MHE. NASSORO RASHID NASSORO aliuliza: -
Je, lini Serikali itaweka kituo kidogo cha uhamiaji katika eneo la Makangale linalokua kwa kasi kiutalii kwa ajili ya ukaguzi wa wageni?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nassoro Rashid Nassoro, Mbunge wa Konde, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya utoaji wa huduma za kiuhamiaji katika maeneo yote ya kimkakati yenye utalii ikiwemo Unguja na Pemba.
Mheshimiwa Spika, Serikali imekamilisha ujenzi wa Ofisi ya kisasa ya Uhamiaji katika Wilaya ya Micheweni Pemba, ambayo inatoa huduma katika Shehia 25 ikiwemo Shehia ya Makangale. Aidha, katika vipaumbele vya bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 Serikali ina mpango wa kununua kiwanja katika eneo la Makangale kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Uhamiaji.
Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.