MHE. ALAN T. MVANO: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ya Kakonko Mkoa wa Kigoma tunao uchimbaji wa madini ya dhahabu Kata ya Nyamtukuza, Vijiji vya Nyamtukuza maeneo ya Nyamwilonge. Tarehe 10 Disemba tulikwenda na Mkuu wa Mkoa pale na akazuia shughuli za uchimbaji kwa sababu zilikuwa zinakiuka sheria za mazingira na zinaathiri wananchi wa Vijiji zaidi ya saba vya Kihomoka, Kumwiyando na Vijiji vingine vya Bwera mpaka Nyamwilonge. Je, ni hatua gani zimechukuliwa na Serikali ili kunusuru maisha ya wananchi hao kwa sababu mto ule haufai kabisa kwa matumizi ya binadamu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala la uchimbaji wa madini linaendeshwa kwa mujibu wa sheria na suala la uhifadhi wa mazingira linasimamiwa kwa mujibu wa Sheria, Sura ya 191.
Mheshimiwa Spika, ninaomba nitumie nafasi hii kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Kakonko kwamba kipaumbele cha kwanza ni kutunza mazingira, lakini Serikali itaendelea kuhakikisha inaweka mazingira wezeshi kwa wachimbaji wa madini ili kunufaika na rasilimali za madini vilevile kutunza mazingira katika maeneo hayo. Tutawasiliana na Ofisi ya Wizara ya Madini ili tuweze kuliweka sawa na wananchi waweze kuendelea kuchimba madini.
MHE. ALAN T. MVANO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa nipongeze na nishukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa taarifa, Mkoa wa Kigoma umekuwa ukizalisha zaidi ya tani milioni moja za muhogo kwa mwaka. Wilaya ya Kakonko imekuwa ikizalisha zaidi ya tani 184,000 na Wilaya ya Kibondo mathalani zaidi ya tani 174,000.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza la nyongeza; je, Wizara ya Kilimo ina mpango gani wa kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara ili kupanua wigo wa masoko ya zao hili la muhogo ndani ya Wilaya ya Kakonko na Mkoa wa Kigoma? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa bei ya zao la muhogo ilianguka sana, kutoka kuuzwa shilingi 800 hadi 1,000 kwa kila kilo moja kwenda kuuzwa shilingi 150 hadi shilingi 200. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwanusuru wananchi ambao ni wakulima wa zao la muhogo ambao hadi sasa wameshindwa kuvuna zao hilo, kwa sababu hata wakivuna hawawezi kuuza kwa bei iliyoko sokoni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze pia bwana Alan Mvano ameanza vizuri kuwafuatilia wananchi wake wa Jimbo la Kakonko na ninaomba nimjibu kwamba, moja sisi kama Serikali, Wizara ya Kilimo pamoja na Wizara ya Viwanda na Biashara tumekuwa tukifanya kazi kwa ukaribu sana. Ndiyo maana utaona katika moja ya hatua ya awali sisi ambayo tunaifanya sasa hivi ni jukumu la kujenga soko katika Halmashauri ya Kakonko. Wizara ya Viwanda na Biashara itakuja ku-complement jambo hili kwa kujenga viwanda ambavyo vitasaidia wakulima katika eneo hilo. Kwa hiyo, huo ni mpango ambao upo na ni endelevu kwa muda wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mpango wa Serikali baada ya bei kushuka; mpango wa Serikali ndiyo huo ambao tumeainisha kwamba kwa nini tunajenga soko. Lengo ni kuhakikisha kwanza moja, tunaongeza thamani, ndiyo maana utaona tumeainisha hapa kwamba tunataka wananchi waongeze tija kwa kuchakata yale mazao yao yaweze kudumu kwa muda mrefu ambapo tunaamini kwamba ukishakausha muhogo badala ya kuuza katika bei ya chini unaweza ukakaa kwa muda mrefu na ukapata bei ambayo ni nzuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sisi kama Serikali, jambo hili tunalifahamu na tunalifanyia kazi kwa ukaribu kabisa. Kwa hiyo, tu nimthibitishie tu Mbunge kwamba moja ya kazi kubwa ambayo tutaendelea kuifanya katika eneo hili ni kuboresha haya mazingira ili bei ya muhogo isiweze kushuka kama ambavyo ameainisha hapa.