MHE. TWAHA S. MWAKIOJA aliuliza:-
Je, ni lini Tembo wanaojeruhi na kuharibu mali majumbani na mashambani maeneo ya Mwakijembe, Bwiti, Daluni na Duga watadhibitiwa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Spika, awali ya yote ninaomba kumshukuru sana sana Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uhai na kuingia katika awamu hii tukiwa salama.
Mheshimiwa Spika, pili, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuniamini. Ninatoa ahadi kwamba nitafanya kazi kwa weledi mkubwa, uadilifu pamoja na ufanisi mkubwa sana.
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutekeleza mkakati wa kitaifa wa kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu katika Wilaya ya Mkinga Mkoani Tanga. Mkakati huu unajumuisha kuweka vikosi vya kudumu vya askari katika Kata za Bwita na Mwakijembe kwa ajili ya mwitikio wa haraka wa matukio ya wanyamapori katika eneo hilo.
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea pia kutumia teknolojia za kisasa hasa visukuma mawimbi (GPS Collars, ndege nyuki pamoja na mabomu baridi katika kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu hususan tembo katika Wilaya ya Mkinga. Ahsante sana.