MHE. TWAHA S. MWAIKOJA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali ningependa kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; Taasisi zetu za Serikali za TANAPA, NCAA na TAWA zinabaki na mapato ili kuweza kutoa huduma mbalimbali. Pamoja na kubaki na mapato (retention) bado tumekuwa na changamoto ya kuwapa waathirika hawa wanaokumbana na majanga haya ya wanyamapori kifuta jasho ambacho ni kidogo na kiwango hiki ni cha muda mrefu sana. Je, Serikali haioni haja sasa ya kufanya mapitio juu ya viwango hivi?
Mheshimiwa Spika, swali la pili; utaratibu wa kufanya uthamini kwa wananchi wanaopata majanga umekuwa na urasimu mkubwa sana na kusababisha baadhi ya wananchi kushindwa kufuatilia na kuendelea kuilalamikia Serikali yetu. Je, Serikali haioni haja sasa ya kufanya mapitio juu ya mchakato huu ili uwe rahisi na kuwaletea tabasamu wananchi wetu na hususan wananchi wa Jimbo la Mkinga? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kabla ya kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Twaha Mbunge wa Mkinga, ninaomba nimpongeze sana pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuaminiwa na wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Serikali ilishafanya marekebisho ya Kanuni ya Mwaka 2011, kanuni hiyo ilionekana ni kweli kifuta jasho ni kidogo imefanyiwa marekebisho mwaka 2024 kwa Tangazo la Serikali Na. 440, mwaka 2024, tarehe 31 Mei na imefanya marekebisho makubwa. Kwa sasa waathirika wale ambao watakuwa na ulemavu wa muda mfupi yaani majeraha ya muda mfupi watalipwa 50%, vifo vya mifugo 50%, uharibifu wa mazao 50%. Pia lipo ongezeko kubwa la vifo na ulemavu wa kudumu kwa 100%.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, Serikali tayari imeliona hilo suala la urasimu na kwa sasa tunatumia mfumo maalum unaotambulika kwa jina la PAIS yaani Problem Animal Management Information System ambao sasa urasimu hautopatikana, maana yake inarekodi moja kwa moja na kuhakiki taarifa zile na kupelekwa kwenye kanzidata. Nina imani kabisa kwamba urasimu huo sasa utakuwa umepata mwarobaini wake. Ahsante sana.