Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Timida Mpoki Fyandomo (4 total)

MHE. TIMIDA M. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya Mheshimiwa John John Nchimbi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na taarifa nyingi kuwa vizimba vya samaki havijengeki Ziwa Nyasa. Swali la kwanza; je, Serikali ipo tayari kupeleka watafiti kwa ajili ya kuchunguza namna ya kufanya ili vizimba hivyo viweze kujengeka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; je, Serikali ipo tayari kuwajengea uwezo vijana wa Wilaya ya Kyela wa kuwahusisha katika minyororo ya thamani ya uvuvi ili kupunguza ukosefu wa ajira kwa vijana katika eneo hilo, lakini pia kuwapa mikopo ya asilimia fulani ya kuweza kupata boti za fibre?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana. Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Timida Fyandomo kwa sababu tangu ameingia Bungeni hapa amekuwa akijitahidi sana kuhakikisha kuwa hoja za vijana zinasikika na sisi Serikali tunazipokea na kuzifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza linahusiana na utafiti juu ya ufugaji wa samaki kwa njia ya vizimba ziwa Nyasa. Ninaomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba ufugaji wa vizimba kwetu sisi Wizara lengo letu ni kuhakikisha kwamba unafanyika katika maziwa yote makuu nchini, lakini na maziwa madogo. Kwa hiyo kwa yale maziwa ambayo bado tunayafanyia tafiti au bado tupo katika taratibu za kuyafanyia tafiti tunaendelea kuhakikisha tunatenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha pia huko tunaweka ufugaji wa samaki kwa vizimba ikiwemo Ziwa Nyasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimtoe wasiwasi, tayari tumeanza utaratibu wa kuhakikisha tunafanya tafiti za kutosha ili kuona namna gani tunaweza tukauanzisha ufugaji huu katika Ziwa letu Nyasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali la pili, amezungumzia suala la boti za fibre kwa vijana wa Wilaya ya Kyela Mkoani Mbeya. Ziwa Nyasa linanufaisha mikoa mikuu mitatu ya Ruvuma, Mbeya na Njombe. Ni kweli kwamba tunahitaji kuendelea kuwawezesha vijana wetu katika wilaya zetu zote za Mbeya na hasa zinazozunguka ziwa hili ili waweze kuingia katika sekta yetu ya uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026, Wizara imetenga shilingi bilioni 9.5 kwa ajili ya kuwawezesha wavuvi kwa kutoa boti hizi za kisasa. Tumetenga bajeti hii kwa ajili ya kununua boti 100 za kisasa na boti 76 shikizi. Nimtoe wasiwasi, kwamba katika wale wananchi 2,100 ambao tumelenga kuwanufaisha kwa fedha hii basi vijana wa Wilaya ya Kyela Mkoani Mbeya nao watanufaika. Ninakushukuru sana.
MHE. TIMIDA M. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Serikali imepitisha vivutio mbalimbali vya kikodi kama Import Duty Exemption, VAT Exemption, Capital Allowance, lakini pia na kuwapa wafanyabiashara na wawekezaji ndani na nje ya nchi the grace period, je, ni kwa nini Serikali inachelewesha kuwaruhusu au kuwapa muda mwafaka wa kutumia zile incentives ambazo wale wafanyabiashara wanakuwa wanataka kuzitumia na wanaruhusiwa kisheria?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili. Je, Serikali ina takwimu ya watu wanaonufaika na vivutio hivi vya kikodi? Kama haina, Serikali inachukua hatua gani kuhakikisha kwamba vivutio hivi haviwanufaishi wachache, bali vinawanufaisha watu wengi wakiwemo vijana? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA (MHE. ENG. MUSHAMU A. MUNDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa vivutio vya kodi katika kuvutia uwekezaji wa ndani na nje. Ni kweli pia kuwa hapo awali kulikuwepo na changamoto zilizosababisha ucheleweshwaji wa utoaji wa vivutio hivyo. Changamoto hizo zilihusisha urasimu wa kiutendaji, ucheleweshwaji wa maamuzi, ukosefu wa utaratibu wa kutosha kati ya taasisi mbalimbali pamoja na mkanganyiko wa tafsiri za baadhi ya sheria na hatua za kuchukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kubaini hali hiyo, Serikali imechukua hatua mbalimbali madhubuti kupitia taasisi mbalimbali ikiwemo TISEZA. Sasa hivi angalau kuna one stop centre ambapo wawekezaji wanaweza wakaenda kuwasilisha maombi yao kuhusiana na vivutio stahiki kwenye sekta ambayo wanaenda kuifanyia biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, kuna ushirikishwaji mkubwa wa taasisi kama TCCIA ambayo pia tunaitumia kwa ajili ya kuwaelekeza wafanyabiashara vivutio stahiki katika maeneo ambayo wanaenda kuwekeza. Jambo hili inaelekea baada ya hatua hizo linaenda kupungua, na hivyo vivutio vitatoka kwa wakati, hasa kwa startups kama vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuhusiana na takwimu, Serikali kweli inatoa vivutio hivyo, hususan kwa vijana. Hata hivyo, kwa sasa hatuna takwimu zinazoonesha asilimia ambayo inatupa picha ya wale ambao wamefaidika na vivutio hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vivutio hivyo vimekuwa vikitolewa, lakini mtazamo siyo vivutio, tathmini imekuwa ikitolewa kwa kuangalia mtazamo mpana kuliko kuangalia asilimia ya watu ambao wanafaidika. Kwa mfano, kwa kuangalia ajira na shughuli za kiuchumi katika jamii. Kwa sasa tunafikiri Wizara ya Fedha inaweza ikapata takwimu nzuri zaidi pale ambapo sasa tumeanza kutumia mfumo wa IDRAS ambao unachukua takwimu za walipa kodi wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, tuko na utaratibu wa kuwaelekeza, na hapa nielekeze kwa dhati kabisa wenzetu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania, waweze kuanzisha utaratibu. Ninajua upo utaratibu wa mafunzo kwa wafanyabiashara, hasa vijana ambao wanaanza biashara kwa sasa, hasa kipindi hiki ambacho Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kuwawezesha vijana hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipokuwa na takwimu na vijana hawa wasipopata mafunzo stahiki kwa ajili ya kutumia zile fedha, zile fedha zitakuwa kama zile ambazo Wabunge tulikuwa tukilalamikia hapa, kwamba, fedha za 10% ya mapato ya ndani ya halmashauri zimekuwa zikienda na maji bila habari kutokana na vijana kuchukua fedha bila kuwa na maarifa stahiki ya kutumia fedha hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi bilioni 200 lazima zilete tija kwa vijana. Kwa hiyo, nawaambia na kuwahimiza Mamlaka ya Mapato Tanzania, pamoja na jitihada wanazofanya za kuwapa mafunzo na kutoa vivutio hivyo ambavyo nimeviongelea, watoe mafunzo stahiki kwa vijana, ili mwisho wa siku shilingi bilioni 200 zilete tija kwao. Pia, kama tunavyosisitiza, wawe ni wajasirimali ambao wanakuja ku-graduate kuwa wafanyabiashara wakubwa watakaoleta tija na kuinufaisha nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. TIMIDA M. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza. Tangu kuanzishwa kwa kodi hii, idadi ya kontena za vinea ambazo zimekuwa zikisafirishwa zimepungua kutoka kontena 3,765 mpaka kontena 2,110 mwaka 2026 hadi mwezi huu Machi. Je, Serikali imefanya tathmini ya kulinganisha mapato inayopata kupitia kodi hii dhidi ya ajira zilizopotea kwenye viwanda vya misitu?
WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba kunakuwa kuna haja ya kufanya tathmini kwenye athari ambazo zimetokeza kutokana na hatua hizi. Hata hivyo, kama nilivyoeleza katika jibu langu la msingi, dhamira moja ya hatua hii ilikuwa ni kupunguza usafirishaji nje ya nchi. Kwa hiyo, kutokana na alichokisema Mheshimiwa Mbunge, inaonekana kweli upande mmoja tumefanikiwa, lakini upande wa pili tunahitaji kufanya tathmini kuona sasa zile faida ambazo zilitarajiwa kama zimepatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kama ambavyo imesemwa hatua hii ilianza kutekelezwa mwezi Julai, 2025, vipindi ni vifupi kufanya tathmini. Tunalipokea na kwamba tutafanya tathmini kama nilivyosema awali, sisi kwa ushirikiano na Wizara ya Utalii na Maliasili.
MHE. TIMIDA M. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Waziri katika nchi za Umoja wa Ulaya, taasisi zinazofanya kazi na Serikali zinapaswa kufanya malipo ya madeni ndani ya siku 30, lakini pia riba hulipwa moja kwa moja endapo malipo yatacheleweshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali yangu ipo tayari kuandaa Prompt Payment Policy ya Taifa ili kuhakikisha wazabuni, wakandarasi, wafanyabiashara hususan vijana na SMEs wanalipwa ndani ya muda maalum unaotambulika kisheria ili kulinda mitaji ya vijana na wananchi wanaofanya biashara na Serikali? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA (MHE. LAURENT D. LUSWETULA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwanza nipongeze sana Mbunge wa Viti Maalum dada yangu Timida ambaye ni Mbaraza la Vijana wa Taifa kutokea Mkoa wa Mbeya kwa namna anavyoendelea kujenga hoja makini hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikirejea kwenye swali la nyongeza, kwanza kabisa miongoni mwa vitu ambavyo hata Kamati yetu ya Bajeti imeweza kutushauri kama Wizara ya Fedha na kama Serikali imetushauri tuweze kupunguza angalau muda wa uhakiki wa madeni ya wazabuni na wakandarasi na watoa huduma mpaka kufikia siku 21.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na sisi tumeweza kupokea, lakini siku hizi 21 zinaweza zikapungua au kuongezeka kutokana na sababu kadhaa ikiwemo ukamilifu wa nyaraka, aina ya madeni lakini pia ushirikiano wa wadau kwa maana wadai pamoja na wadaiwa, lakini pia umri wa deni pamoja na wigo wa deni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali, kama ambavyo nimejibu kwenye swali langu la msingi, tumeendelea kulipa madeni ya wazabuni, wakandarasi pamoja na watoa huduma na mpaka kufikia Februari, 2026 zaidi ya shilingi bilioni 477.6 ambazo tayari wakandarasi hawa na watoa wa huduma wamekwishalipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya vipaumbele vikubwa vya Serikali katika bajeti yetu ya mwaka 2026/2027, tumetenga na tumekubaliana kuwa na mkakati wa kutenga shilingi bilioni 100 kila mwezi kwa ajili ya kulipa madeni ya wakandarasi, watoa huduma pamoja na wazabuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha.