Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. YUMNA MMANGA OMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi hii. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema ya uhai na uzima, lakini kwa kunipatia kibali cha kuwa miongoni mwa Wabunge wa Bunge hili la Kumi na Tatu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwa heshima kubwa nipende kumshukuru kipenzi chetu Mama yetu, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha nimshukuru pia Mama yetu, mlezi wetu Mama Mary Pius Chatanda, kiongozi na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania kwa uongozi wake ulio thabiti na kutulea sisi mabinti na wanawake ndani ya jumuiya hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo sasa nielekee moja kwa moja kwenye kuchangia hoja iliyopo mezani ambayo ni hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Mimi nitagusia vipengele viwili ambavyo ni sekta ya elimu na sekta ya afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijakwenda moja kwa moja nipende tu kuipongeza Serikali kwa hatua kubwa za maendeleo inayoendelea kuzipiga katika sekta hizi. Pia, kama Taifa tulipo sipo tulipotoka, lazima tukiri hilo ila sipo tunapotaka kufika. Kwa hiyo inatulazimu tuseme ili tuweze kufikia kule tunapotaka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, inazungumzia kwamba kupitia Wizara ya Elimu, Serikali imetenga shilingi bilioni tisa kwa ajili ya ufadhili wa wanafunzi kwa masomo ya Sayansi, Teknolojia, Uhandisi, sambamba na Hisabati ambapo Serikali imefadhili wanafunzi 1,786. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, imetoa pia shilingi bilioni tano kwa Samia Super Scholarship Fund kwa wanafunzi 50 bora kwa sekta ya akili unde na Sayansi data. Hapa napatwa na maswali, kwenye ufadhili huu wanafunzi wenye ulemavu wamefikiwa kwa kiasi gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunafahamu kwamba, ndugu zetu watoto wetu wenye ulemavu wanakumbana na changamoto mara tatu zaidi kuliko wanafunzi wengine, kuanzia elimu ya msingi hadi elimu ya juu na ndiyo maana hata ukitazama takwimu zimejichora kabisa pyramid kwamba huku ngazi ya chini wanakuwa wengi, lakini kutokana na changamoto mbalimbali ikiwemo miundombinu, vifaa saidizi, uelewa, mazingira, vinawarudisha nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kumwangalia mwanafunzi mwenye ulemavu ambaye amepata division two, ukam-recognize sawasawa na asiyekuwa na ulemavu ambaye ana division one. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila shaka huyu ametumia nguvu mara tatu zaidi afikie pale highest of his/her potential. Kwa hiyo, ni ombi langu kwa Serikali kuhakikisha kwamba fursa hizi tunaweka mikakati madhubuti (affirmative measures) ambazo zitaongeza ushiriki wa wanafunzi wenye ulemavu kwenye fursa hizi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukizungumzia science technology engineering and mathematics ni uchumi wa nchi, tunapoliacha kundi hili nyuma, maana yake tunawaacha nyuma katika ushiriki wao wa uchumi ndani ya Taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuendelea mbele nigusie sekta ya afya; ambapo tumeona Serikali kwa kuimarisha ubora wa sekta ya afya nchini, imesomesha madaktari bingwa na bingwa bobezi kwenye kada mbalimbali. Nipende tu kutoa ushauri wangu kwa Serikali kwamba madaktari hawa waende wakagusie kada ambazo zinatugusa sisi watu wenye ulemavu moja kwa moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaathiriwa na mionzi ya jua; mionzi hiyo hupenya hadi kupitia kioo, hata kunapokuwa na mawingu ya mvua, bado hupita. Hivyo basi, ninahitaji kuwa na periodic check up ambazo zitaniwezesha kuangalia uwezo wa ngozi yangu, kwa kuwa ninafanya kazi siwezi kuepuka jua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama binadamu ninakonda, ninanenepa, ninakua ule mguu bandia ambao umenipatia unaweza ukawa haunitoshi ni lazima niende kwa daktari kila baada ya muda akaangalie, aniongezee, anipunguzie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zetu wenye ulemavu wa uziwi pia wanahitaji kwenda kwa daktari kuangalia zile shime sikio waliozopatiwa zinawasaidia? Wapewe nyingine. Ndiyo maana idadi kubwa ya ndugu zetu wenye ulemavu wa uziwi hawataki kutumia shime sikio kwa sababu madaktari hawa hawapo ni pungufu kwa kiasi kikubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi, ni mapendekezo yangu kwa Serikali kuhakikisha kwamba wanaongeza madaktari bingwa kwenye kada hizi ili kupunguza, lasivyo tutakuwa tunaongeza intensity ya ulemavu kwa watu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie kwamba, tunapoandaa bajeti zetu tuhakikishe kwamba hizi bajeti zinakuwa inclusive budget ili katika kila eneo tuone ni kwa namna gani tunatenga fedha kuwajumuisha watu wenye ulemavu kwenye sekta ya afya, kwenye sekta ya elimu, kwenye sekta ya michezo katika kila eneo pamoja na zile key performance indicators ili tuone kama Taifa tuko wapi na tunahitaji kwenda wapi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba, sisi kama Taifa, sisi kama Wabunge humu ndani kila mmoja ana haki na wajibu wa kuzungumzia watu wake, nami kwa niaba ya watu wenye ulemavu, ninaunga mkono hoja pamoja na mapendekezo hayo. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. YUMNA MMANGA OMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema ya uhai na uzima na kutujaalia sote tukiwa hapa leo tukiendelea na majukumu yetu ya kikatiba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na vijana wenzangu kwa kumshukuru na kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan sambamba na Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kuanzisha Wizara hizi ambazo zinagusa mahsusi maendeleo ya vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kupoteza muda, na mimi niende moja kwa moja katika hoja iliyopo Mezani. Wakati ninasoma hotuba hii ya Waziri, nimeona kwamba ameomba shilingi milioni 35 kwa ajili ya utekelezaji wake wa mwaka 2026/2027, lakini 83% ya fedha hizi zinakwenda kwenye uendeshaji ikiwemo mishahara na OC na 17% zinakwenda kwenye uwezeshaji wa vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ombi langu ni kwamba, kama Wabunge wenzangu waliotangulia kusema, fedha hizi shilingi bilioni 200 ambazo zimetolewa kwa maendeleo ya vijana zingeletwa kwenye Wizara hii zikaweza kuratibiwa vizuri. Kuzipeleka kwenye Wizara nyingine, inasababisha fragmentation ya activities, ujasiriamali na kupelekea kutokupimwa, ufanisi wa upimaji wa matokeo wa hizi fedha kuwa ni mdogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia inclusivity ya uwezeshaji inaweza kupungua kwa sababu tunatambua Wizara hizi za sekta ziko zaidi katika uzalishaji, siyo uwezeshaji wa vijana, na sisi vijana wa Kitanzania tunataka kuwezeshwa na siyo kuendeshwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo, niseme tu kwamba, moja ya malengo la Wizara hii ni kuongeza kuhamasisha vijana kushiriki kwenye nafasi za uongozi kuanzia ngazi za Taifa hadi kata. Hii ameanza kumdhihirisha Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kuanzia Baraza lake la Mawaziri, humu ndani ya Bunge, pamoja na maeneo mengine ndani ya Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yetu hii imezindua kamati ya utekelezaji wa kusimamia programu za uwezeshaji wa vijana ikiwemo Hub Challenge na Idea Kitaa. Kamati ile haina uwakilishi wa vijana wenye ulemavu. Hatulilii uwakilishi, tunalilia meaningful participation, kwa sababu ni sisi ndio tunatambua pilipili inatuwasha kwa namna gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni sisi ndio tunatambua kiatu kinatubana kwa namna gani? Ni sisi tunatambua changamoto zetu na namna gani ya kwenda kuzitatua. Kwa maana hiyo, basi hata ile fomu ya maombi ya kwenye programu hii, inapokosa kipengele cha ulemavu, ni kipengele kidogo, lakini impact yake ni kubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia kukosekana kwa kipengele hiki, tunaweza kukosa takwimu sahihi ni vijana wangapi wenye ulemavu wamefikiwa na taarifa ya fursa hii? Ni vijana wangapi wenye ulemavu ambao wameomba fursa hii? Ni vijana wangapi wenye ulemavu wamepatiwa fursa hii? ni vijana wenye ulemavu wa aina gani wamepata fursa hii? Vivyo hivyo, kutokana na ukosefu wa takwimu hizi tunashindwa kupima matokeo halisi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye ulimwengu wa sasa ambao ni data driven decision making, ukitutoa kwenye nafasi ya maamuzi, maana yake umekusudia kwa madhumuni mazima kutoa kwenye matokeo. Hivyo basi, ninaiomba Wizara ikaangalie namna inavyokwenda kutushirikisha sisi vijana wenye ulemavu kwenye nafasi hizi, na pia nafasi ya kurekebisha ile fomu kwa matokeo mazuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Wizara imeanzisha makongamano mbalimbali ambayo yanakutanisha vijana sehemu mbalimbali kujadili fursa na changamoto. Makongamano haya ni kwa namna gani yanajumuisha vijana wenye ulemavu in terms of miundombinu na kufikiwa na taarifa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafanya makongamano mijini na vijijini, ni lazima tuhakikishe tunaweka mazingira ya kwenye kivuli, yaani miundombinu rafiki ili vijana wenye ulemavu wa viungo waweze kufika, na pia wakalimani wa lugha ya alama ili ndugu zetu wenye ulemavu wa uziwi waweze kupata taarifa na kunufaika na fursa hizi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni mapendekezo yangu kwa Wizara kuona ni namna gani wanaweka jitihada za makusudi za kuweza kuhakikisha kuwa nasi vijana wenye ulemavu tunatufaika kwa 100% kwenye fursa hizi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaweza tukaweka specific intervention. Kama ni mashindano, tunaweka mahususi kwa vijana wenye ulemavu; na yapo yanaendelea. Tarehe 7 Machi, nimehudhuria Programu ya Wazo Bora, Pitch Programme, ambayo vijana wenye ulemavu wameshindanishwa mawazo yao, ideas zao za ubunifu na washindi watatu walipewa zawadi. Shindano hili lilianzishwa na Standard Chartered Bank wakishirikiana na Side Saver Organization. Taasisi hizi zipo, na sisi kama Serikali tuna nafasi kubwa ya kutekeleza haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninawasilisha hoja na ninakubaliana nayo. (Makofi)