MHE. SARA M. ALLY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara nyingi zimekuwa zikiharibika kwenye Jimbo la Mvomero hasa maeneo wanayofanya shughuli za uchimbaji wa madini; kama Kata ya Mvomero, Kata ya Lubungo na maeneo mengine.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza bajeti kwenye maeneo hayo ya barabara ili ziweze kupitika kipindi chote cha shughuli za wananchi wanapofanya shughuli zao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 mpaka sasa imeongeza bajeti ya TARURA kwa zaidi ya takribani mara nne na dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kwamba barabara zetu zote za vijijini na mijini zinapitika ili kuwawezesha wananchi kusafiri na kusafirisha bidhaa zao kwa ufanisi mkubwa zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninaomba nikuhakikishie Mheshimiwa Sara Msafiri, Mbunge wa Jimbo la Mvomero, kwamba Serikali inatambua changamoto na hususani ya Mvomero kwa hali ya hewa mvua nyingi mafuriko na shughuli nyingine za kiuchumi ambazo zinapelekea barabara nyingi kuharibika na majimbo mengine yenye sura ya aina ya Mvomero, Serikali imeweka mpango madhubuti kuhakikisha kwamba barabara hizo zinajengwa na kupitika vizuri. (Makofi)