Contributions by Hon. Edwin Enosy Swalle (4 total)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hotuba hii na ninaomba ku-declare interest kwamba ni Makamu Mwenyekiti wa Wizara hii ya Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Kwanza nimshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Waziri Ridhiwani Kikwete, Naibu wake kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya kwenye hii Wizara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, niwapongeze Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu na Wakuu wa Taasisi mbalimbali chini ya Wizara hii. Ninataka nianze kwa kuchangia eneo muhimu sana hasa eneo la Utawala Bora. Ukisoma taarifa ya Mheshimiwa Waziri kwa sababu ninafanya kazi kwenye hii Kamati, kwenye Taarifa ya Mheshimiwa Waziri imeeleza mambo mengi ya msingi kuhusu Utawala Bora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya eneo ambalo limesemwa ni juu ya kazi nzuri inayofanywa na Taasisi ya TAKUKURU nchini. Ninaomba nirejee takwimu, nimemsikia mdogo wangu Mheshimiwa Ado, amezungumza hapa ameamua kutafuta habari nzuri kaacha taarifa nzuri ya kwenye taarifa ya Mheshimiwa Waziri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma kwenye taarifa kuhusu mapambano ya rushwa, TAKUKURU imeendesha kesi 664 na imeshinda kesi 260, kesi 300 zinaendelea Mahakamani. Kwenye kesi hizo TAKUKURU wameokoa zaidi ya bilioni 102. Pia kwenye taarifa ya Mheshimiwa Waziri TAKUKURU wamepitia miradi mbalimbali ya majimboni kwetu Waheshimiwa Wabunge miradi 885. Katika hiyo miradi, miradi 13 imebainika kuwa na kasoro na TAKUKURU imeokoa zaidi ya trilioni 1.3 kwa ajili ya faida ya Serikali ya walipakodi wa nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hilo halitoshi taarifa imesema uko msemo unasema “Usiboziba ufa utajenga ukuta.” Lakini pia, kuna msemo unasema “Samaki mkunje angali mbichi.” TAKUKURU wamefanya kazi kubwa sana ya kuunda klabu za rushwa za shule ya msingi na sekondari zaidi ya 4,000 nchi nzima ya Tanzania ili kuwaelimisha Watanzania wachukie rushwa nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka nitumie nafasi hii kama kuna jambo Mheshimiwa Rais amelifanya kwa weledi mkubwa ni kuwezesha TAKUKURU iweze kufanya kazi yake vizuri. Ili uone dhamira hiyo, sisi kwenye Kamati tulipitia miradi mbalimbali ukiona miradi ya TAKUKURU inavyojengwa kwa viwango vya mfano utaamini kwamba TAKUKURU ni chombo ambacho kinaisaidia sana hii nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikwambie pia wako watu mahali fulani waliwahi kupuuza uwezo wa polisi kwenye nchi yao. Ninataka nikwambie polisi wasipofanya kazi yao ndiyo utajua umuhimu wa polisi. Kwenye hii nchi yetu TAKUKURU wasingekuwepo na kufanya kazi nzuri wanayoifanya ndiyo ungejua umuhimu wa TAKUKURU hapa nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpe taarifa Mheshimiwa Ado jana kwenye Wizara ya Mipango na Uwekezaji tumesomewa hapa, nchi yetu ya Tanzania kwa hivi sasa inaongoza kwa kuvutia uwekezaji Afrika Mashariki. Kwa muda wa miezi nane Tanzania uwekezaji wamesajili miradi ya uwekezaji 611, tafsiri yake ni kwamba nchi yetu inaaminika na utawala bora unakwenda vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kwenye taarifa ya Mheshimiwa Waziri hapa imesomwa tarehe 31 Machi, juzi tu nchi yetu imeidhinishiwa fedha zaidi ya dola milioni 300 na Benki ya Dunia kwa ajili ya TASAF hii ni kazi nzuri ya Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kama hilo halitoshi, utawala bora maana yake ni nini? Utawala bora una mambo mengi. Juzi hapa Mheshimiwa Waziri wa Bunge, Sera na Uratibu Chief Whip alisema ndani ya Bunge hili akapongeza uteuzi wa Eveline Munisi kuwa Mbunge kwenye hili Bunge kutoka Chama cha NCCR Mageuzi. Hiyo ndiyo maana ya uongozi jumuishi, ndiyo maana ya utawala bora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo lingine kuhusu uwazi. Kwenye taarifa ya Mheshimiwa Waziri hapa imesemwa vizuri sana, sasa hivi miradi yote nchini ili kudhibiti rushwa na ubadhirifu tenda zote zinaombwa kwenye Mfumo wa NeST siyo kwa upendeleo, huo ni uwazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ili kuimarisha uwazi hapa nchini Serikali imeunda Mfumo wa E-Mrejesho. Sasa hivi wananchi wanaruhusiwa kuongea na viongozi wao moja kwa moja kuanzia Waziri Mkuu, Mawaziri, Wakuu wa Mikoa mpaka Wakuu wa Wilaya. Hii ndiyo maana ya utawala bora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo lingine la muhimu sana. Ukifanya tathmini ya kazi ambayo TAKUKURU inafanya kazi ambayo vyombo vingine kama vile Mahakama inafanya, wote wanashuhudia Waheshimiwa Wabunge huu ni mfano muhimu ninaoutoa sasa, juzi wameshuhudia Mahakama ya Rufani imeifungulia CHADEMA kufanya siasa nchini, huu ni utawala bora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hilo halitoshi mama Samia amesema ndani ya Bunge hili, kwamba anataka kurejesha tabasamu kwa Watanzania na amekuja na 4R. Nami nikiwa Mbunge wa Awamu ya Pili humu ndani ninafahamu katika jambo Mheshimiwa Rais amekusudia kulifanya ni kuimarisha Mfumo wa Haki Jinai ambao Mheshimiwa Ado anauzungumzia ndani ya Bunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma kwenye taarifa Mfumo wa Haki Jinai ambao utakuja kuleta mabadiliko ya sheria mbalimbali zitakuja ndani ya Bunge ili kuboresha utawala wa Haki Jinai na Kutenda haki mbalimbali kwa wananchi wake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu kwa Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote ni muhimu sana kwenye hiki kipindi kwa kazi ambayo mama Samia anaifanya kwa nchi hii tuendelee kumuunga mkono, mama anaipenda Tanzania, mama anapenda vyama vyote, mama anampenda kila mtu. Tukimuunga mkono kwenye ndoto aliyonayo, nina uhakika nchi hii tutazidi kwenda mbele vizuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana kwenye taarifa ya Mheshimiwa Waziri hapa, utakuwa shahidi, kwa muda huu wa miaka mitano ya mama Samia Suluhu Hassan hata manunguko ya watumishi maeneo mbalimbali yamepungua sana. Madaraja yamepandishwa, mishahara imepandishwa, tumeona hapa kwenye mpango wa Watumishi Housing, nyumba za watumishi pia zinajengwa kwenye wilaya, halmashauri, mikoa ili kupeleka tabasamu kwa watumishi na Watanzania kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu kama Mjumbe wa Kamati hii ninaomba tuitie moyo Kamati, tuiunge mkono bajeti hii, tuipitishe kwa kishindo ikatekeleze majukumu ya kitaifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, ninataka nimhakikishie Waziri,sisi kama Kamati tumepitia miradi mingi, tumepitia taarifa nyingi za TAKUKURU na mamlaka mbalimbali. Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora mnyonge mnyongeni, haki yake apewe, lakini wizara hii inafanya kazi kubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo...
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Muda wako umekwisha.
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuhitimisha. Ninataka nitoe rai Mheshimiwa Waziri kwamba kazi yako ni njema, tunaliunga mkono Bunge na kwa sababu hii Wizara iko chini ya mama Samia Suluhu Hassan tunamuunga mkono na kumtakia kila la kheri kwa utumishi wa nchi yetu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Wizara ya Katiba na Sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme mwanzoni kabisa kwamba nimeisoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri kwa umakini mkubwa sana, page kwa page na nimevutiwa nayo sana. Baadhi ya mambo mahsusi ambayo Mheshimiwa Waziri ameyasema kwenye hotuba hii, ninaomba niyataje matatu: Moja, anasema Sekta ya Sheria ni mlinzi wa amani, utulivu na usalama wa nchi; Pili, anasema Sekta ya Sheria ni mlinzi wa uwekezaji nchini; na Tatu, anasema sheria siyo kikwazo bali ni daraja la maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mtazamo huu wa hii Wizara unaonesha jinsi ambavyo hii Wizara wamejipanga kuwa sehemu ya kutekeleza Dira 2050. Mheshimiwa Waziri, Dkt. Juma Zuberi Homera, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Naibu Waziri na Katibu Mkuu wa Wizara hii na Naibu wenu hongereni sana kwa kazi nzuri ya Wizara ya Katiba na Sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, baada ya kuwapongeza hivyo, ninaomba pia niwasemee kwa kifupi waajiri wangu toka Jimbo la Lupembe, wananchi wa Jimbo la Lupembe wanaishukuru sana Serikali kwa kupeleka Mahakama ya Mwanzo Tarafa ya Lupembe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, wananchi wangu wa Kata ya Mtwango, Kata ya Kichiwa, Ninga, Igongolo, Ikuna, wanaomba Mahakama ya Mwanzo pale Mtwango. Ninamwomba sana Waziri na ninajua Katibu Mkuu ananisikia, wananchi wa Kata hizi tano muhimu hawana Mahakama ya Mwanzo wanafuata mahakama Njombe mjini na Makambako.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Mahakama ya Mwanzo pale Mtwango ili tuweze kuendeleza ujenzi wa Mji wa Mtwango ambapo tayari kuna kituo cha afya na vitu vingine, tupate huduma ya haki ya sheria pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ninataka nichangie kuhusu eneo la mfumo wa Mahakama nchini. Kwanza kabisa, nitumie nafasi hii kumpongeza sana Jaji Mkuu wa Tanzania, Mheshimiwa Masaju, kwa jinsi ambavyo amekuwa positive sana kwenye reforms za kisheria nchini, kama Wabunge tumekuwa tukimfuatilia namna ambavyo ana kiu ya kuona mabadiliko na mfumo wa sheria ukiwa rafiki kwa wananchi wa Tanzania. Tunamuunga mkono aendelee kuchapa kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa karibuni tumemsikia akisema kwamba ni muhimu mashauri mahakamani yakaisha kwa muda mfupi. Pia, amekuwa akisisitiza umuhimu wa Mahakama kuzingatia matumizi ya tamaduni na mila zetu kama Watanzania. Kama Waafrika, tunamuunga mkono na kwa hili aendelee kuchapa kazi. Pia, Mahakama nzima, majaji na Mahakimu wafuate aina hii ya mtazamo kwenye Mahakama yetu ili kutekeleza dira ya mwaka 2050.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kwenye mfumo wa Mahakama asubuhi imesemwa hapa na ninaunga mkono sana, kwamba Mabaraza ya Ardhi Nchini ni muhimu yakarudi kwenye mfumo rasmi wa mahakama yetu na sababu zipo kadhaa. Sababu ya kwanza, haya mabaraza yameshindwa kuleta tija iliyokusudiwa. Kwa sababu takwimu zinaonyesha 32% ni migogoro ya ardhi, maana yake dhumuni la haya mabaraza halijafikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya yako mbali sana na wananchi, kwa mfano, Mkoa wa Njombe, tunalo Baraza moja la Ardhi Mkoa mzima. Wananchi wa kule Madeke, umbali wa kilomita zaidi ya 120 wanafuata Baraza la Ardhi na Nyumba Wilayani Njombe. Barabara za matope, wananchi wa Ludewa na Wanging'ombe wanafuata Baraza Njombe Mjini. Kwa hiyo, yako mbali na wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu Mabaraza haya pia yamelalamikiwa mara kadhaa kwa ajili ya kesi mbalimbali za wananchi kutofanyiwa kazi vizuri. Kubwa kuliko yote, ipo kanuni ya haki ya asili au tuseme natural justice, kwamba hapa nchini Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya yako chini ya Wizara ya Ardhi, lakini Wizara ya Ardhi ndiyo wanaopima ardhi, ndiyo wanaotoa hati. Sasa, haiwezekani ndani ya hii Wizara tena wakasimamia haya mabaraza. Kwa misingi ya rule against bias, jambo hili haliwezekani! Kwa hiyo ni muhimu haya mabaraza yakarudi kwenye mfumo wa Mahakama ili tutoe haki kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ninataka pia nishauri. Kwa kuwa, tunazo Mahakama za Mwanzo nyingi nchini, ambazo kule chini wako Mahakimu wenye weledi wa degree, lakini pia tumeweka sheria Mawakili wanaruhusiwa kwenda Mahakama za Mwanzo, ninashauri Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, tuanze kuruhusu Mahakama za Mwanzo kusikiliza mashauri ya ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hizi Mahakama za Mwanzo ndiyo zipo karibu na wananchi na Mabaraza ya Ardhi ya Kata tumeshayaondolea mamlaka ya kuamua kesi za ardhi. Kwa hiyo, ni muhimu Mahakama za Mwanzo sasa zikaingia kwenye mfumo wa kusikiliza mashauri ya ardhi nchini ili kusudi mfumo huu uweze kwenda kwenye Mahakama ya Wilaya, Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, niseme kidogo hapa kuhusu Law School of Tanzania. Law School of Tanzania kama ambavyo imesemwa na wengi, iliundwa maalum kuzalisha wasomi wa sheria nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2025 Desemba, Law School au tuseme mawakili walioingia kwenye mfumo wetu wa uwakili walikuwa 774. Katika mawakili 774, mawakili 388 hawajapitia kusoma Law School darasani. Wamepata uwakili kwa njia ya kuomba nje ya kwenda kusoma Law School. Tafsiri yake ni nini? Kama utaratibu huu ukiendelea, tunaenda kuua Law School.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, hii ni alert kwamba watu baada ya kuona Law School ni ngumu, wameamua kutanua goli waweze kufunga magoli kwa urahisi zaidi. Ninaomba Serikali ilete sheria Bungeni, tubadili hii sheria ili watu wakasome Law School tupate mawakili wenye viwango, wenye ubora watakaoweza kufaulu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kabisa, ninataka niseme kidogo sana hapa kuhusu uhuru wa Mahakama. Hapa ninaongelea mahsusi, uhuru wa Mahakama juu ya kuisaidia Mahakama iwe na uwezo wa kuamua mashauri bila kuwa na sheria ambazo zinailazimisha mahakama kutoa adhabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee ninarejea Sheria ya Makosa ya Kujamiiana. Sheria ambayo imelazimisha Mahakama za Tanzania kutoa adhabu kwa washtakiwa wanaotiwa hatiani, kumfunga mtu kifungo cha minimum miaka 30 kwenda juu. Maana yake nini? Hata kama Jaji au hakimu ataona kesi ingefaa kumpunguzia mfungwa adhabu, amefungwa mikono kwenye sheria. Ninaomba Serikali ifike wakati tutunge sheria kuisaidia Mahakama iwe huru kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kwa sababu hii bajeti ni nzuri, ninaiunga mkono kwa asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nami nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu aliyetupa afya na uhai wa kuwemo ndani ya Bunge hili siku ya leo na hasa, Bunge la Kumi na Tatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ninaishukuru sana Serikali. Wahenga walisema “Usione vyaelea, vimeundwa.” Sisi Wabunge wengi kwenye majimbo na mikoa ambako tunatoka, zipo kazi nyingi zimefanywa na Serikali. Hata Jimbo la Lupembe, kwa mfano, ukienda leo, hali ilivyokuwa miaka mitano iliyopita, Jimbo la Lupembe, leo jimbo zima linawaka umeme vijiji vyote 45.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tumepata vitongoji vingine 28, tunaendelea kukamilisha vitongoji vyote kwa ajili ya umeme Jimbo la Lupembe. Hii ni kazi kubwa ya Serikali ya Awamu ya Sita. Ukienda kwenye elimu, madarasa yamejengwa, ukienda kwenye zahanati vituo vya afya hadi kule Ikondo vimejengwa, ambako havijawahi kujengwa tangu kuumbwa kwa dunia hii. Hii ni kazi nzuri ya Chama cha Mapinduzi. Ninaishukuru sana Serikali kwa kazi ambayo inaifanya, kwa ajili ya Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najielekeza kwenye mchango wangu wa siku ya leo, kwenye eneo la Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Sehemu ya kwanza ambayo imesemwa na Wabunge wengi ni kuhusu hali ya barabara nchini. Tumeambiwa kwenye hotuba, Wabunge wengi wamesema na mimi naomba kupaza sauti kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Lupembe. Hali ya barabara za nchi yetu hivi sasa siyo nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Lupembe leo hii kwa mfano, Barabara ya Njombe – Lupembe – Madeke mpaka Mlimba kule Morogoro, nimekuwa naisemea ndani ya Bunge hili kila wakati. Sasa hivi yako maeneo yanaleta shida, magari yanakwama, wananchi hawasafiri vizuri na imeahidiwa takribani miaka 20 sasa. Barabara hii ni muhimu kwa sababu, inaunganisha Mkoa wa Njombe na Mkoa wa Morogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wananchi wa Mkoa wa Morogoro wanategemea Mkoa wa Njombe kwa ajili ya mbao. Bidhaa za majani ya chai, parachichi na mazao mengine mbalimbali. Tukijenga hii barabara itaweka msukumo wa uwekezaji Lupembe na kufanya wananchi wengi wapate ajira na viwanda vingi sana kujengwa Lupembe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali, umefika wakati sasa tujifunge mkanda tuandae mkakati maalum wa kujenga barabara za nchi hii ili kusudi wananchi wetu waweze kuwa na uhakika wa kusafiri kutoka eneo moja kwenda eneo lingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhusu Barabara za TARURA. Hapa nina ushauri maalum kidogo na ninaomba Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, Profesa Shemdoe na Manaibu wako mnisikilize vizuri sana kwenye sehemu hii ya TARURA. Mheshimiwa Rais alimengea wakati fulani, ukisoma kwenye hotuba ya leo hapa TARURA imeongeza bajeti kutoka shilingi bilioni 940 mpaka shilingi trilioni 1.2.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ni habari njema, lakini lipo tatizo kwenye Barabara za TARURA, na hapa ndipo naomba Serikali mnisikilize vizuri. Hizi barabara maeneo mengi tunajenga kila mwaka, barabara hizo hizo. Tunaweka shilingi bilioni moja mwaka huu, shilingi milioni 500 mwakani, mvua ikija inasomba barabara zote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wa nchi yetu alitoa maelekezo kwamba, ni muhimu TARURA mkatafuta teknolojia ya kujenga hizi barabara zikae kwa muda mrefu, ili kusudi tukijenga mwaka huu barabara mwakani tusirudie tena.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa, Profesa ninakuomba sana ukae na wataalamu wako mjifunze teknolojia mpya ya kujenga hizi barabara, ili fedha ya walipakodi isipotee kila mwaka kwa sababu, bila kufanya hivyo ni kama kila mwaka fedha ya wananchi inapotea kwa kusombwa na maji kwenye barabara za TARURA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukienda Jimbo la Lupembe, Barabara pale Mtwango – Welela kwenda Kichiwa, Barabara pale Itunduma – Ibumila – Ikando kwenda Nyombo haipitiki vizuri kwa sababu, barabara hii mwaka 2025 imejengwa, lakini mwaka huu tena imeharibika. Ukienda kule Njinga kwenda Ikondo, mwaka 2025 imejengwa, mwaka huu tena haipitiki, kwa nini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa sababu, tunajenga barabara za tope bila kuwa na teknolojia nzuri, ili hizo barabara ziweze kukaa kwa muda mrefu. Hili Mheshimiwa Waziri ni muhimu sana mlifanyie kazi, ili kusudi hii fedha iwe na thamani, ili kila mwaka tujenge eneo lingine, kwa ajili ya ufanisi wa barabara zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo wananchi wa Lupembe wamenituma kusema kwa niaba yao, ni kuhusu mikopo ya 10%. Ukisoma kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali imetoa mikopo mingi sana, zaidi ya shilingi bilioni 130 zimetolewa, kwa ajili ya mikopo ya vijana, wanawake na wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niliongea wakati fulani hapa ndani ya Bunge, moja ya changamoto kubwa kwenye mikopo hii ya 10% ni hairejeshwi. Ninamshukuru Mungu kwa wananchi wa Mkoa wa Njombe, nimefuatilia Taarifa ya TAMISEMI, Mkoa wa Njombe na Halmashauri ya Njombe DC ni kati ya mikoa ambayo wananchi wake wanaongoza kwa kurejesha mikopo ya 10%. Hongereni sana Mkoa wa Njombe. Watu wa Njombe ni waaminifu sana, lakini maeneo mengi mikopo ya 10% hairejeshwi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu kubwa ya mikopo kutokurejeshwa, na hapa ndipo naomba kushauri, ni huu utaratibu wa kupeana mikopo kwenye vikundi peke yake, hauwezi kuwa na tija. Inawezekanaje unamchukua mtu mmoja mwenye ujuzi wa biashara unasema aunde kikundi na watu watano au kumi, ambao hawajui mambo ya biashara?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mikopo hiyo wanagawana fedha, wanaenda kutumia, lakini ukimpa mkopo mfanyabiashara mmoja mwenye biashara, anayejua biashara, anaweza kuajiri wenzake 50 mpaka 100 ikawa na tija kubwa. Kwa hiyo, ninaiomba Serikali, sheria hii ya mikopo ya 10% ya mwaka 2024 iletwe Bungeni tuifanyie marekebisho, ili mwananchi mmoja mmoja mwenye wazo zuri la biashara, mtu mwenye biashara yake, apate mkopo urejeshwe kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo, tutaendana na Dira yetu ya 2050 ya kusaidia wananchi wetu kuweza kuwa na tija na ajira kwenye maeneo yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, naomba nichangie kuhusu dawa za kulevya. Tumesoma hapo kwenye Taarifa yetu ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu kwamba, watu wa kudhibiti dawa za kulevya wamefanya kazi nzuri sana nchini. Leo hii nchini dawa za kulevya zimedhibitiwa kwa zaidi ya 80%. Ninatumia nafasi hii kuwapongeza sana DCEA na Ofisi ya Waziri Mkuu kwa udhibiti wa jambo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwao ni pamoja na mafanikio kwenye dawa za kulevya. Limetokea tatizo lingine, kuna ongezeko kubwa la bidhaa fake mitaani. Zipo pombe nyingi fake mitaani ambazo watu wetu wanaendelea kunywa na zinaweza kuwa na madhara zaidi kuliko hata cocaine na dawa za kulevya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza Waziri wa Viwanda, ameanza vizuri, washirikiane na Taasisi ya Kudhibiti Dawa za Kulevya wadhibiti uholela wa pombe haramu, pombe fake na bidhaa fake ambazo zinaweza kuathiri afya za wananchi wetu kuliko hata dawa za kulevya. Hili ni jambo muhimu sana kwa Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kwa siku ya leo, Wenyeviti wa Vijiji, Vitongoji na Madiwani, wanaiomba Serikali inapoendelea na mipango yake iangalie uwezekano wa kuona namna ya kuwapa posho watu hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Madiwani, Wabunge pia waliongea wakati fulani hapa, wanakaa vikao siku mbili, siku moja, Waziri Profesa Shemdoe, atoe maelekezo kwa Wakurugenzi kwamba Madiwani wetu wapate muda wa kutosha kukaa vikao kwenye Halmashauri, angalau kwa siku tano hadi siku saba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hatuwezi kuwaongezea mishahara, basi wakae vikao muda wa kutosha wajadili vizuri miradi ya maendeleo kwenye halmashauri ili kuwe na tija, lakini pia waweze kujikimu kama viongozi wetu wa halmashauri. Hali kadhalika kwa vijiji na vitongoji vyetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo Rais wa Awamu ya Pili, Alhaj Ali Hassan Mwinyi aliwahi kutuasa kwamba maisha haya ni hadithi tu. Akasema: "Ewe ndugu yangu, andika hadithi yako vizuri." Ninataka niwaombe viongozi walioko Serikalini, Mawaziri, tuandike hadithi yetu vizuri kwa kupeleka maendeleo kwa wananchi wetu. Asanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo kwa Mwaka wa Fedha 2026/2027
MH. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi nianze kuchangia hotuba hii ya Wizara ya Kilimo ambayo ni hotuba muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, niseme kwamba, nilikuwepo hapa ndani wakati Rais, Samia Suluhu Hassan, anakuja kuhutubia Bunge kwa mara ya kwanza. Nikiwa kama Mbunge wa awamu ya pili, ninaweza kusema kwa ushahidi, Dkt. Samia anawapenda sana wakulima wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata Chama Cha Mapinduzi kinawapenda sana wakulima wa nchi hii. Kwa kiwango ambacho Rais ameongeza bajeti, kutoa ruzuku ya mbolea na kununua mahindi, ni dhahiri Dkt. Samia anawapenda wakulima wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ninatumia nafasi hii pia kumshukuru sana Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Daniel Godfrey Chongolo, kwa hotuba yake nzuri iliyoonesha dhamira ya kweli ya kuwasaidia wakulima wa Tanzania. Ninampongeza pia Mheshimiwa Silinde na wataalam wote wa Wizara hii akiwemo Katibu Mkuu, Ndugu yetu Mweli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongea mambo matatu tu kwa asubuhi ya leo. Jambo la kwanza nianze na ushirika. Nimesoma kwenye hotuba ya Waziri ukurasa wa 117-124, wameongea vizuri kuhusu ushirika, wana mpango wa kuhamasisha wananchi wafungue SACCOS, vikundi viunde SACCOS na kadhalika. Ushauri wangu kwa Serikali, ndugu yangu Dkt. Ndiege ninajua ananisikia vizuri sana. Tatizo kwenye ushirika ni vyama vya ushirika kuwaibia wakulima. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kule Njombe kwa mfano, maeneo mengi vyama vya ushirika vimeibia wakulima fedha. Lupembe wananchi wangu wameibiwa fedha, Makambako ambako Mheshimiwa Waziri ametoka pale na nimsemee yuko hapa. Pale Makambako chama cha ushirika kimekula fedha za wakulima, ukienda Igumila, ukienda Njombe. Ninamwomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo kwenye hotuba hawajasema wana mpango gani wa kuwasaidia wakulima walioibiwa fedha zao kwenye ushirika ziweze kurejeshwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni jambo muhimu sana, waje na huo mpango mahsusi watuambie wakulima hawa kabla ya kuhamasisha kufungua SACCOS zingine, watuambie wananchi ambao hela zao zimeibiwa wanawasaidiaje fedha iweze kurudi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhusu zao la parachichi. Sisi Mkoani Njombe kama wakulima wa zao la parachichi, wananchi wengi wanalima haya matunda. Changamoto kubwa ni juu ya uhifadhi wa mazao ya parachichi. Wananchi wa Lupembe wamenituma, niiombe sana Serikali kwenye mpango wake ambao inakwenda nao watusaidie kujenga cold rooms kwa ajili ya kuhifadhi matunda ya parachichi ili kusudi yaweze kuwa na bei nzuri na yasiuzwe kwa kutupwa kama sehemu ya reject. Hii ni hoja muhimu, jimbo la Lupembe wanaomba kujengewa cold room na hata wananchi wa Makambako kwa Mheshimiwa Waziri wanahitaji cold room pia kwa ajili ya matunda ya parachichi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni zao la chai. Ninaipongeza sana Wizara hii, nimesoma kwenye hotuba, kwa mara ya kwanza zao la chai limeandikwa angalau kwa page nne. Hongera sana kwa Mheshimiwa Waziri, ameandika page nne kujadili zao la chai na hapa ninampongeza sana pia Mkurugenzi wa Bodi ya Chai, dada yangu Beatrice Banzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wameandika mipango humu kwenye hotuba hii kwamba wana mpango wa kulikwamua zao la chai. Ombi langu Mheshimiwa Waziri, wananchi wa Lupembe wamelia kwa muda mrefu kutaka kiwanda chao kirejeshwe. Ninamwomba Mheshimiwa Waziri, wamesema kwenye taarifa hii, wakirudi ofisini baada ya bajeti hii wakarejeshe kiwanda cha wakulima wa Lupembe tuweze kwenda mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, wamesema zao la chai duniani bei imepanda kutoka shilingi 2,450 mpaka shilingi 4,000. Ninataka niiombe sana Serikali, badala ya kujadili kupunguza bei ya chai, tufikirie kuongeza bei ya wakulima wa chai hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine pia kwenye chai, sisi watu wa Mkoa wa Njombe wanaweza wasituelewe, tunaposema kuhusu viwanda vya DL, hatusemi personal. Viwanda hivi vilichukuliwa vikiwa vinafanya kazi, lakini baada ya viwanda vyote vile kuwa vimechukuliwa sasa havifanyi kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma kwenye taarifa kwamba wanakwenda kufanya tathmini. Mheshimiwa Waziri, waende wakafanye tathmini viwanda vya chai, kama wawekezaji hawa wamekiuka masharti, wachukue hatua wapewe watu wengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwa asubuhi hii pia niseme kuhusu pembejeo za wakulima. Wananchi wetu ni kweli wanapata mbolea na mbegu, lakini masoko ya uhakika kwenye mazao wanayovuna, bei ambayo wanalima na bei ambayo wanauza haviendani! Tunaiomba Serikali iwasaidie wakulima wapate bei nzuri ya kuuza mazao yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hoja hizo tatu, ninaunga mkono hoja hii ipite kwa kishindo ili Waziri akafanye kazi yake. Ahsante sana. (Makofi)