Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Name
Neema Peter Majule
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Primary Question
MHE. DKT. NEEMA P. MAJULE aliuliza:- Je, Serikali imechukua hatua gani kudhibiti mikopo hatarishi yenye riba kubwa inayotolewa na baadhi ya Taasisi zisizo rasmi?
Supplementary Question 1
MHE. DKT. NEEMA P. MAJULE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri yaliyotolewa na Naibu Waziri kijana kabisa. Nina maswali ya nyongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; kwa kutambua umuhimu wa sekta ya fedha, Serikali imeandaa au kusimamia miongozo ipi ya kuhakikisha wananchi hususan wanawake na vijana wanapata elimu ya fedha ili kuchochea jitihada za ukuaji wa kiuchumi? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili; Serikali imechukua gani sasa kwa hao watu ambao wamejinufaisha sana kwa mikopo hii yenye riba kubwa? Waingereza wanasema Predatory Loans, lakini sisi tumeitafsiri kama ‘Mikopo ya Kausha Damu’. Kwa maana kwa namna walivyofanya wameweza kabisa wenyewe kujinufaisha na kupunguza kabisa jitihada ya Serikali ya kuwakwamua wananchi kiuchumi hususan wanawake na vijana. (Makofi)
Name
Laurent Deogratius Luswetula
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Kavuu
Answer
NAIBU WAZIRI WA FEDHA (MHE. LAURENT D. LUSWETULA): Mheshimiwa Spika, ahsante sana Mheshimiwa Dkt. Neema Peter. Kwanza ninakushukuru kwa maswali mawili ya nyongeza, maswali mazuri, lakini hii inamaanisha kwamba wanawake wa Dodoma hawakukosea kukuchagua. Kweli Ph.D kichwani ipo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, baada ya hayo sasa, niseme tu kwamba, Serikali imeendelea kuandaa na kusimamia miongozo na utekelezaji wa sekta ya fedha ili kuchochea uchumi wa wananchi, hasa vijana pamoja na wanawake. Serikali imekuja na mkakati maalum ambao unaitwa Programu ya Elimu ya fedha ya mwaka 2020/2021 – 2025/2026, ikiwa ni mpango maalum wa kutoa elimu kwa wananchi (wanawake wanaume na makundi mengine) ambayo inalenga zaidi kuwawezesha Watanzania kupata uelewa, maarifa na kuwajengea kujiamini katika kusimamia mapato na matumizi na kufanya maamuzi sahihi katika kutumia huduma rasmi za kifedha.
Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, ninyi mnaweza mkawa ni mashahidi ya kwamba kama Wizara ya Fedha tumekuwa kila mwaka tukiadhimisha maadhimisho ya Huduma ya Wiki ya Kifedha; ambapo tumeanza mwaka 2021 – 2026 (ambapo yamefanyika rasmi tarehe 21 mwezi huu, 2026). Mimi binafsi nikimwakilisha Waziri wa Fedha nimeenda kufungua rasmi maadhimisho hayo ambayo yamefanyikia nchini (Tanga) ili wananchi waweze kupata elimu ya kifedha. Kweli wananchi wa Tanga waliyapokea kwa hali ya juu, walikuwa ni wengi. Hii ni mikakati maalum ya Wizara ya Fedha kuhakikisha ya kwamba wananchi wanapata elimu ya fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, maadhimisho haya yameanza muda kidogo, tangu mwaka 2021. Mikoa ya Dar es Salaam, Mwanza, Arusha na mikoa mingine imeendelea kunufaika na elimu hii.
Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, zaidi ya mikoa 16 mpaka sasa hivi tumeweza kufikisha huduma hiyo ya fedha, kuwapa elimu ambapo zaidi ya wananchi 64,000 ikiwemo wanawake 40,000 na wanaume 24,000 wamepata elimu hii kuhusu elimu ya fedha. Vilevile, zaidi ya halmashauri 94 nazo tumepita kuhakikisha kwamba wanapata elimu ya fedha ili waweze kufanya maamuzi sahihi katika uwekezaji wao, katika uwekezaji na kuingia sasa kuwekeza kwenye mambo yetu ya kifedha ikiwemo uwekaji akiba, mikopo, uwekezaji, bima, Bima-amana, kodi, hati fungani na mengineyo mengi, kwa sababu sisi kama Wizara ya Fedha tumejipanga ipasavyo. (Makofi)
SPIKA: Ahsante!
NAIBU WAZIRI WA FEDHA (MHE. LAURENT D. LUSWETULA): Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili, lililenga zaidi kwamba sasa sisi kama Wizara ya Fedha tumejipanga kwa namna gani kuhakikisha kwamba wale wanaokiuka taratibu zilizowekwa sasa wanaweka riba kubwa ili kujinufaisha wao.
Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba, katika mkakati ambao tumesema kwamba tumeandaa rasimu ya kusimamia mikopo ya kidijiti ambayo inatarajiwa kuanza mwaka 2026 na 2027, sisi kama Wizara ya Fedha tumejipanga kuhakikisha ya kwamba taasisi zote zinazotoa mikopo zinafuata taratibu zote. Yeyote anayekiuka tayari tumeshaanza msako huo kuhakikisha kwamba tunasitisha leseni na kufunga kabisa, kwa sababu anakiuka taratibu ambazo Serikali imeziweka. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa nyongeza tu kwa niaba ya Waziri wa Fedha, tunaiagiza Benki Kuu ya Tanzania kuendelea kuongeza juhudi zaidi katika udhibiti wa mikopo hii, kuhakikisha kwamba wananchi hawa ambao sasa wanatuamini na Serikali yetu hii ya Awamu ya Sita wanapata mikopo ambayo sasa inawanufaisha na wala si ile wanayoiita ‘Kausha Damu’ na sisi tumejipanga kuhakikisha kwamba tuko pamoja kuwasaidia wananchi kwa sababu ndiyo wananchi wetu. Ahsante sana. (Makofi)
Copyright © Bunge Polis 2026. All Rights Reserved