Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Name
Patali Shida Patali
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Mbeya Vijijini
Primary Question
MHE. PATALI S. PATALI aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga soko la uhakika la mazao Mbeya Vijijini?
Supplementary Question 1
MHE. PATALI S. PATALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Ninaiomba sana Serikali kuharakisha mchakato huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, 85% ya wananchi wa Jimbo la Mbeya Vijijini ni wakulima na wafugaji. Mathalani kwa mwaka huu unaoisha, umezalisha zaidi ya tani 700,000 za mazao ya chakula. Wakati huo mahitaji yetu ni tani laki 200,000...
MWENYEKITI: Mheshimiwa, ninaomba uulize swali.
MHE. PATALI S. PATALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la msingi ni kuiomba Serikali kuharakisha ujenzi wa hilo soko, lakini pamoja na kiwanda kilichoahidiwa kwa ajili ya uchakataji wa nyama ili wananchi wa Jimbo la Mbeya Vijijini wapate soko, sehemu ya kwenda kuuzia mifugo yao kama mbuzi na ng'ombe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili. Ninatambua hivi karibuni Mheshimiwa Waziri Mkuu kupitia hotuba yake alikemea vikali uuzaji wa mazao uliozidi kiwango, almaarufu kwa jina la lumbesa. Je, Serikali haioni haja sasa ya kuleta Muswada hapa Bungeni ili tupitishe sheria ya udhibiti wa kudumu suala hili la lumbesa ambalo limekuwa likisababisha maumivu makali sana kwa wakulima?
Name
Dr. Festo John Dugange
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Wanging'ombe
Answer
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Mbeya Vijijini pamoja na wananchi wa Mbeya Vijijini kwamba Serikali inatambua kwamba zaidi ya 85% ya wananchi wa Mbeya Vijijini ni wakulima na wafugaji, na ndiyo maana tayari tumeshaandaa eneo kwa ajili ya kujenga kiwanda cha kisasa cha nyama. Eneo hili limeshakabidhiwa kwa TISEZA kwa ajili ya kufanya utaratibu wa kupata mwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili lipo, linaendelea na utaratibu wa kufanyiwa kazi na Serikali. Mara utaratibu utakapokamilika, tutapata mwekezaji ambaye atajenga kiwanda hicho ili kuboresha huduma za nyama katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, eneo la mazao ya nafaka pia limetengwa kwa ajili ya utekelezaji huo na tutakwenda kutekeleza. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba dhamira ya Serikali ni kuhakikisha tunakuwa na masoko mazuri kwa ajili ya bidhaa za mifugo na mazao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kuhusiana na lumbesa, ni kweli kumekuwa na changamoto kubwa ya lumbesa na inaleta hasara kwa wakulima. Wizara ya Viwanda na Biashara na Serikali kwa ujumla imeendelea mara kwa mara kutoa miongozo, maelekezo na kusimamia ili kudhibiti lumbesa kwa wakulima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepokea wazo lake la kuwa na Mswada wa Sheria na sisi kama Serikali tutalifanyia kazi kuona uwezekano wake. Lengo ni kuhakikisha kwamba tunadhibiti lumbesa na kuleta faida kwa wakulima.
Copyright © Bunge Polis 2026. All Rights Reserved