Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Jafari Wambura Chege (4 total)

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi. Nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini nina swali la nyongeza. Mradi wa Maji wa Miji 28 Rorya, Tarime umesimama kwa muda mrefu na Mheshimiwa Naibu Waziri atakubaliana nami mradi ule umekwenda kwa kusuasua sana kwa muda mrefu kwa sababu ya ukosefu wa fedha. Je, ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa mradi huo.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Jafari Chege, Mbunge wa Rorya, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa Mradi huu wa kutoka Tarime – Rorya ambao awali tulitegemea mradi huu pia ukatoe huduma maeneo ya Serengeti, Mugumu kule ni kweli umesuasusa. Hata hivyo, Wizara tumechukua hatua ya kukaa na Wakandarasi wakati Serikali ikiendelea kutafuta fedha. Mradi huu Mkandarasi aendelee kuutekeleza ili lengo ni kwamba atakapokuwa ana-raise certificate, basi Serikali itaweza kumlipa kulingana na kazi atakayokuwa ameifanya. Ninakushukuru sana.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa kunipa nafasi. Barabara ya Utegi – Shirati – Kirongwe yenye kilometa 56, kwa bahati nzuri kilometa 27 za Utegi – Shirati zilitangazwa kwa ajili ya ujenzi wa kiwango cha lami. Ninataka nipate status, so far barabara ile sasa imefikia wapi kwa ajili ya ujenzi wa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, hiyo barabara inasubiri tu kufanya signing tutakapokuwa tumekamilisha taratibu zote.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nataka nijue ni lini Uwanja wa Ndege wa Musoma, kama kielelezo cha Mkoa wa Mara, utakamilika?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kutambua umuhimu wa Mkoa wa Mara, ilianza ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Mara. Pale Serikali inajenga runway, kwa maana ya njia ya kuruka na kutua ndege, pia inajenga na majengo mbalimbali. Tayari runway imekamilika, tunakwenda kumalizia majengo yaliyobaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema ninaomba kurejea kauli yangu niliyoitoa siku tano au sita kwamba, kuanzia mwezi ujao au unaofuatia, Serikali ina mpango wa kuanza kufanya testing ya ndege za Shirika letu la Ndege ATCL kwenye viwanja vitatu; Uwanja wa Musoma, Shinyanga na Sumbawanga. Hii ni kuthibitisha dhamira ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwamba, ameamua kuitendea haki nchi hii kwenye sekta ya anga.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kuniona. Barabara inayotuunganisha kati ya Shirati – Minigo na Kata ya Nyamtinga Rung’enye imeharibika kwa muda mrefu na haipitiki kwa sasa. Ninataka kujua Serikali ina mpango gani juu ya ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha changarawe, pamoja na makalavati yanayozunguka barabarani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamhakikishia Mbunge wa Rorya, Mheshimiwa Wambura Chege kwamba, Serikali hivi sasa inafanya tathmini ya barabara zote zilizokatika kufuatia mafuriko na mvua nyingi. Tutatoa kipaumbele kwenye barabara hiyo katika Jimbo la Rorya, kwanza, kupata taarifa za tathmini na mahitaji ya gharama mapema. Pili, kutenga fedha, kwa ajili ya matengenezo, ili barabara iweze kupitika wakati tunaendelea kupanga mipango ya muda wa kati na muda mrefu, kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami kwa kadiri itakavyoonekana inafaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge ninamhakikishia kwamba, suala hilo tumelichukua, tunalifanyia kazi. Meneja wa TARURA wa Mkoa wa Mara na Wilaya ya Rorya wakamilishe tathmini ya barabara hiyo mapema iwezekanavyo na kuiwasilisha Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI kwa sababu, tupo hatua za mwisho za ku-comply yale mahitaji ya kupeleka fedha, kwa ajili ya ujenzi wa barabara hizo. Ahsante sana.