Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Twaha Said Mwakioja

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Primary Question

MHE. TWAHA S. MWAKIOJA aliuliza:- Je, ni lini Tembo wanaojeruhi na kuharibu mali majumbani na mashambani maeneo ya Mwakijembe, Bwiti, Daluni na Duga watadhibitiwa?

Supplementary Question 1

MHE. TWAHA S. MWAIKOJA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali ningependa kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; Taasisi zetu za Serikali za TANAPA, NCAA na TAWA zinabaki na mapato ili kuweza kutoa huduma mbalimbali. Pamoja na kubaki na mapato (retention) bado tumekuwa na changamoto ya kuwapa waathirika hawa wanaokumbana na majanga haya ya wanyamapori kifuta jasho ambacho ni kidogo na kiwango hiki ni cha muda mrefu sana. Je, Serikali haioni haja sasa ya kufanya mapitio juu ya viwango hivi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; utaratibu wa kufanya uthamini kwa wananchi wanaopata majanga umekuwa na urasimu mkubwa sana na kusababisha baadhi ya wananchi kushindwa kufuatilia na kuendelea kuilalamikia Serikali yetu. Je, Serikali haioni haja sasa ya kufanya mapitio juu ya mchakato huu ili uwe rahisi na kuwaletea tabasamu wananchi wetu na hususan wananchi wa Jimbo la Mkinga? Ahsante.

Name

Hamad Hassan Chande

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kojani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kabla ya kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Twaha Mbunge wa Mkinga, ninaomba nimpongeze sana pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuaminiwa na wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali ilishafanya marekebisho ya Kanuni ya Mwaka 2011, kanuni hiyo ilionekana ni kweli kifuta jasho ni kidogo imefanyiwa marekebisho mwaka 2024 kwa Tangazo la Serikali Na. 440, mwaka 2024, tarehe 31 Mei na imefanya marekebisho makubwa. Kwa sasa waathirika wale ambao watakuwa na ulemavu wa muda mfupi yaani majeraha ya muda mfupi watalipwa 50%, vifo vya mifugo 50%, uharibifu wa mazao 50%. Pia lipo ongezeko kubwa la vifo na ulemavu wa kudumu kwa 100%.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, Serikali tayari imeliona hilo suala la urasimu na kwa sasa tunatumia mfumo maalum unaotambulika kwa jina la PAIS yaani Problem Animal Management Information System ambao sasa urasimu hautopatikana, maana yake inarekodi moja kwa moja na kuhakiki taarifa zile na kupelekwa kwenye kanzidata. Nina imani kabisa kwamba urasimu huo sasa utakuwa umepata mwarobaini wake. Ahsante sana.

Name

Ado Shaibu Ado

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Tunduru Kaskazini

Primary Question

MHE. TWAHA S. MWAKIOJA aliuliza:- Je, ni lini Tembo wanaojeruhi na kuharibu mali majumbani na mashambani maeneo ya Mwakijembe, Bwiti, Daluni na Duga watadhibitiwa?

Supplementary Question 2

MHE. ADO S. ADO: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kuniona. Kwa vile tatizo hili la tembo kuvamia vijiji na kuharibu mazao, kuuwa binadamu ni tatizo kubwa sana katika Jimbo la Tunduru Kaskazini na Wilaya ya Tunduru kwa ujumla wake. Ambapo kwa msimu wa kilimo wa 2025/2026 peke yake jumla ya waathirika 1791 wameharibiwa mazao yao na askari wa vijiji mpaka sasa wako 23 tu. Je, ni lini Serikali italipa fidia kwa waathirika wote na kuongeza idadi ya askari wanyamapori wa vijiji (VGS)?

Name

Hamad Hassan Chande

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kojani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tayari Serikali imeshaweka fedha na zimeshaingia na sasa tunafanya utaratibu wa kulipa kupitia mfumo. Kilichochelewesha ilikuwa tunalipa manual, unaenda kijijini unaenda kulipa, pengine unaenda kulipa milioni tano unatumia gharama ya milioni nne, lakini kwa sasa tunatumia mfumo na mfumo huu umetuwezesha. Nimwombe tu Mheshimiwa Mbunge awe na subira hawa watu wetu watapata malipo yao.