu ambayo yamekuwa yakizungumzwa kwenye taarifa zote za kamati na michango ya Bunge hili. Moja; tumekuwa tukizungumzia sana umuhimu wa Sera ya Taifa ya Ardhi ya Mwaka 1995. La pili; tumekuwa tukizungumzia umuhimu wa RERA (Real Estate Regulatory Authority). Pia, tatu; tumekuwa tukizungumzia sana Kamisheni ya ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema nimeanza kutangulia kwa kipekee kabisa kuchukua nafasi kwa moyo wangu wa dhati kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa sababu haya yote matatu ambayo tumekuwa tukisema kwenye Bunge hili kwa miaka minne, kwenye Taarifa zetu za Kamati, kwenye michango ya Wabunge na ndiyo yamekuwa mapendekezo ya Kamati kwa miaka yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaona wakati huu wa Mheshimiwa Waziri Ndejembi, yametekelezwa na yamefanyika vizuri sana. Mheshimiwa Ndejembi hongera sana wewe pamoja na Naibu Waziri wako, watumishi wote wa Wizara kwa kweli wametufikisha vizuri sana. Hili si tu kwamba wamekosha Bunge lakini mmekidhi haja ya wadau wa sekta ya ardhi nchini. Sera ya Taifa ya Ardhi ya Mwaka 1995, tumekuwa tukiisemea sana ifanyiwe mabadiliko ili iendane na kasi ya ukuaji wa uchumi na sekta ya ardhi nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Sera ya Taifa ya Ardhi ya Mwaka 1995 tumekuwa tukiisemea sana ifanyiwe mabadiliko ili iendane na kasi ya ukuaji wa uchumi, iendane na kasi ya ukuaji wa Sekta ya Ardhi nchini, lakini maeneo mengine ilikuwa inamwacha mwanamke katika sekta ya umiliki wa ardhi hasa sehemu ya mirathi.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo kwenye Sera ya Taifa ya Ardhi tumeona inakwenda kumweka mwanamke kutambulika kumiliki ardhi, hata akinamama ambao wanakaa vijijini ambao kimsingi kwenye umiliki wa ardhi hasa maeneo ya mirathi walikuwa wameachwa, walikuwa hawana haki ya kumiliki ardhi, lakini sera hii inakwenda kutambua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri yale ambayo Mheshimiwa Rais ameyasema wakati anazindua sera hii, lakini pia malengo ambayo ameyaainisha kwenye taarifa yake na haya ambayo tumeyasema leo kupitia Bunge hili, nenda ukayafanye ili uweze kuboresha Sera hii ya Taifa ya Ardhi na iweze kufanya kazi vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ambalo ningetamani kwenye maeneo hayo ni kutambua mabadiliko ya kanuni na sheria mbalimbali kwenye sekta ya ardhi ambazo zinashabihiana na sekta ya ardhi nchini. Waziri anapofanya mabadiliko ya sera lazima aende akatambue sheria mbalimbali ambazo zinashabihiana na sekta ya ardhi nchini ili na zenyewe ziweze kufanyiwa mabadiliko ziendane na kasi yake na ziendane na dhamira na mwelekeo wa Mheshimiwa Rais nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema pia, lazima iendane na mabadiliko ya sheria na kanuni ya Wizara ya Ardhi peke yake. Kwa sababu zipo sheria, kama tunavyosema kwamba mwanamke sasa anakwenda kumiliki ardhi, tusipofanya mabadiliko ya Sheria ya Mirathi ya Ardhi maana yake itakuwa sera ipo, lakini mwanamke bado atakuwa hatambuliki katika umiliki wa sekta ya ardhi nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamwomba pia Mheshimiwa Waziri tena katika sekta hii kwamba Mamlaka za Upangaji na Upimaji, sheria inasema hivyo, tunatambua sheria inasema kwamba, mwenye mamlaka ya upangaji na upimaji ni Mamlaka ya Serikali za Mitaa na mimi ni Mjumbe wa Kamati ya TAMISEMI. Ninamwomba sana Mheshimiwa Waziri, atengeneze connection kati ya Wizara ya TAMISEMI na Wizara yake kwa kutambua sera mama ili angalau sera hii iende ikatengeneze usimamizi mahiri, kwenye usimamizi kwa upande wa TAMISEMI, Wakurugenzi waweze kusimamia hili zoezi ambalo linatamkwa kwenye sheria lakini halifanyiki vile ambavyo inapaswa kufanyika kwa sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri lazima atambue kwamba mfumo wa usimamizi wa ardhi nchini siyo rafiki sana. Mfumo wa usimamizi wa ardhi nchini hauko rasmi kwa sababu hatuna chombo kinachosimamia Real Estate Regulatory Authority. Hatuna chombo kinachosimamia watu wa Real Estate Agent, hatuna chombo kinachosimamia Real Estate Developers Consultant, hawa brokers ambao wanafanya kazi zao. Nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kuja na RERA. Nimeona sasa wanakwenda kuunda hii taasisi, kuunda mfumo ambao utawaratibu na kuwasimamia hawa watu, hawa watu hawakuwa wanatambulika.

Mheshimiwa Naibu Spika, National Housing anafanya kazi ya usimamizi wa miliki, lakini zipo private company nyingi zinafanya kazi ya usimamizi wa miliki lakini hazitambuliki. Hazina Regulatory ambayo inawaongoza namna nzuri ya kwenda na kwa kutokuwa na usimamizi mahiri maana yake Serikali inakosa kodi, wao wanakuwa hawatambuliki na hata wao wanakosa wakati mwingine mikopo kwenye taasisi za Serikali kwa sababu hawaeleweki wako wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamwomba Waziri hii RERA, Real Estate Regulatory Authority Mheshimiwa Waziri ipe kipaumbele sana kwa sababu watu wengi ambao ni brokers na Real Estate Agent wanakwama kwa sababu ya ukosefu wa kuwa na sheria ambayo inawasimamia.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hili lipo jambo lingine ninaomba nimshauri Waziri. Ni kwenye mkopo wa KKK - kwenye Kupanga, Kupima na Kumilikisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kutoa fedha kwa miaka mingi mfululizo. Tumeona alitoa mara ya mwisho bilioni 50 kwenda kwenye Mamlaka za Upangaji na imetumika kwenye kupanga maeneo mengi nchini na kwenye Halmashauri. Ninamwomba tuzingatie mambo mawili. Pamoja na kuwa tumegundua kwamba kuna changamoto kubwa sana fedha hizi namna ya kurudi, baadhi ya Halmashauri hazirudishi fedha ipasavyo. Ninaomba mambo mawili haya angeyafanyia kazi ili angalau hizi fedha ziendelee kuwa na tija. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza, wakati mikataba inasainiwa kati ya wakurugenzi na Wizara ya Ardhi, lazima TAMISEMI ihusike. Husisha TAMISEMI kama wasimamizi wa Wakurugenzi wale mnaosaini nao mikataba. Pili, anayetakiwa kuhusika, ni lazima umhusishe RAS wa Mkoa ili atambue na akusaidie namna ya kusimamia zile fedha zinazokwenda kwenye taasisi, kwenye maeneo ya Wakurugenzi. Haya mawili Mheshimiwa Waziri akiyafanya, itatusaidia sana kuhakikisha fedha hizi zinarudi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima Wizara ya Fedha ihakikishe na yenyewe inahusika kwenye mkataba ule ili kurahisisha kusaidia zile fedha kurudi kwa wakati. Leo tunatoa bilioni 50, lakini Waziri mwenyewe anaona changamoto namna ya fedha hizi zinavyorudi, hii fedha ni revolving, inatakiwa irudi ili halmashauri zingine ziweze kupewa fedha, lakini hazirudi kwa wakati. Ninaomba sana Mheshimiwa Waziri hili alione na aone namna ambavyo wanaweza wakalifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine Mheshimiwa Waziri nimesema hapa ni Commission ya Ardhi Nchini. Kunakuwa hakuna connection kati ya Wizara ya Ardhi ambao ndiyo wanasimamia policy, TAMISEMI wanaosimamia sheria za utekelezaji wa ardhi, pamoja na watendaji wa maeneo yote mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Commission hii inakwenda sasa kuwa sehemu ya kusimamia yote mawili, inakwenda kusimamia utendaji wa Wizara ninyi wenyewe kwa yale yote wanayozungumza katika kupanga, kumilikisha ardhi, lakini pia inakwenda kuwa sehemu ya katikati kama broker au kuwarahisishia mahusiano yao wao na Wizara ya TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yake ni nini? Kwanza itarahisisha upangaji na upimaji kwenda kwa kasi, itarahisisha master plan ambayo tumeizungumza ya sekta ya ardhi nchini itakwenda kwa kasi, pia itawasaidia kuondoa hilo gap ambalo mnalo kati ya sekta ya ardhi kwa maana ya Wizara ya Ardhi na TAMISEMI nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri kuliona hili, kuanzisha Commission ya Ardhi, nimeona hapa anasema anaianzisha, hii iende kwa kasi kwa sababu kuna wakati hawakutani sekta ya ardhi na mipango au usimamizi wa sera na kule wasimamizi wa utekelezaji wanaotekeleza sheria, hawana namna ambavyo wanakutana ili kuhakikisha haya wanayafanya. Akiwa na Commission ya Ardhi itamsaidia sana Waziri angalau kufanya regulation na kuhakikisha kwamba haya mambo yote yanakwenda sawasawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine amelisema Mwenyekiti wa Kamati hii, juu ya utengano wa watumishi wa ardhi, hasa Maafisa Ardhi, Surveyors, Town Planners, hawa ambao wanaitika wako chini ya Kurugenzi, lakini wanaitika ndani ya Wizara. Huu mkanganyiko kwamba wako chini ya Mkurugenzi kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa, lakini wanawajibika kwenye sekta kwenye Wizara ya Ardhi nchini, kuna mkanganyiko mkubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyosema Mwenyekiti ni kwamba, wakati mwingine Wakurugenzi wanashindwa kuwatambua kama wako chini yao, kuna wakati mwingine wanapata maelekezo kutoka Wizara ya Ardhi juu ya jambo lolote linalotakiwa kufanywa kwenye sekta ya ardhi, hapo hapo anapata maelekezo kwa Mkurugenzi ambaye ndiyo bosi wake kwenye eneo lile la Mamlaka ya Serikali za Mitaa, ile contradiction inawafanya wale watu wanashindwa kuelewa wasimamie lipi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamwomba sasa Mheshimiwa Waziri akae na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI waamue hawa watumishi wakae upande upi. Ndiyo maana maeneo mengi hawa watu wanapata lawama kubwa sana, kwamba wanashindwa kutatua migogoro au wanashindwa ku-meet ile objective ambayo wamewapa ni kwa sababu ya hiyo contradiction, anapata maelekezo kwenye Wizara mbili tofauti, matokeo yake ni kwamba wanashindwa kusimamia na hawajui wasimamie lipi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sana Mheshimiwa Waziri, kwa kuwa hili Wakurugenzi wako chini ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa, wala hakuna sababu, wawarudishe kama walivyokuwa zamani, warudi kule chini ili wasimame kwenye command moja, ikitoka Wizara ya TAMISEMI inashuka mpaka kwa watumishi inakwenda, kuliko hivi ambavyo iko ilivyo hivi sasa. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa mud awa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa ni kengele ya pili.

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie jambo la mwisho kabisa ambalo ni kubwa ninatakiwa kulizungumza ni juu ya kupunguza gharama ya kumiliki ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona wamepunguza kiasi kikubwa sana cha fedha kwa wananchi wanaotaka kumiliki Hati ya Umiliki wa Ardhi nchini, ninamwomba sana hili Kamishna wa Ardhi atoke atoe semina kwa wananchi, ajue namna Mheshimiwa Rais alivyokubali na ameridhia kupunguza bei ya wananchi sasa kumiliki ardhi, zaidi ya asilimia kadhaa kwenye eneo hili ili angalau uweze kuongeza umiliki wa hati na ndiyo sehemu pekee inayoweza kutatua changamoto za ardhi nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana na naunga mkono hoja. Hongera sana kwa Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa nzuri, hongera sana Wizara ya Ardhi pamoja na watumishi wote. Ahsanteni sana. (Makofi)
Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa kutoka kwa Waziri Profesa Mkumbo, lakini pia nipate nafasi ya kuchangia mapendekezo ya mwongozo wa maandalizi ya bajeti kutoka kwa Waziri wa Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kusema ninaunga mkono hoja zote mbili na ninakubaliana na maono yao mazuri yaliyopo kwenye taarifa zao zote mbili kwa Mawaziri hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuridhia na kukubali kuanzishwa mchakato wa Dira mpya ya Taifa ya mwaka 2050. Pia nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa mambo makuu matatu. Moja kwa kutekeleza maono ya Dkt. Samia, maono ya Watanzania na mwelekeo wao na dhamira waliyokuwa nayo juu ya kupatikana kwa dira mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbili, nimpongeze pia Mheshimiwa Waziri kwa kuandaa mpango elekezi na dira yenyewe, kiukweli amefanya kazi kubwa nzuri kama ambavyo tunatambua changamoto ya Dira ya mwaka 2025 ilikwenda kwa kusuasua kwa sababu ya kukosekana kwa mpango elekezi wenyewe ya namna dira inavyokwenda kutekelezwa. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa hilo. La pili, nimpongeze pia kwenye taarifa yake kwa kutambua umuhimu wa wawekezaji hasa wazawa na kurudi kuangalia namna ambavyo Serikali inapaswa kushirikiana na private sectors bila kuwaacha wazawa katika kuinua uchumi wetu kama watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili Mheshimiwa Waziri aende alitazame upya pamoja na kwamba wazawa wanaruhusiwa kufanya kutekeleza miradi iliyo chini ya bilioni 50, ninashauri Serikali ipanue wigo iende zaidi ya bilioni 100 mpaka bilioni 200 kwa sababu ninaamini tunao wazawa ambao wana uwezo mkubwa wa kufanya haya. Tatu, nimpongeze Mheshimiwa Waziri, kwenye taarifa yake na ndiyo jambo muhimu sana la kuanza la kupendekeza walau Wakurugenzi wa Halmashauri kupata nafasi kulingana na uwezo wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu nimeona kwenye Kamati pia wamekwenda mbali wameshauri Wakurugenzi wa Taasisi mbalimbali na Mashirika ya Umma nao waende watazamwe katika nyanda hiyo, wateuliwe kulingana na nafasi zao ili tuweze kuwapima kulingana na ukuaji wa taasisi zao na utendaji wao wa moja kwa moja. Kwa hiyo, kwa kweli nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa taarifa hii. Nina maoni kadhaa kwa malengo mahususi katika dira. Yapo malengo mahususi manne, lakini nitajikita leo kwenye lengo moja tu la maisha bora na ustawi wake kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza dhana ya maisha bora, kama taifa linaloendelea tunatambua yapo maeneo kadhaa ambayo Serikali kwa ujumla wake inapaswa kujikita ili kuinua uchumi wa wananchi kwa ujumla wake. Wizara hii imeonesha mwelekeo na njia ya kupita, ni kazi sasa ya wizara za kisekta kuchukua maono ya wizara hii ya mipango na uwekezaji, kuyachakata na kuyaingiza kwenye mipango ya wizara za kisekta ili yaende yakashamiri na yasambae kwa wananchi kwenye maeneo yote kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye maeneo hayo nilitaka nijikite kwenye maeneo kadhaa. Mfano, tunapozungumzia maisha bora ni lazima uzungumze maisha bora kwa wananchi kwa kutazama miundombinu ya barabara inayozunguka wananchi wale. Katika miundombinu ya barabara lazima tuiangalie kwa nafasi mbili tofauti. Lazima tuangalie barabara zinazosimamiwa na TANROADS, lazima tuangalie barabara zinazosimamiwa na TARURA katika kutekeleza na kupunguza minong’ono na kuimarisha Maisha bora kwa ustawi wa wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utakubaliana na mimi, kuna baadhi ya meneo mengi sasa barabara imekuwa ni changamoto kubwa sana na Waheshimiwa Wabunge wamesema hapa, zipo barabara ambazo zimetangazwa, wakandarasi wapo site, wanatekeleza, zipo barabara ambazo zimesaini mikataba, wakandarasi hawajaingia site na zipo barabara ambazo zipo kwenye procurement process kwenye maeneo mbalimbali. Lazima tukubaliane kwa kuwa Wizara ya Fedha imesema hapa imetoa mwelekeo wake wa uandaaji wa bajeti, watenge fedha ya namna ya ukamilishaji wa barabara hizi kwenye maeneo yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko barabara ambazo tunazungumzia maisha bora kwa wananchi zimetajwa kwa awamu nne, tano kwenye maeneo tofauti toka miaka ya 95 zinatajwa barabara zile, mpaka sasa tuko mwaka 2025 tunakwenda 2030. Mfano wa Barabara yangu ya Utegi - Shirati kwenda Kirongwe ni matarajio yangu sasa Mheshimiwa Waziri, Wizara ya Fedha itatenga fedha kusaidia Wizara ya Ujenzi ili kuimarisha maisha bora kwenye maeneo yale, ili barabara zile ziweze kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara inapokamilika ndiyo inakwenda kuinua uchumi wa eneo husika kwa sababu kuna barabara zinaunganisha kati ya mkoa na mkoa, wilaya na wilaya na zingine zinaunganisha nchi na nchi. Kwa hiyo, katika kuimarisha na kutengeneza maisha bora lazima uweke fedha ya kukamilika kwa barabara ile ili wananchi waweze kupita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni utekelezaji wa miradi ya maji nchini. Niombe sana Wizara husika ya sekta ya maji, ifanye tathmini ijiridhishe badala ya kuwa na tathmini ya namna tumetatua maji kwa asilimia ngapi iangalie upatikanaji wa maji kwenye maeneo yale. Yako maeneo ambayo yana miundombinu ya maji, tunayahesabu kama asilimia katika kutekeleza mpango kazi wa maji, lakini maji hayatoki kwenye maeneo yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo wito wangu ni nini, Wizara ya Maji, kwanza ihakikishe miradi ya maji iliyoanzishwa inakamilika, inakwenda, inafika mwisho na inatoa maji. Mbili, wafanye tathmini kwenye miradi ambayo tayari walipeleka miundombinu badala ya kuihesabu kwenye asilimia ya utekelezaji wa maji wajiridhishe kama miradi hiyo kweli inatoa maji na wananchi wananufaika kwenye yale maeneo. Wakifanya hivyo, maana yake watakuwa wanakwenda kwenye ile itifaki ya maisha bora na ustawi wa wananchi kwa ujumla wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu ni sekta ya ardhi, hili eneo tumekuwa tukilisahau sana. Kipanga, kupima na kumilikisha tumezungumza kwa mda mrefu sana. Niombe Waziri wa Sekta kwenye awamu hii ya bajeti inayokuja, hili jambo liende lipewe msukumo mkubwa kwa sababu ardhi isiyopangwa na kupimwa kwani ndiyo chanzo cha migogoro ya ardhi kwenye maeneo yetu, maana yake kunakuwa hakuna amani kwenye maeneo yetu. Ardhi yetu inakosa thamani halisi pale inapokuwa haijapangwa, kupimwa na kumilikishwa kwenye maeneo yao. Niombe sana Mheshimiwa Waziri husika, aende alione hili tunapokwenda kuchakata bajeti yake ili waweze kulipa nguvu ili waweze kupata ustawi ulio mzuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa hapa jambo la soko la vijana, ajira kwa vijana na nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuanzisha Wizara husika ya Vijana, lakini ningeomba sana Waziri husika pamoja na michakato mbalimbali inayoendelea kwenye Wizara hii, lazima waende wakawa-group vijana, tujue hawa vijana wanaowazungumzia ni kuanzia umri upi mpaka umri gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, twende pia tukazungumze fursa sawa kwa hawa vijana kwa kutazama mazingira ya vijana wanayotoka. Kijana wa Rorya mazingira yake kwenye fursa hayawezi kuwa sana na kijana anayeishi Dar es Salaam. Kwa hiyo, Wizara iende ikajikite itazame kama inakwenda kusaidia vijana, isaidie vijana kulingana na mazingira ya maeneo yao wanayotoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, itazame fursa za kimaeneo hayo wanayotoka hao vijana. Tusizungumze general moja kwa moja kwa kuwa-generalize vijana wote kama vile ni sawa kutokana na fursa wanakotoka. Kijana wa Rorya inawezekana fursa yake isiwe sawa na kijana wa Tandahimba, haiwezi kuwa sawa na kijana wa Kinondoni. Kwa hiyo, ni lazima Mheshimiwa Waziri, aende alione hili namna ambavyo anaweza akaliweka ili litengeneze ustawi ulio mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kwenye mpango, ni kuhusiana na kilimo. Sisi tunazungumza Mkoa wa Mara, leo hii hatuna zao kuu la kibiashara tunalojivunia, tunazo skim mbalimbali za umwagiliaji pamoja na kuzunguka Ziwa Victoria zaidi ya 70%, hatuna skim kubwa ya kuzungumza leo kama kielelezo cha ukuaji wa kilimo kwenye Mkoa wa Mara. Tunatamani Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na mpango huu umekwishaonesha ili waende wakatengeneze upembuzi yakinifu kwenye maeneo yale na sisi tunatamani kupitia mkoa ule tuwe tuna skim ambazo zinawainua wananchi kwenye uchumi na zinaleta manufaa kwenye Wizara hii na kwenye sekta ya kilimo kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri alitazame hili. Mfano, mimi Rorya nimezungukwa na maji 77% lakini ninavyozungumza na wewe hatuna skim yoyote tunayojivunia pamoja na kuzungukwa na maji 77%. Tazama katika 100%, ni 23% peke yake nchi kavu, lakini sina skim yoyote ya umwagiliaji. Kwa hiyo, nikatamani pamoja na kusema, wenzangu wameshauri hapa kuwe na timu ya monitoring and evaluation lakini Wizara ione namna bora ya kusaidia maeneo haya ili waweze kuwasaidia kwenye kilimo, badala ya kubaki na kuzungumza kilimo kwa ujumla wake, lakini maeneo ambayo yana fursa hayanufaiki na kilimo hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ningetamani nizungumzie juu ya uchumi wa kimaeneo na Mheshimiwa Waziri amelizungumza sana hapa kwamba, pamoja na kwamba tunakwenda kuunda timu ya monitoring and evaluation lazima tuangalie maeneo hasa ya kimkoa namna yalivyokaa, ni fursa zipi za kiuchumi ambazo zinaweza zikaanzishwa zikawanufaisha mikoa husika. Mkoa wa Mara hatuna mradi mkubwa kama kielelezo kinavyozungumza, hatuna mradi wa skim ya umwagiliaji lakini viwanda tulivyokuwanavyo vyote vimekufa. Matarajio yetu ni nini kutoka kwa Serikali?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba, Serikali ione namna ambavyo kama fursa yetu ni kufufua viwanda vilivyokuwepo vikiwemo viwanda vya nguo, kiwanda cha maziwa na fursa zingine ambazo zinaweza zikainua uchumi wa maeneo yale. Ningetamani sana nione Wizara hii na Serikali ikiona namna ya kuweka fedha kuinua mkoa ule. Kwa sababu, ukifanya hivyo kwanza unainua ajira kwa wale vijana, lakini pia watatengeneza uchumi wa mkoa wenyewe husika, kuliko namna inavyokwenda kwa ujumla wake na sisi kama mkoa tunabaki tukiwa bado hatujapata kitu ambacho tunaweza tukasema tunajivunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi na ninasema tena kwa mara nyingine kwamba, ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)