Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Benjamin Lukubha Ngayiwa (1 total)

MHE. BENJAMIN L. NGAYIWA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali kuhusu kuboresha huduma katika hospitali yetu ya Manispaa ya Kahama, ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; Mheshimiwa Naibu Waziri amesema Serikali inatenga bajeti kwa ajiili ya kuboresha huduma kwa kujenga jengo la dharura na kuweka vifaa vya uchunguzi kwa maana ya CT- Scan. Sasa ni lini Serikali ina mpango wa kupeleka CT- Scan kwenye hospitali hii ambayo inapokea wagonjwa wengi sana kutoka hospitali zingine?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; ni lini sasa Serikali ina mpango wa kuboresha na kukamilisha majengo ya zahanati ambayo yamefikia hatua za lenta kama vile Chalya, Nyandekwa na sehemu zingine za Wilaya yetu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. JAFAR R. SEIF): Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ngayiwa. Kwanza, ninampongeza Mjumbe wa Kamati ya TAMISEMI anatoa michango mizuri kwa ajili ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kweli kwa idadi kubwa ya wagonjwa ambao tunawapokea katika hospitali hii ya Halmashauri ya Manispaa ya Kahama na uhitaji wa CT- Scan kwa ajili ya upimaji, uchunguzi wa mifupa kwa wagonjwa wetu, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa maana ya kwamba ndani ya muda mfupi Serikali imekwishafanya tathmini na uhitaji huo tumeshauona, tunaipeleka CT-Scan pale ili iende kutoa matibabu kuwahudumia wahitaji wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu zahanati nilikwishaeleza hapa kwamba zaidi ya zahanati 1,841 zinakwenda kufanyiwa ukarabati na kumaliziwa maboma, Serikali inajielekeza zaidi katika miradi hii ambayo tayari imekwishaanzishwa ili tuweze kuikamilisha kabla ya kuanza miradi mingine ya zahati na vituo vya afya. (Makofi)