Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025
MHE. BENJAMIN L. NGAYIWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii pia kukushukuru kwa kunipatia nafasi hii ya kuchangia katika mjadala wa kujadili hotuba ya Mheshimiwa Rais ambayo aliitoa wakati wa kufungua ama kuzindua Bunge letu la Kumi na Tatu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninakupongeza kwa kuteuliwa kwako kuwa Naibu Spika wetu. Pia ninampongeza Waziri Mkuu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba kwa nafasi hiyo ambayo anaitumikia. Nichukue fursa hii pia kuwashukuru wapigakura na wananchi wenzangu wa Jimbo la Kahama Mjini kwa imani yao kubwa waliyonipatia kwa kunichagua kuwa mwakilishi wao Bungeni.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo ni siku njema ambayo tunajadili hotuba ya Mheshimiwa Rais, lakini ni siku pia ya kumbukizi ya kuzaliwa kwake. Kwa hiyo, tunampongeza na kumwombea maisha marefu huko aliko, aendelee kututumikia Watanzania kwa moyo wote kama ambavyo ameonesha kwa kipindi chote.
Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba hii ya Mheshimiwa Rais ni hotuba ya kwanza kabisa aliyoitoa tangu tulipomaliza uchaguzi wetu mkuu tangu Oktoba, 2025. Hotuba hii iliakisi na kugusa maeneo karibu yote muhimu ya kisekta katika kuonesha Dira ya Maendeleo ya Taifa letu na kuinua hali ya uchumi kwa mwananchi mmoja mmoja katika Taifa letu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sote ni mashahidi, Mheshimiwa Rais alipogusia kwa mfano, katika sekta ya ujenzi aliposema na ninamnukuu hapa anasema; “Tutaongeza pia bajeti na uwezo wa TARURA katika kuboresha barabara za ndani na za vijijini ili kuhakikisha zinapitika mwaka mzima na kuwa wakulima wanaweza kuyafikia masoko kwa urahisi.”
Mheshimiwa Naibu Spika, humu Waheshimiwa Wabunge tulimpongeza kwa kumpigia makofi mengi sana, ikionesha kwamba shida kubwa au sehemu kubwa ambayo inatakiwa tuelekeze nguvu zetu ni katika kuboresha miundombinu yetu hasa barabara za ndani na zile za vijijini. Mheshimiwa Rais ameonyesha dhamira hiyo ya kuongeza bajeti kwa TARURA.
Mheshimiwa Naibu Spika, TARURA hii ikiwa na umri wa miaka minane, kwa kweli imefanya kazi nzuri sana, lakini bado tunatakiwa kuendelea kufanya kazi iliyo bora zaidi na katika kuonesha kwamba tunamuunga mkono Mheshimiwa Rais katika adhima yake ya kuboresha hali ya miundombinu yetu ambayo yeye anatamani ipitike kwa mwaka mzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi ninawaomba tu watendaji wetu katika ngazi zote kwamba Mheshimiwa Rais anapohangaika usiku na mchana kutafuta fedha kwa ajili ya maendeleo, basi na sisi tuoneshe ile nia thabiti na dhamira ya kwenda kumuunga mkono katika kusimamia shughuli hizi za maendeleo ili wananchi wetu waweze kufaidika na jitihada hizi za Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikijielekeza katika ukurasa wa 25 wa hotuba ya Mheshimwa katika sekta ya madini, pia Mheshimiwa Rais ameonyesha kutambua mchango wa sekta ya madini katika maendeleo ya Taifa letu. Katika hotuba yake inaonesha kwamba kiwango cha mchango wa sekta ya madini katika pato la Taifa, kiliongezeka kutoka asilimia 6.8 mwaka 2020 mpaka kufikia asilimia 10.1 mwaka 2024.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ameonesha utayari wa kuwaunga mkono na kuwa-support wachimbaji wadogo kwa kuwawezesha kuwapatia vifaa vya uchimbaji kama vile vya uchorongaji, lakini na taarifa za jiolojia kuonesha kwamba madini yanapatikana wapi? Kwa wingi gani? Ni madini ya aina gani?
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ninaiomba tu pia Wizara yetu ya Madini iende ikasimamie vizuri eneo hili kwa kuhakikisha kwamba ile mikopo ambayo Serikali inaenda kuitoa kwa wachimbaji wadogo, iende basi kwa walengwa ambao kweli wana uhitaji, mikopo isiende kwa wachimbaji ambao tayari wana uwezo wa kujiendesha wao wenyewe na kuendesha shughuli zao za uchimbaji, na tuende tukawaangalie wale vijana ambao wapo katika hali za kati ambazo sasa wanataka kupambana kuweza kuona kwamba wanaongeza tija ya uzalishaji katika sekta hii ya madini.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni wazi kwamba hata asubuhi wakati wa michango ya Waheshimiwa Wabunge walieleza kuhusu masuala ya mirabaha ambapo wachimbaji wanaonekana wanatozwa mirabaha mara mbili pale ambapo wanakuwa wameshatoa mawe juu, lakini pale ambapo wanakuwa wameshachenjua dhahabu na penyewe pia dhahabu inaenda kutozwa mrabaha tena kwa mara nyingine.
Mheshimiwa Niabu Spika, kwa hiyo, tuende tukaangalie maeneo haya ili wachimbaji wetu, sisi kule usikumani tunaita wasitegemee tu miganyalo. Miganyalo ni zile posho ndogo ndogo zinazopatikana kwa wachimbaji hawa wadogo wanapokuwa wanachimba katika maeneo yao hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa jitihada kubwa ambazo anazifanya na hotuba hii iende ikawe dira kwa taasisi zote za Serikali, taasisi binafsi, Wizara zote, tuweze kwenda kupita humu ambapo Mheshimiwa Rais wetu ameonesha dira kwamba sasa tunataka kuelekea upande gani?
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051, Mapendekezo ya Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/2027–2030/2031 na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2026/2027; na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali Katika Muda wa Kati ya 2026/2027 hadi 2028/2029.
MHE. BENJAMIN L. NGAYIWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ili nichangie katika Mpango huu wa Taifa wa Maendeleo. Awali ya yote ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kunijalia uhai na afya njema lakini pia niendelee kuwashukuru wananchi wema wa Jimbo la Kahama Mjini ambao walinichagua na kuniamini ili nije kuwa mwakilishi wao katika Bunge hili Tukufu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru pia familia yangu kwa maana ya mke wangu Happiness Kalugaba, lakini na Mama Gaudensia Ngayiwa na Mzee Ngayiwa Pascal Maziku na ndugu na jamaa wote wanaoendelea kunitia moyo katika kuwatumikia wananchi wa Jimbo la Kahama Mjini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nijielekeze sasa katika kuchangia mapendekezo ya Mpango huu elekezi wa maendeleo wa muda mfupi, muda wa kati na mrefu. Niseme tu kwamba Mpango huu umetambua rasilimali zetu ambazo tupo nazo katika Nchi yetu tukufu ya Tanzania. Rasilimali hizo ni uoto wa asili; ardhi kubwa ambayo ina rutuba inayo support kilimo cha aina zote kwa maana ya mazao ya chakula na mazao ya biashara, lakini tuna water bodies ambayo ni mito; maziwa lakini na bahari ambayo yote haya yana support shughuli za uvuvi na kilimo lakini na matumizi mengine ya nyumbani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hoja yangu hapa, ninaamini Serikali yetu ambayo inaongozwa na Mheshimiwa mama yetu Rais mpendwa Mama Samia, ipo na nia thabiti na ya dhati katika kuwatumikia wananchi wetu. Kwa hiyo, hapa nishauri tu katika mikataba ambayo inajumuisha rasilimali zetu hizi nilizozitaja basi ipitie katika Bunge hili ili Wabunge tuweze kutoa ushauri wetu kwa sababu mikataba inayohusu rasilimali, inahusu pia kizazi chetu na dira hii ya maendeleo ya miaka 25, tunapoongelea mtoto wa miaka mitano, leo baada ya miaka 25 kufikia 2050 atakuwa ni mtoto mwenye miaka karibu 30. Sasa tunakuwa na Mpango huu wa maendeleo ambayo kwa kweli umelenga katika kuendeleza kizazi chetu ambacho kitakuja kunufaika na rasilimali hizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mpango huu wa maendeleo umeweka vichocheo vya maendeleo ambavyo ni imetambua kuhusu nishati, logistics kwa maana ya uwekezaji katika miundombinu lakini sayansi na teknolojia, mageuzi ya kidijiti, mazingira ya biashara na uendelezaji wa uwekezaji katika kuboresha mifumo ya kisheria na kukuza ubia kati ya sekta za umma na sekta binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapa niseme tu kama wachangiaji waliotangulia kuchangia, idadi ya vijana kwa maana hawa ndiyo wabeba maono na watekelezaji wa huu Mpango wa Maendeleo wa Muda Mfupi, Muda wa Kati na Muda Mrefu. Hawa vijana kati ya umri wa miaka 15 na 35 ni zaidi ya 60% na hawa ndiyo nguvu kazi: kwa maana wale watoto na wazee ni tegemezi kwa nguvu kazi hii. Kwa hiyo, ni lazima tuangalie sera na mpango wetu katika kuwawezesha vijana wetu, waweze kuingia moja kwa moja katika kutumia hizi rasilimali nilizotaja hapa ikiwemo madini; ikiwemo rasilimali zetu za ardhi, lakini na maji ambayo tupo nayo katika mito, maziwa na bahari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Serikali kupitia Wizara na ninashukuru kwamba Wizara ya Vijana imeanzishwa, kwa hiyo tuweke sera ambazo zitaenda kuwawezesha vijana wetu kwa mitaji, lakini kuwawezesha vijana wetu kwa skills kwa maana ya teknolojia ili waweze kuhimili ushindani wa kibiashara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliposema kwamba tuboreshe miundombinu…
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.
MHE. BENJAMIN L. NGAYIWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi Jimbo langu la Kahama Mjini…
MWENYEKITI: Mheshimiwa Benjamin, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Esther Matiko.
TAARIFA
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru. Nilitaka kumpa taarifa mchangiaji, anachangia vizuri kabisa kwenye kuishauri Serikali jinsi ya kuhakikisha kwamba vijana ambao ndiyo nguvu kazi wanawezeshwa kuhakikisha kwamba wote wanakuwa ni wazalishaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa takwimu za sasa hivi 87% ya population tuliyo nayo ni tegemezi, kwa maana watoto chini ya miaka 15 na wazee kuanzia miaka 65. Kwa hiyo, wazalishaji tu ni 13%, sasa Serikali ikichukua hizo takwimu ikazifanyia kazi kwa vile anavyosema mchangiaji pale ni hakika sasa hii percent ndogo ambao ndio wazalishaji ambao ndiyo wanabeba jukumu kubwa la kuwasaidia hao wengine ambao ni tegemezi itasaidia kukwamua hilo eneo ambalo linategemea sana 87%.
MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Benjamin, taarifa ya Mheshimiwa Matiko, unaipokea?
MHE. BENJAMIN L. NGAYIWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea na ninaomba niendelee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naongea hapa kuhusu uboreshaji wa miundombinu, lakini na mazingira ya kibiashara. Pale Jimboni kwangu Kahama ni jimbo zuri na lina watu ambao wanajituma sana katika kufanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Serikali iwawezeshe wafanyabiashara pale ambao Mji wa Kahama ni kama lango la kuingia na kutokea katika nchi yetu ambayo inaunganisha Nchi zaidi ya nne; tunaunganisha Burundi, Rwanda, Kongo, Sudani na Uganda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa pale ningeomba sana wafanyabiashara wale wawezeshwe kwa mitaji, lakini na zile kodi, sipingi kwamba Serikali ikusanye kodi, lakini tuangalie namna ya kuwawezesha wafanyabiashara wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale pia kuna ujenzi wa ghala la biashara kwa maana ya kuweka kitovu cha kuuza mazao ya biashara na chakula nchi jirani. Ninaomba lile soko liweze kumaliziwa, lakini na miundombinu kama ambavyo Mheshimiwa Rais, alieleza katika hotuba yake ya ufunguzi wa Bunge, kwamba ipitike muda wote wa mwaka mzima wa kiangazi na masika, basi twende kuiboresha ili wananchi wetu waweze kusafirisha mazao yao kutoka sehemu nyingine na kufanya biashara bila bugudha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba, wawekezaji kupitia EPZ na SEZ wawezeshwe wapunguziwe masharti ili waje nchini waweze kuwekeza. Pale Kahama tuna kongani ya viwanda pale katika Mgodi wa Buzwagi. Wawekezaji wapunguziwe masharti waje wafungue viwanda, waweze kuzalisha ajira kwa vijana wetu na hapo Serikali inaweza ikaanza kukusanya kodi kwa maana ya kwamba zile raw materials wanazozitumia, lakini na huduma nyingine kwa maana ya service levy, watakuwa wameweza kulipia na wakati huo huo wakiwa wameajiri sehemu ya vijana wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, waache kucheza mabonaza vijana wetu, kwa sababu mabonaza haya kwanza ninapendekeza hata Serikali iangalie kuyatokomeza kabisa, yasiwepo katika nchi yetu ya Tanzania. Mabonaza haya yamekuwa tu mufilisi kwa vijana na wananchi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ninaomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)