Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. KHALID M. NSEKELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa nafasi hii ya kuchangia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai na afya ya kuweza kuwa hapa leo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachukua nafasi hii kukushukuru wewe hapo na ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ambayo ameifanya, hasa ya kuzunguka ndani ya Nchi ya Tanzania, mikoa mbalimbali na kutatua kero. Nichukue nafasi hii, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Kyerwa, Mkoa wa Kagera kumwomba kwamba, angalau tunashukuru kama tutawekwa kwenye ratiba atutembele Mkoa wa Kagera na Jimbo la Kyerwa na sisi tuna kero nyingi sana, tunapenda tumwambie uso kwa uso. Hili ninamshukuru Mheshimiwa Rais, ninakumbuka wakati anafungua Bunge hili alielekeza kwamba, uongozi wake utajikita sana kwenda kuwasikiliza Watanzania na kutatua kero zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nichangie kidogo kwenye hotuba hii nzuri kabisa ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Ninachangia maeneo matatu, eneo la kwanza ninaomba nichangie kwenye suala la barabara, miundombinu ya barabara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatokea Jimbo la Kyerwa, sisi ni wakulima wa zao la kahawa, zao kubwa kabisa, zao la kimkakati. Sisi tuna athari kubwa sana kutokuwa na barabara nzuri, hasa barabara ya lami, barabara za vijijini. Kutokuwa na barabara za vijijini ni tatizo kwa sababu, tunatambua kwamba, barabara siyo tu kwa ajili ya kusafirisha mazao na watu, lakini ni uti wa mgongo wa huduma za jamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia suala la afya, Mheshimiwa Rais ameleta vituo vya afya vya kutosha. Tunavyo vituo vya afya vitano katika Jimbo la Kyerwa, lakini kitendo cha kutokuwa na barabara imara inakuwa ni changamoto kwa mwananchi kutoka nyumbani kwake kwenda kupata huduma kituo cha afya kwa sababu, hawezi kupita ile barabara na hasa katika hali hii ya mvua, unakuta kuna sehemu huwezi kuvuka. Mvua ikianza lazima wananchi wakae hapo mpaka iishe ndiyo waweze kuvuka. Barabara kama sehemu za Munchwekano kule, ukienda Kihea, ukienda Rwabwere, vijiji ni vingi sana ukisema uvitaje huwezi kupata muda wa kutosha, lakini barabara zile ni mbovu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda vilevile kwenye suala la kilimo. tunajua wakulima, ili waweze kupata tija ni lazima waweze kupeleka mazao yao sokoni. Kitendo cha kutokuwa na barabara imara, mkulima anapata changamoto na sana sana, tunakuja kupata tatizo la post harvest loss, mazao mengi sana hayafiki sehemu za masoko. Barabara ni muhimu sana na katika suala la uchumi wa Tanzania nzima, tumeona nchi nyingi sana zimetoka hatua moja kwenda hatua nyingine baada ya kuwa na miundombinu imara ya barabara, tunatambua hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la maji. Tunatumia gharama nyingi sana kupeleka mitambo, sijui wataalam kwenda kutengeneza miradi ya maji, lakini kitendo cha kutokuwa na barabara ni shida kubwa sana, hasa katika Jimbo la Kyerwa ambalo jiografia yake kidogo imekaa vibaya, milima na mabonde. Kutokuwa na barabara unakuta ni changamoto sana kupeleka miradi sehemu ambayo inatakiwa kwa sababu, wataalam wa mradi huo hawawezi kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kuhudumia ile miradi vilevile inakuwa ni ngumu pale tunapokuwa na changamoto ya hiyo miradi. Kwa hiyo, rai yangu ni kwamba, tunaomba TARURA iongezewe nguvu ya kuweza kuhudumia hizi barabara, tunatambua umuhimu wake, tunatambua umuhimu katika uchumi na katika kutoa huduma. Tukiwa na barabara imara hatutatumia gharama nyingi kupeleka zile huduma pale zinapotakiwa. Ninatoa rai kwamba, ni muda sasa hizi halmashauri ziongezewe nguvu na kujengewa uwezo wa kuhudumia hizi barabara za TARURA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni sehemu ya vijana. Tunatambua tuna zaidi ya 60% ya vijana katika nchi hii. Hii ni asset kubwa sana kwa Nchi ya Tanzania, hasa tunapojiandaa kwenda katika Dira yetu ya 2050. Tukiwekeza vizuri katika hawa vijana, tukawapa ujuzi na tukawatengeneza, tunaamini kabisa kwamba, sisi tutafika vizuri katika hiyo dira yetu na hapa namshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa jitihada na initiative ambazo amezifanya katika kumkomboa na kumnyanyua kijana wa Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona ameanzisha Wizara ipo chini yake, lakini bado ametoa shilingi bilioni 200 ambazo nyingi zinaenda kwenye sekta ya vijana. Hii ni dhahiri kwamba, Mheshimiwa Rais ana maslahi mapana ya vijana wa Tanzania. Mimi hapa, kama kijana, ninaomba nitoe rai kwamba, hizi hela zinakwenda kwa vijana ambao tayari wameanza kuwa na biashara ndogondogo kuwawezesha kuwa na mtaji mdogo, lakini wapo vijana wengi sana mtaani ambao hawana uwezo wa kuanza biashara hata ndogondogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu ni kwamba ni muda sasa hizi halmashauri ambazo ziko mikoani na halmashauri zote nchi nzima ziwe na kitengo ambacho kitawaruhusu vijana waje pale watoe mawazo yao yanayohusu TEHAMA, kilimo na biashara. Halafu sasa Serikali ione ni jinsi gani ya kuwezesha yale mawazo ili kuwanyanyua, kwa sababu tunajua wapo vijana wengi, tukiwawekea chumba maalum bila hata kuwalipa na kuwaambia vijana njooni hapa, toeni mawazo yenu ya TEHAMA, kilimo, biashara, chochote wewe elezea, wazo lako likoje wataeleza. Tukae pamoja, tuwape na mwalimu au mentorship wa kuwaongoza vizuri, tutapata mawazo mazuri, tutaweza kuanzisha vijana ambao tayari watakuwa kwenye biashara na kuendelea juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu, ninaomba nichangie kwenye suala la dira kulingana na hii hoja au hotuba ya Waziri Mkuu. Hii ni bajeti ya kwanza kuelekea Dira ya 2050 na ninamshukuru sana Waziri Mkuu ameelezea vizuri uelekeo wa Dira hii ya 2050, lakini hoja yangu ni jinsi gani mipango yetu inaakisi hii Dira ya 2050? Je, sekta zetu zote zinajielekezaje kumfikisha Mtanzania wa leo kwenye 2050? Kwa sababu tunapokaa hapa Bungeni ninaona kabisa Mawaziri wetu, ukimwona Waziri Profesa Shemdoe na timu yake wapo kwenye field wanahakikisha tupate matokeo lakini nani yuko ofisini kwa ajili ya kuandaa TAMISEMI ya 2050?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukimwona Mheshimiwa Waziri Aweso anashughulika na maji ameenda China, amekuja wapi, lakini nani kabaki ofisini kuhakikisha kwamba Wizara ya Maji ya 2050 itakuwa hivi? Kwa hiyo, rai yangu hapa ni kwamba kuna haja sasa rasmi tuwe na kitengo maalum kwenye kila Wizara, kila Taasisi cha ubunifu na mabadiliko makubwa ya kuziandaa sekta zote za Tanzania kwa ajili ya 2050, maana yake ninasema future ready economy au future ready government.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tuwe na vitengo ambavyo vinakaa ofisini kwamba wakati hawa wako field wanafanya kazi hii, lakini hatoki kwenye mstari, tunataka sekta ya afya iwe hivi kwa 2050, sekta ya ujenzi, sekta ya maji, tuwe nazo tayari na mwelekeo mzuri ambao unatuongoza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili ninaomba tunapokuwa tunafanya kazi au Wizara zetu tunaambiwa Waziri Mkuu aje na ajenda ya kuchangamana au ku-incorporate hizi Wizara zishirikiane kwa sababu, kwa sasa unavyoweza kuangalia kila Wizara inafanya kazi pekee yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aliwahi kuongea Mheshimiwa Musukuma pale, alitoa mfano mdogo akasema Barabara ya kutoka Airport kuja Posta - Dar es Salaam ina kona nyingi sana ambazo hazina umuhimu wa kuwa nazo. Lakini ukiangalia ni kwamba Wizara ya Ujenzi haina mahusiano na Wizara ya Utalii. Sisi tunavyotoka kwenda Dubai tunashangaa Barabara za Sheikh Zaid Road ni barabara tu. Kwa hiyo, barabara hii nayo ni utalii siyo mpaka uende msituni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Wizara ya Kilimo au tubaki hapa kwenye Wizara ya Ujenzi, Wizara ya Ujenzi lazima ishirikiane na Wizara ya Nishati, siyo unajenga halafu ndiyo anakuja kuvunja anapitisha nguzo. Wizara ya Maji barabara imejengwa huyu anakuja kuvunja apitishe bomba. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kabisa mfano tu Wizara ya Kilimo, lazima ikae na Wizara ya Elimu, haiwezekani muda huu hatuna graduate anaweza akasema au wanatoka graduate saa hizi wanakuja, hana elimu inayohusu madini. Wapo graduate hawana elimu kuhusu kilimo, wapo hawana elimu kuhusu utalii. Hii maana yake hatushirikiani Wizara ya Kilimo na Wizara ya Elimu kuona kwamba tunatoa graduates gani kwa ajili ya kuiandaa Tanzania. Uchumi wetu wote uko kwenye kilimo, upo kwenye utalii, upo kwenye madini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni hayo ninashukuru sana na ninaunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. KHALID M. NSEKELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa nafasi hii niweze kuchangia hoja ambayo iko Mezani. Kwanza nimshukuru Mheshimiwa Rais na kumpongeza kwa kazi kubwa na juhudi za makusudi za kumtua ndoo mama kichwani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, nitoe pongezi kubwa sana kwa Mheshimiwa Waziri na timu nzima ya Wizara ya Maji kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya, lakini kwa wasilisho zuri sana la bajeti ambayo siyo tu kwamba inaonesha namba kwenye jedwali, lakini ni bajeti ambayo inaakisi maono ya Mheshimiwa Rais na Dira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemsikiliza vizuri na kuisoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Ukiangalia hii bajeti ya Wizara ya Maji ni bajeti ambayo inamgusa kabisa mwanamama ambaye anatembea kilometa zaidi ya tano kufuata maji saa 11 asubuhi. Pia ni bajeti ambayo inamhusu kabisa mwanafunzi ambaye anakosa masomo akiwa kwenye harakati za kwenda kuchota maji. Vilevile, ni bajeti ambayo inamhusu mkulima na mfugaji ambaye anategemea majisafi na salama na wingi wa maji katika uzalishaji wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti ukiangalia takwimu za Tanzania kutoka World Bank, ni kwamba tume-improve sana katika suala la kupata majisafi na salama. Ni 30% mpaka 40% ya wananchi wana majisafi na salama, 70% mpaka 85% wana maji ya msingi, lakini kwenye takwimu hizi kwa mimi ambaye ninatokea Kyerwa, bado ninakuwa na ugomvi nazo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru kwa kazi kubwa inayofanyika. Kuna miradi ambayo inagusa vijiji 21 na nimeona kwenye bajeti fedha zimetengwa, ambazo zitaenda kukamilisha miradi hii. Ukiangalia idadi kubwa ya Vijiji vya Kyerwa bado tunategemea maji ya visima, maji ya chemchem na maji ya mvua ambayo hayana uhakika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi ninaomba nitoe rai kwamba, bajeti tumeiona, lakini tunaomba fedha hizi zitoke mapema. Nimwambie Mheshimiwa Waziri kwamba, mafanikio ambayo anataka ayaone, na nimeona jitihada zake zilivyo, ni mafanikio ambayo yatakuwa na maana pale yatakapokuwa yamemgusa mwananchi wa kawaida, hasa mwananchi wa kijijini, vikiwemo Vijiji vya Kyerwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili ninaomba nitoe rai kwamba, vile vyombo vya watumia maji vya vijijini vijengewe uwezo, vipewe nguvu na viwajibishwe katika kukusanya mapato na kusimamia miradi. Hapa ninaomba kidogo Mheshimiwa Waziri aniazime masikio yake kwa sababu, kuna siku niliuliza swali la Mradiwa Kigorogoro, Rulamana Kashandana Mheshimiwa Naibu Waziri akanipa majibu kidogo, ambayo sikuridhika nayo, lakini nikaona nifanye kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetembelea mradi ambao uko Kigorogoro, Kata ya Kibale, ule mradi umejengwa 2009. Ule mradi uko kilometa tano kutoka makazi ya watu, uko msituni, lakini tenki la maji limejengwa kilometa 12 kutoka kisima kilipochimbwa. Sasa unaweza ukaona kwamba, tayari usalama wa mradi ni shida kwa sababu, uko msituni, lakini una gharama kubwa ambayo inatumika ku-pump maji kilometa 12 kutoka kwenye kisima kuja kwenye tenki la maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kibale, Kigorogoro, Rulama na Kashanda wameji-commit. Nimeongea nao wanasema wao hawakushiriki kuharibu mradi, kama ilivyojulikana toka mwanzo, na mimi kwa niaba yao ninaomba, sasa wameahidi kwamba, wako tayari, wanaomba Serikali sikivu ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan iwapelekee mradi wa maji kwa sababu, miaka mingi hawana majisafi wala hata maji ya msingi hakuna. Kwa hiyo, wanaomba, na wako tayari kutoa ushirikiano wa kutosha wakipata kisima cha maji pale kwenye Kata ya Kibale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ninaomba nitoe rai kwamba, ni muda mwafaka sasa, wakati Wizara ya Maji inafanya kazi kubwa kusambaza majisafi na salama kwa wananchi, na kuna haja ya ushirikiano mkubwa sana na Wizara ya Nishati, nikimaanisha TANESCO, kwamba, wasambaze umeme pale pote kwenye miradi ambapo inapelekwa kwa sababu, ukienda Jimbo la Kyerwa, miradi mingi ipo sehemu, hakuna umeme.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali inaingia gharama kubwa sana kwenda kuvuta yale maji kwa kutumia sola. Kama hakuna mvua, maji hakuna, kwa sababu, changamoto nyingi ambazo zinatokea kwenye shida ya maji ni uhakika wa maji. Miradi ipo, lakini uhakika hamna, umeme hamna, sola ina shida, mvua imenyesha, watu hawana huduma ya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mwisho kabisa, kuna Mradi wa Kuvuta Maji kutoka Mto Kagera ambao unakwenda kugusa Kata ya Nyaruzumbura, Kyerwa, Nyakatuntu, Businde, Bugarana Kamuli, ambao utahudumia vijiji 21. Ninamwomba Mheshimiwa Waziri, hili suala la wanakijiji wa Kyerwa au Kyerwa kwa ujumla watashukuru watakapoona kuna jitihada za msingi zinafanyika ili mradi huu uweze kukamilika. Ninashukuru sana.