Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Paschal Inyasi Chinyele (2 total)

Hotuba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Ufunguzi Rasmi wa Bunge la Kumi na Tatu, Tarehe 14 Novemba, 2025
MHE. PASCHAL I. CHINYELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza kabisa ninaomba kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema na mimi binafsi ninashukuru kwa mara ya kwanza kusimama katika Bunge hili kutoa hoja. Pia, ninamshukuru Mwenyezi Mungu, watu wa Dodoma tumepata mvua nzuri tunamshukuru sana Mwenyezi Mungu. Ninamshukuru vile vile Mheshimiwa Rais kwa kunikubali mimi kugombea katika Jimbo la Dodoma Mjini, ninashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawashukuru pia wakazi wa Jimbo la Dodoma Mjini kwa kuniamini na kunichagua kwa kura nyingi mimi pamoja na Mheshimiwa Rais na Madiwani. Wamekiheshimisha sana Chama Cha Mapinduzi na mimi binafsi ninaahidi kutumia nguvu zangu zote kuhakikisha kwamba matarajio yao yanafikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kufanya mambo mengi katika Jimbo la Dodoma Mjini, lakini kwa haraka haraka tu niseme, tumejengewa SGR, sasa hivi watu wa Dodoma tunapata usafiri kwa urahisi zaidi kwenda Morogoro na Dar es Salaam, hospitali pamoja na vituo vya afya kadhaa vimejengwa, miradi ya maji na umeme, barabara hii ya mzunguko pia tumejengewa kiwanda kikubwa cha mbolea katika eneo la Nala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo ni baadhi, yapo mengi kwa sababu ya muda nitajikita katika maeneo matatu na niseme tu ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa hotuba nzuri iliyosheheni matumaini makubwa wa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo na mimi ningependa nijadili ni suala la uchukuzi ambalo katika hotuba ya Mheshimiwa Rais ameliweka suala hili vizuri katika ukurasa wa 32 na ninaomba nisome kwa jinsi lilivyowekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais ameeleza kuhusiana na kufungamanisha sekta za uchukuzi, sekta hizi zinapofungamanishwa zinaleta tija kubwa sana kwa uchumi wa nchi. Ninaomba niseme tu, katika Jimbo la Dodoma Mjini tumepata bahati ya kupitiwa na barabara ya mzunguko (ring road), katika eneo la Zuzu barabara hii inakutana na SGR, reli ya mwendokasi. Hata hivyo, katika kituo hiki hakuna kituo cha SGR ni ombi la wakazi wa Dodoma Mjini kwamba eneo hili la Zuzu lipate stesheni ya SGR kwa kuwa tayari kuna access road ambayo ni ring road.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vituo kadhaa ambavyo SGR inapita kwenda Dar es Salaam, maeneo ya Soga na Gulwe, Serikali ya Dkt. Samia inajitahidi sana kujenga access roads lakini hapa Zuzu tayari ipo access road ambayo inakwenda katika maeneo mbalimbali, hii barabara inashika maeneo ya Nala, Mbalawala, Bihawana, Matumbulu mpaka Mpunguzi, kote huko inafika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jirani kabisa na hiki kituo ambacho tunapenda kijengwe cha Zuzu kuna kongani ya viwanda inatarajiwa kujengwa katika eneo la Zuzu, ambapo ni maombi ya wananchi kwamba litoke tawi la reli ya SGR kutoka hapa Zuzu kuelekea Nala ili mizigo itakayokuwa inakwenda kwa ajili ya ujenzi wa viwanda hivi ipite kwenye reli badala ya kupita kwenye barabara zetu ambazo zinajengwa kwa gharama sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande mwingine ambao ningependa nichangie ni sekta ya ujenzi ambayo katika ukurasa wa 28 imewekwa vizuri na ninaomba ninukuu. Mheshimiwa Rais amesema hivi; “eneo lingine tutakalolipa uzito mkubwa ni sekta ya ujenzi. Kipaumbele kitakuwa ni kukamilisha miradi mbalimbali ya ujenzi wa barabara ambazo tayari zimeanza na zinaendelea. Tutaendelea na kasi ya utekelezaji wa miradi ya barabara pia TANROADS ili kufikia lengo la kuunganisha barabara za Makao Makuu ya Wilaya na Mikoa.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa sana ya kujenga barabara za nchi hii, ningependa nitoe wito kwa vijana wetu katika nchi hii na niseme tu kwamba nchi hii imetoka mbali sana katika sekta ya barabara. Miaka ya kabla ya 2000 wakazi wa Dar es Salaam na maeneo mengine kama Morogoro na Dodoma walikuwa wanakwenda katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa kwa kutumia treni peke yake. Hakukuwa na usafiri mwingine zaidi ya treni, ilikuwa inachukua hata siku tatu na hiyo ni katika hali ya kawaida, lakini ikitokea reli imekwama katika maeneo ya Kidete kwa mfano, ambapo kila mara huwa kuna shida wakati wa mvua, basi abiria walikuwa wanaweza kukaa njiani hata kwa wiki nzima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefika mbali katika ujenzi wa barabara ambapo kwa sasa Mheshimiwa Rais amefanikiwa kujenga kilomita 11,900 hadi 12,197 za barabara nchi nzima. Tuko mbali katika barabara na suala hili Watanzania tunapaswa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa juhudi zake hizo. Nitatoa mfano mdogo wa hii Barabara ya Ring Road, barabara hii ni barabara ambayo ni ya mfano. Nilikuwa najaribu kupitia nchi mbalimbali kuona ni nchi zipi ambazo zina barabara zenye urefu kama huu, tunaambiwa kwamba barabara hii ya ring road ambayo ina kilomita 112 .3 ni barabara kubwa kuliko zote katika Nchi za Kusini na Mashariki mwa Afrika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeenda mbali zaidi nikaangalia Morocco pamoja na South Africa, lakini nimekuta wote wana barabara za ring road ambazo zina urefu mdogo. South Africa wana kilomita 83, Morocco wana kilomita 41 ni Misri peke yake ina kilometa 400 ambayo ndiyo inatuzidi, sisi ni wa pili tunayo barabara ambayo kwa kweli ni kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta wote wana barabara za ring road ambazo zina urefu mdogo. South Africa wana kilometa 83, Morocco wana kilometa 41; lakini ni Misri peke yake ina kilometa 400, ndiyo inayotuzidi. Sisi ndiyo wa pili na tuna barabara ambayo kwa kweli ni kubwa. Barabara hii ya ring road inasaidia sana ufikaji katika Jiji la Dodoma. Ninasema tu, ndugu zangu wanaotoka Iringa na wanakwenda labda mji wa Serikali, hawana haja tena ya kwenda mjini, wanafika Matumbulu wanaingia moja kwa moja Mji wa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu pia wanaotoka Mwanza, Shinyanga na kadhalika, wakifika maeneo ya Nala hawana haja tena ya kuja mjini, wanaingia kushoto, wanapita Veyula wanakwenda Mji wa Serikali wanakuwa wameshamaliza. Kwa hiyo barabara hii ni msaada mkubwa sana kwa sisi Watanzania hasa ndugu zangu tunapoingia katika Mkoa wa Dodoma, kwa hiyo barabara hii ni nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Muda wako umekwisha Mheshimiwa.

MHE. PASCHAL I. CHINYELE: …barabara katika mkoa wetu, tuna Barabara kutoka Mjini Dodoma kuelekea Mvumi. Barabara hii ni ya muhimu na wananchi wetu ambao wanapitiwa na hii barabara hawajalipwa fidia. Ninapendekeza walipwe fidia zao kwa sababu ni haki yako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho…

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa, muda wako umeisha.

MHE. PASCHAL I. CHINYELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. PASCHAL I. CHINYELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi hii. (Makofi)

Kwanza kabisa na mimi namshukuru sana Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema kwa kunijalia uhai, lakini pia sisi Wana-Dodoma tunamshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa hali nzuri ya hewa mwaka huu, kwa kweli chakula tunacho, mahindi tunayo, uwele tunao, tumeshiba mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru pia Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa miradi hii ya maji, limetajwa Bwawa la Kidunda, napajua pale Kidunda na Dar es Salaam nimekaa najua shida wanayoipata wakati wa kiangazi. Kwa hiyo Mradi huu wa Kidunda, Mheshimiwa Rais amewatendea haki sana Watanzania. Nasema tu, hizi hatua za Mheshimiwa Rais siyo za bure, hizi hatua za Mheshimiwa Rais zina mkono wa Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kusema, kwa ndugu zangu Wabunge ambao mlipata bahati ya kuwepo wakati Mheshimiwa Rais anaapishwa pale Dodoma, kwa aliyekuwepo kama kuna kitu alikiona, yangeyange wale ndege weupe wakati anajiandaa kuapa Mheshimiwa Rais, wale ndege walisimama juu na waliondoka baada ya Mheshimiwa Rais kumaliza kuapa. Kwa hiyo, hatua za Mheshimiwa Rais zina mkono wa Mungu wa moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mimi namshukuru sana Mheshimiwa Aweso na Naibu Waziri wake kwa wasilisho zuri ambalo lina matumaini makubwa sana kwa Watanzania lakini pia na wakazi wa Dodoma Mjini kwa namna ya pekee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nafarijika sana, Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia na kuweka msisitizo kwa upatikanaji wa maji katika Jiji la Dodoma na hii si bahati mbaya. Hawa Wabunge waliopo walio wengi ni wakazi wa hapa Dodoma na wengine ambao ni Wabunge wameingia karibuni, nina hakika ni wakazi watarajiwa wa Dodoma ndiyo maana wanasema sana kuhusiana na miradi hasa Mradi wa Nzuguni, Nala pamoja na Zuzu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa tunavyoongea, mradi mkubwa, tuseme mtambo mkubwa wa maji kwa Dodoma ni Mzakwe ambao unatupa lita milioni 88 kwa siku mpaka sasa. Lakini hii Miradi ya Nzuguni, Nala pamoja na Zuzu ikikamilika, pamoja na huu wa Mzakwe kwa pamoja, itazalisha kwa siku lita milioni 127, lakini mwaka jana mwezi wa Mei tarehe kama ya jana, Dodoma ilikuwa inahitaji lita za maji milioni 143 lakini kwa sasa mwaka mmoja baadaye, tunahitaji lita milioni 159.9.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii maana yake ni nini, maana yake ni kwamba ongezeko la watu katika Jiji la Dodoma ni kubwa kuliko maji yanavyopatikana. Kwa hiyo, naomba sana ndugu yangu Mheshimiwa Aweso, unajua kuna mradi huu wa Farkwa na nimefarijika sana kila wakati tukikutana unaniambia Mradi wa Farkwa unakaribia kusainiwa, mimi nashukuru sana. Pamoja na huu Mradi wa Ziwa Victoria, yote ni miradi ambayo kwa kweli sisi tunadhani itakuwa ni mkombozi kwetu. Kwa sababu kama nilivyosema, ongezeko la watu katika jiji letu ni kubwa mno. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na miradi hii miwili, naomba tu kushauri Mheshimiwa Waziri, pia sisi Dodoma tuna bahati kwamba maji yako jirani. Ukipiga chini meta 150 unapata maji, kuna vyanzo vingi navyo hivyo vitasaidia kwa sababu ongezeko la watu, lakini na pia nafahamu Serikali ina miradi mingi ya maji kwa hiyo fedha ni changamoto.

Sasa ili kwenda sambamba na hali hii, tunapendekeza vyanzo vingine vitafutwe, visima vya maji vya kutosha vichimbwe. Mheshimiwa Waziri, mimi Jimbo la Dodoma lina vijiji pia ingawa …. lakini lina vijiji ambavyo havina kabisa huduma ya maji ya RUWASA ama DUWASA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo miradi ya maji midogomidogo itakaposisitizwa, inaweza kutusaidia sana sisi watu wa Dodoma kuendelea kupata huduma nzuri ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Dodoma sisi vijana wetu walio wengi, ikishafikia mwezi wa tatu, wa nne mvua zinakuwa zimekoma, kwa hiyo, hawana cha kufanya. Tunaomba sana miradi hii ya maji, na ninaendelea kusisitiza mara kwa mara, yajengwe matanki katika maeneo ambayo vyanzo vya maji vipo. Sasa hivi kuna mipango ya kujenga matenki katika bvilima katika kata zetu mbalimbali, Kata za Mpunguzi, Matunguru na kadhalika. Yajengwe kwa kiasi kikubwa ili kuwasaidia vijana hawa kupata cha kufanya wakati wa kiangazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa mvua hawa vijana wanalima bustani, wanalima nyanya, wanalima vitunguu, wanalima hoho, lakini mvua zikishakata hawana cha kufanya tena, wanakuwa wanakaa mitaani wanakunywa na kufanya mambo mengine ambayo hayafai. Tafadhali Mheshimiwa Waziri tusaidie vijana wetu waweze kupata cha kufanya na hawa naongelea vijana wetu ambao kwa kweli hawakubahatika kusoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema pia kuhusiana na umuhimu wa kuwasaidia ndugu zangu wa Kata ya Mbalawala. Mheshimiwa Waziri nimekuwa nikiongea na wewe mara kwa mara kuhusiana na wasiwasi walionao ndugu zangu wa Mbalawala pamoja na sehemu ya Nala kwamba eneo wanaloishi wanaambiwa ni Bonde la Mto Wami-Ruvu na hawaruhusiwi kuendeleza kwa namna yoyote maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa naongea sana hili jambo kwa sababu kwa kweli inauma, ukienda wakazi wale wapatao 12,000 kila wakati wanakuuliza Mheshimiwa Mbunge vipi mbona sisi haturuhusiwi kupima maeneo yetu, haturuhusiwi kujenga, haturuhusiwi kuwekeza chochote, tunaambiwa ni bonde.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Mbalawala na Nala vilikuwa ni vijiji toka mwaka 1971, vilipimwa kihalali. Ninaomba Mheshimiwa Waziri tulishaongea, lakini naomba tutakapomaliza kipindi hiki cha bajeti uende Mbalawala mimi na wewe…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umeisha.

MHE. PASCHAL I. CHINYELE: ... ukawape majibu ndugu zangu wa Mbalawala na Nala ili waweze…