Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Fadhili Fabian Ngajilo (1 total)

MHE. FADHILI F. NGAJILO: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa kupewa nafasi hii kuuliza swali la nyongeza. Mkoa wa Iringa unasemekana una maeneo yenye madini. Ukienda mfano Ihomasa, Ihandutwa, Sinai, Ulata, Mtera, Kitonga, Image na maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Iringa. Swali, je, ni lini sasa Serikali wataifungua na kuipa kipaumbele Iringa ili mkoa huu ujulikane ni mkoa wa madini kwa kufanya mining survey lakini kutangaza maeneo yenye madini na kuwawezesha vijana kwa teknolojia ya kuchimba madini na kutengeneza mabilionea kutoka mkoa wa Iringa?
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, ninampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa swali lake zuri na nimjulishe tu kwamba Iringa nayo ni mikoa yetu ya kimadini, wana madini ya aina mbalimbali na nimpe ushauri kwamba atembelee Kituo chetu cha Jiolojia (TGC) pale GST kwa sababu kuna kitabu ambacho huwa kinahuishwa kila baada ya miaka mitatu, kinachoeleza madini yanayopatikana katika kila eneo la nchi yetu ikiwepo Mkoa wa Iringa.

Mheshimiwa Spika, hatuishii hapo tu, tuna wachimbaji wadogo wengi pale Iringa, eneo la Nyakavangala ambalo lipo katika Jimbo la Mheshimiwa Lukuvi, tayari ambako kuna wachimbaji wa dhahabu na madini ujenzi. Hivyo ni wajibu wetu kama Wizara kuendelea kutoa elimu kwa vijana ili waingie katika sekta hii kwa wingi, kwa sababu madini haya yanaenda kubadilisha sura ya uchumi wa wananchi wetu na vijana hasa ambao wanahitaji ajira.

Mheshimiwa Spika, kwa suala la survey, sisi kama Wizara ya Madini kwa maelekezo ya Rais tuko katika mchakato wa mwisho wa kununua ndege yetu wenyewe ya kufanya survey, lakini pia tuna wadau wa sekta binafsi ambao wameanza kurusha ndege, wameanza kurusha helikopta, wameanza pia kurusha na zile ndege nyuki katika kutafuta madini yalipo katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Tumeshafanya hivyo Shinyanga, wiki iliyopita na maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, ninaomba kuwasilisha.